WANAJESHI WA SUDAN KUSINI WAUKOMBOA MJI WA BENTIU

Taarifa kutoka Sudan Kusini zasema kuwa wanajeshi wa taifa hilo wamechukua udhibiti wa mji wa Bentiu kutoka kwa waasi watiifu kwa aliyekuwa makamu wa Rais wa nchi hiyo Riek Machar.

Msemaji wa kijeshi huko Juba ameiambia BBC kuwa majeshi ya serikali kwa sasa yamechukua usukani wa mji huo.

Amesema kulikuwa na makabiliano madogo kwani waasi walikuwa wakitumia vifaru katika daraja moja nje kidogo ya mji huo.

Hakuna taarifa iliyotolewa kuhusiana na majeruhi.

Maelfu ya raia wamekimbia mji wa Bentiu ambao ni makao makuu ya jimbo lenye utajiri wa mafuta la Unity kabla ya serikali kuukomboa.

Mpatanishi mkuu katika mkutanowa mazungumzo ya kuleta amani huko Ethiopia anasema kuwa ana imani muafaka wa kukomesha vita utaafikiwa karibuni.