MSAFARA WA RAIS KAGAME WAPATA AJALI

Watu wawili wamejeruhiwa katika ajali iliyohusisha mojawapo ya magari ya msafara wa magari ya Rais Paul Kagame nchini Kenya.

Rais Mwenyewe hata hivyo hakujeruhiwa katika ajali hiyo iliyotokea saa mbili asubuhi katika eneo la Limuru eneo la Kati mwa Kenya.

Dereva wa gari hilo alipoteza mwelekeo katika barabara kuu ya Nairobi-Limuru.

Gari hilo hata hivyo lilipoteza mwelekeo likiwa mbali na msafara wenyewe.

Waliojeruhiwa walipelekwa hospitalini.

Rais Kagame alikuwa anarejea mjini Nairobi kutoka katika kongamano la magavana wa Kenya mjini Naivasha katika bonde la ufa.

Kwa sasa Kagame anakutana na Rais Uhuru Kenyatta katika Ikulu ya Rais.

Kagame alialikwa kuhudhuria kongamano la Magavana nchini Kenya kuhusu uongozi mzuri na utawala bora.

Aliwahutubia Magavana hao siku ya Jumatatu na kuwashauri kuwa husisha wananchi katika maamuzi yao ya maendeleo.

Aliwataka kuwahusisha wananchi katika maamuzi ili waweze kujieleza wenyewe kuhusu matatizo na changamoto wanazokabiliwa nazo pamoja na kutafuta suluhisho kwa pamoja.

Mfumo wa serikali za majimbo nchini Kenya ulitokana na katiba mpya ambapo huduma nyingi zilizokuwa zinatolewa na serikali kuu sasa zinapaswa kutolewa na magavana ambao ndio wakuu wa majimbo.

Kumekuwa na maandamanao ya mara kwa mara katika majimbo kutokana na magavana kuanza kuwatoza kodi za ajabu wananchi ili kuweza kupata pesa za maendeleo.