WALIOPORA KUFIKISHWA MAHAKAMANI MALAWI

Kesi ya maafisa wa zamani wa serikali ya Malawi wanaodaiwa kuhusika katika wizi wa mamilioni ya dola kutoka kwa hazina ya serikali inatarajiwa kuanza Jumatano.

Sakata hiyo ilifichuliwa kufuatia jaribio la mauaji dhidi ya mkurugenzi wa bajeti, Paul Mphwiyo - ambaye ameripotiwa alikuwa tayari kufichua kashfa kubwa zaidi.

Hii imetambuliwa kuwa kashfa kubwa zaidi kuwahi kutoke nchini Malawi.

Kashfa hiyo inayojulikana kama Cashgate imevuruga uhusiano mzuri ulioko kati ya Malawi na wafadhili huku raia wakikasirishwa na wizi huo wa mali ya umma.

Kashfa hiyo inaanzia katika eneo la kompyuta ambapo habari za siri kuhusu uwekaji fedha zimehifadhiwa.

Maafisa kadhaa wa Serikali wamekuwa wakitumia udhaifu fulani katika mpango wa uhifadhi wa kompyuta hizo na kuiba mamilioni ya pesa kutoka hazina ya Serikali.

Inadaiwa kuwa huenda Dola Milioni 250 ziliporwa kwa kuwalipa wafanyabiashara kimagendo kwa huduma ambazo hazikutolewa kwa Serikali.

Habari za uporaji huo wa mali ya umma zilifichuka wakati Mkurugenzi wa Bajeti katika Wizara ya Fedha, Paul Mphwiyo, alipopigwa risasi Septemba mwaka 2013.

Tukio hilo lilitekelezwa siku chache kabla ya mfanyakazi wa Cheo cha chini Serikalini alipopatikana na pesa taslimu ya Dola 300,000 katika buti ya gari lake. Pesa nyingi zaidi zilipatikana na kupokonywa wafanyakazi wa umma manyumbani mwao katika buti zamagari yao.

Wafadhili waku wa taifa hilo walikasirishwa pakubwa.

Wamesitisha utoaji wa Dola milioni 150 wakisubiri kufanya uamuzi baada ya uchunguzi katika kashfa hiyo kufanywa. Zaidi ya asilimia 40 ya bajeti yote ya Malawi hutegemea wafadhili.

Hata hivyo kungali kuna matumaini kwa Serikali ya Rais Banda kwa sababu Shirika la Fedha Duniani (IMF) limeamua kutoa kwa Serikali jumla ya Dola Milioni 20, ambazo lilikuwa limezuilia.

Matokeo ya uchunguzi wa awali, uliofanywa kuhusiana na kashfa hiyo, kwa ushirika wa wataalamu kutoka Uingereza, umekamilika lakini matokeo yake hayajatangazwa.

Hadi kufikia sasa polisi wameshikilia magari, nyumba na afisi za washukiwa wote wa kashfa hiyo ya Cashgate.

Kesi ya wawili kati ya watu 70 ambao wameshtakiwa kufikia sasa itakapoanza juma hili, wengi wanatarajia kuwa ukweli zaidi utafichuka mahakamani.