MUGABE ACHAGULIWA MWENYEKITI MPYA AU

Rais mkongwe wa Zimbabwe Robert Mugabe, mwenye umri wa miaka tisini, sasa ameteuliwa kuwa mwenyekiti wa muungano wa Afrika-AU.

Wajumbe walimteuwa Mugabe kwa kauli moja katika mkutano wa AU unaoendelea mjini Addis Ababa-Ethiopia.

Uteuzi wa Mugabe kuongoza muungano huo mkubwa ulio na wanachama zaidi ya arubaini, sasa umeingiza doa ndani ya AU, kwani Mugabe hana uhusiano mzuri na mataifa ya Magharibi, hasa baada ya kukaa uongozini tangu Zimbabwe ilipojipatia uhuru mnamo mwaka wa 80.

HEZBOLLAH WASHAMBULIA JESHI LA ISRAEL

Kundi la wapiganaji wa Washia wa Lebanon walio chini ya vugu vugula Hezbollah, linasema kuwa limetekeleza shambulio dhidi ya msafara wa wanajeshi wa Israeli katika mpaka wa mataifa hayo mawili.

Kwa upande wake, Jeshi la Israeli linasema wanajeshi wake wanne wamejeruhiwa pale kombora lililorushwa kwa kifaru kupiga gari lake la kijeshi karibu na mpaka wa Lebanon.

Taarifa nyingine kutoka kwa Hezbollah zinasema kuwa zaidi yawaisraeli 15 yamkini wameuwawa au kujeruhiwa.

Kundi la Hezbollah linasema kuwa lilikuwa likijibu mashambulio ya angani yaliyofanywa na Israeli yaliyomuua jenerali mmoja wa Iran na wapiganaji kadhaa wa Hezbollah Nchini Syria siku kumi zilizopita.

Israel ilijibu mashambulizi hayo kwa kurusha makombora Kusini mwa Lebanon

Waziri mkuu Benjamin Netanyahu alionya kwamba jeshi la Israel liko tayari kutumia nguvu dhidi ya mashambulizi yoyote kutoka kwa washambuliaji.

VIBOKO WASHAMBULIA WAVUVI

WAKAZI wa kijiji cha Chimati wilayani Butiama mkoani Mara wamekubwa na hofu kubwa baada kuibuka kundi la wanyama wakali aina Viboko ambao wamekuwa wakiwashambulia wavuvi katika eneo hilo na kusabisha mtu mmoja kufariki dunia huku wawili wakijeruhiwa vibaya.

Afisa mtendaji wa kijiji hicho Bw Benedicto Sonenga katika taarifa yake yenye kumbukumbu namba CMT/BT/VOL.01 kwenda kwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Musoma na nakala kuwasilishwa kwa kamanda wa polisi mkoa na mkuu wa mkoa Mara kwa ajili ya msaada, amesema hivi sasa kundi hilo la wanyama hao wakali limekuwa likiwashambulia wavuvi na kusababisha hofu kubwa kwa wananchi.

Katika taarifa hiyo afisa mtendaji huyo wa kijiji amesema kuwa usiku wa juzi wavuvi watatu wakiwa ndani ya mtumbwi katika eneo la kome katika ya ziwa Viktoria Viboko hao walivamia mtumbwi na kuanza kuwashambulia huku wakimng'ata mmoja wao Mtiti Magesa Masige nakutoa utumbo wake nje kabla ya kunyofoa sehemu zake za siri na kuondoka nazo na hivyo kusababisha kifo chake.

Kiongozi huyo wa kijiji amewataja walionusurika katika tukio hilo kuwa ni Bw Mugeta Magembe na Petro Matete wote wakazi wa kijiji cha Chimati huku akimuomba mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Musoma kuchukua hatua za haraka za kudhibiti wanyama hao hatari ambao amedai mbali na kuwa tishio kwa kushambulia wavuvi ndani ya ziwa hilo lakini pia wamekuwa wakivamia makazi ya wananchi na kuharibu pia mazao mbalimbali ya wananchi mashambani.

POLISI YASAMBARATISHA MAANDAMANO YA CUF

Jeshi la polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam leo limetumia mabomu ya machozi kutawanya msafara wa mwenyekiti chama cha Wananchi CUF Profesa Ibrahim Lipumba, uliokuwa ukitokea Temeke jijini DSM kuelekea Mbagala Zakiem, ambako ulikuwa ufanyike mkutano maalum kwa ajili ya kumbukumbu ya wafuasi wa chama hicho waliofariki mwaka 2001 visiwani zanzibar.

Jeshi hilo limetumia nguvu kubwa kuwapiga waandishi wa habari waliokuwa wakitekeleza majukumu yao ambapo mwenyekiti wa taifa wachama Profesa Ibrahim Lipumba na viongozi wengine wamejikuta wakipata kipigo na hatimaye kuwekwa chini ya ulinzi wa polisi.

Awali polisi ilizuia wafuasi hao kufanya maandamano kutokea Temeke kuelekea mbagala na kuwataka waende bila maandamano, Professa Lipumba alitii amri hiyo na kutangaza kuahirisha mkutano huo.

Hali ya sintofahamu ilianzia katika ofisi CUF Temeke pale mwenyekii wao Profesa Lipumba alipowatangazia wafuasi hao kuwa hakutakuwepo na maandamano ya kuelekea katika viwanja wa Zakhem na badala yake atakwenda mwenyewe katika mkutano huo kuwatangazia wananchi ambao tayari walikuwa wameanza kukusanyika katika eneo la mkutano.

Baada ya tangazo hilo safari ikaanza na ndipo mvutano ukaanza baina ya polisi na viongozi wa CUF ambapo baada ya mabishano na majadilino ya muda mrefu safari ikaanza tena kutokea Temeke kuelekea Zakhem.

Baada ya hapo msafara wa Professa Lipumba ulianza kuelekea Mbagala Zakiem lakini walipofika maeneo ya Mtoni kwa Azizi Ally jeshi la Polisi lilizuia msafara huo na likatolewa agizo lingine la kusitishwa kwa msafara huo.

Baada ya majadiliano hayo hali ya hewa ikabadilika ambapo jeshi hilo lilianza kulipua mabomu ya machozi na kuwakamata wafuasi wa chamahicho huku likiwapa kichapo wakati wa kuwapakiza kwenye gari lao akiwemo Professa Lipumba.

Baadhi ya mabomu yaliyokuwa yanarushwa yalidondoka katika makazi ya watu likiwemo darasa dogo la wanafunzi wenye umri usozidi miaka mitano ambapo walionekana wakitokwa machozi huku mwalimu wao Bi Halima Semsela akidai kuna watoto wengine hajui walipokimbilia.

Alitafutwa Kamanda wa Polisi Kanda maalum ya DSM Kamishna Suleiman Kova lakini simu yake imepokelewa na msaidizi wake ambaye amedai kuwa Kamanda yupo kwenye kikao, pia Kamanda wa Polisi wa Polisi Mkoa wa Temeke ACP Kihenya M Kihenya ametafutwa lakini simu yake haikupatikana.

FACEBOOK YATOWEKA KWA DAKIKA 40

Mtandao wa kijamii wa facebook ulikuwa hauingiliki katika maeneo mengi duniani mapema leo kabla ya huduma zake kurudi.

Mamilioni ya watumizi wa mtandao wa facebook walishindwa kuingia katika akaunti zao.

Wateja wake katika mataifa mengine walishindwa hata kutumia hudumu ya Instagram.

Facebook ilisema kuwa wahandisi wake ndio walioababisha tatizo hilo, na kukana madai kwamba kundi moja linalotekeleza uhalifuwa mitandaoni lilihusika.

''Awali watu wengi walikuwa hawawezi kuingia katika akaunti zao za mitandao ya facebook pamoja na huduma ya Instagram'', msemaji wa facebook aliiambia BBC.

''Hili halikuwa shambulizi kutoka kwa watu wengine lakini lilitokea baada ya kufanya mabadiliko ambayo yaliathiri mpangilio wa mfumo wetu''.

Tuliharakisha na kutatua tatizo hilo na sasa huduma zote zimerejelea asilimia 100 kama kawaida

Mitandao hiyo ilitoweka kwa takriban dakika 40 kabla ya kurudi.

Programu ya mtandao unaowaunganisha wapendanao Tinder ambayo hutegemea facebook ili kutoa huduma zake pia iliathiriwa na tataizo hilo.

Kundi moja la uhalifu wa mitandano kwa jina Lizard Squad liliandika ujumbe kwa twitter kuhusu hudumu hiyo kutoweka na kusababisha ripoti kwamba huenda lilihusika.

Kundi hilo limeshtumiwa kwa mashambulizi ya mitandaoni mwishoni mwa mwaka uliopita ambapo michezo ya video ya Sony pamoja na Xbox ilipotea.

WATU WAWILI WAFA KWA KULA UYOGA

WATU wawili wa familia moja wamefariki dunia katika Kijiji cha Masyalele, Wilaya ya Nanyumbu Mkoa wa Mtwara baada ya kula uyoga unaosadikiwa kuwa sumu. Pia wengine wanne walazwa akiwamo mtoto wa miaka mitatu katika kituo cha afya cha Mangaka.

Tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki baada ya mume na mke kufikishwa katika kituo hicho cha afya Januari 24 mwaka huu ambapo walilazwa lakini baada ya muda mfupi walifariki.

Akizungumza na mwandishi wa habari ofisini kwake jana, Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo, Salvatory Chinguile alisema kuwa marehemu hao baada ya kufikisha katika kituo hicho hawakusema ukweli kama wamekula uyoga na baada ya kufanyiwa uchunguzi walikutwa wana malaria kali.

"Baada ya kufika katika kituo cha afya hawakusema kama wamekula uyoga na ndipo tuliwafanyia uchunguzi na kukuta wana malaria kali na kuwaanzishia matibabu lakini walifariki wakati wakiendelea na matibabu hayo," alisema Chinguile.

Dk Chinguile aliwataja marehemu hao kuwa ni Hasani Mtumbele (68) na mkewe Zena Ibrahimu (55). Waliolazwa ni pamoja na Shamila Faina (19), Mohamed Milinje (69), Maimuna Bakari (29) na Keshneti Kazumari (3).

Naye Mkuu wa Wilaya hiyo, Festo Kiswaga amewataka wananchi wa wilaya hiyo kuacha kula uyoga ili kuepukana na madhara ambayo yanaweza kujitokeza pamoja na kusababisha vifo.

"Nawaomba na nashauri wananchi wote waache kula uyoga kwa sasa kwani wanaweza kupata madhara makubwa hata kusababisha vifo kutokana na uyoga mwingi kuwa na sumu," alisema Kiswaga.

Pia alisema kuwa wilaya imepeleka timu ya madaktari watatu kwa ajili ya kuwafanyia uchunguzi wananchi wa eneo hilo ambao walikula uyoga tangu zilipoanza mvua.


Chanzo: Habari Leo

TRAFIKI FEKI ATUPWA JELA MIAKA SITA

ALIYEJIFANYA Askari Polisi wa Usalama Barabarani, James Hassan (54) amehukumiwa kifungo cha miaka sita jela baada ya kupatikana na hatia ya kukutwa na sare za Polisina kujifanya mtumishi wa jeshi hilo.

Aidha, adhabu hiyo ilitokana na makosa mawili ambapo mshitakiwa huyo atatakiwa kutumikia kifungo cha miaka mitatu mitatu kwa kila kosa.

Akisoma hukumu hiyo jana, Hakimu Mkazi Mwandamizi, Hassan Juma wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala, alisema kwamba ametoa adhabu hiyo ambayo haitaenda kwa pamoja, kutokana na mshitakiwa huyo kuwa ni mkosefu mzoefu.

Pia alisema kwamba mahakama hiyo imemtia hatiani kupitia kwa mashahidi watatu wa upande wa mashitaka walioithibitishia mahakama bila ya kuacha shaka.

Kabla ya hukumu, mshitakiwa huyo alidai kwamba kwa kuwa mahakama imemwona kuwa ana hatia, yeye hakufanya kosa hilo na hata ikiwezekana mahakama imuachie huru.

Hata hivyo, mahakama hiyo ilitupilia mbali maombi hayo na badala yake alihukumiwa kifungo hicho. Wakili wa serikali, Florida Weneslaus alidai kuwa mshitakiwa apewe adhabu iwe fundisho kwa wengine.

Katika kumbukumbu za makosa ya nyuma ya mshitakiwa, ilibainika kwamba mshitakiwa huyo alihukumiwa kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la unyang'anyi wa kutumia silaha, katika mahakama yaWilaya ya Isanga, Dodoma na kufungwa katika gereza la Isanga mkoani humo.

Pia mshitakiwa huyo alihukumiwa kifungo cha miaka sita jela kwa kosala kukutwa na sare za Jeshi la Polisi.

Katika barua iliyoandikwa na Mkuu wa Gereza la Keko kwenda kwa Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, iliithibitishia mahakama kwamba mshitakiwa huyo alikuwa na kesi namba 32 ya mwaka 2004 na kwamba mshitakiwa alijiandikisha kwa jina la Ally Kinanda.


Chanzo: Habari Leo

MGANGA WA KIENYEJI ATUPWA JELA MIAKA SABA

MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala, imemhukumu mganga wa kienyeji, Yahaya Michael (34) kifungo cha miaka saba jela baada ya kupatikanana hatia ya wizi wa gari kwa njia ya udanganyifu.

Akisoma hukumu hiyo jana, Hakimu Mkazi Mwandamizi, Hassan Juma alisema kwamba kutokana na mshitakiwa kutoroka chini ya dhamana, atatumikia kifungo hicho mara baada ya kukamatwa.

Alisema kwa kuwa mshitakiwa alitoroka chini ya dhamana, mahakama hiyo ilisikiliza shauri hilo kwa mujibu wa sheria ya makosa ya jinai.

Alisema upande wa mashitaka ulikuwa na mashahidi watatu ambao waliithibitishia mahakama bila ya kuacha shaka.

Ilidaiwa kwamba gari hilo lilipatikana maeneo ya Urambo Tabora huku mshitakiwa huyo akiwa analiendesha.

REAL MADRID KUJENGA KITUO CHA MICHEZO NCHINI

Klabu tajiri duniani, Real Madrid ya Hispania imesaini Hati ya makubaliano na Shirika la hifadhi ya Jamii Tanzania (NSSF) kwa ajili ya kujenga na kuendesha kituo cha michezo kitakacho gharimu Shilingi bilioni 16.

Ujenzi huo utajumuisha Viwanja vitano ya Mpira wa miguu, Mabweni ya Wachezaji na Wageni, Maduka na huduma nyingine muhimu.

Pia patajengwa Uwanja wa Gofu wa Mashimo 18 utakaoambatana na ujenzi wa Nyumba za kisasa katika eneo la Ekari 400 lililopo katika Mji uliopangwa kuwa wa kisasa wa Kigamboni, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.

Makubaliano yalifanyika jijini Dares Salaam muda mchache baada ya maofisa wa Real Madrid, akiwemo mkuu wa vituo vya kulelea wachezaji wa Real Madrid, Rayco Garcia,ambaye wakati wa uchezaji wake alicheza na Ronaldo de Lima, Roberto Carlos na Zinedine Zidane. Kwa sasa ni kocha wa kikosi cha timu ya Real Madrid chini ya miaka 19.

"Tumefurahishwa sana na ubia huu wa kimaendeleo utakaodumu kwa miaka 18 katikakutafuta, kukuza na kuendeleza vipaji nchini Tanzania kwa ajili ya kutafuta kucheza soka la kulipwa barani Ulaya na kwingineko duniani", alisema Garcia.

Kwa mujibu wa mkurugenzi mkuu wa NSSF, Ramadhani Dau, hati ya makubaliano ina sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ni kazi ya Shirika hilo kubwa Tanzania kujenga kituo hicho na sehemu ya pili itakuwa ni ya Real Madrid ikihusisha kuleta makocha, kusimamia mchakato wa kupata vijana chini ya miaka 13, 14, 15, an 16 watakaoingia katika kituo hicho na kusimamia chakula bora.

Pia itahusika na kutafuta Masoko kwa Wachezaji hao baada ya kuwatangaza kupitia Televisheni ya Real Madrid.

Pia Dau alisema uwekezaji huo utatoa fursa kwa Tanzania kupata wachezaji kwa ajili ya kushiriki kucheza kombe la dunia katika miaka ijayo ili kutimiza ndoto ya muda mrefu.

Tanzania imekuwa moja ya kivutio kikubwa barani Afrika kwatimu za Ulaya. Hiki kitakuwa ni Chuo cha pili kujengwa baada ya Klabu ya Sunderland ya Uingereza nayo kuendelea na ujenzi wa kituo kingine.

Hivi karibuni, maofisa wa Klabu ya Arsenal ya Uingereza pia walitua Tanzania kwa ajili ya kutafuta ubia wa kuuza Vifaa vyake vya michezo kama vile Jezi baada ya kugundua kuwa wana wapenzi na mashabiki wengi.

Wengine walioambatana na Garcia ni Francisco Martin, , Juan Jose Milla (makocha) na mkurugenzi wa ufundi Ruben de La Red.

MAMA AUWA WATOTO WAKE WAWILI

(Tunaomba radhi kwa muonekano wa picha kuwa wa kutisha)


Katika hali isiyotegemewa watoto wawili wameuawa na mama yao , Zuhura Steven, anayedhaniwa kuwa anaupungufu wa akili na kufukiwa katika mashimo mawili tofauti, katika nyumba walimokuwa wakiishi, katika Mtaa wa Salimini Kata ya Chemchemu Manispaa ya Tabora.

Wakizungumzia tukio hilo linalodhaniwa kutokea kuanzia asubuhi ya Januari 25,2015, hadi majirani walipogundua tukio hilo usiku jana, Mwenyekiti wa Mtaa wa Barehani pamoja na wananchi walioshuhudia tukio hilo wanasema kuwamchana watoto hao hawakuonekana kama mazoea yao ambapo wamekuwa wakionekana kila siku nyakati za mchana wakicheza.

Jeshi la Polisi mkoani Tabora limethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuwataja marehemu kwa majina ya Mwamvua Mrisho (4) na Soud, (miezi 4) na upelelezi unaendelea pindi utakapokamilika mtuhumiwa atafikishwa Mahakamani.

Chanzo cha tukio hilo bado hakijajulikana na mtuhumiwa yuko mikononi mwa polisi hadi sasa.

RAIS KIKWETE ATEUA MAWAZIRI WAPYA

Rais Jakaya kikwete ametangaza mabadiliko katika baraza lake la mawaziri.

Rais amewateua mawaziri wanane wapya pamoja na manaibu watano.

Tangazo hilo lilifanywa na katibu katika ikulu ya rais balozi Ombeni Sefue.

Mabadiliko hayo yanajumuisha wadhfa wa waziri wa nishati na kawi wa Profesa Muhongo ambaye amejiuzulu mapema leo pamoja na wadhfa wa waziri wa ardhi ambao uliwachwa wazi baada ya kupigwa kalamu kwa Anna Tibaijuka.

Mawaziri hao wawili wanahusishwa na kashfa ya ufisadi ambayo ilimshinikiza mwanasheria mkuu pia kujiuzulu.

Rais Kikwete anatarajiwa kuwaapisha mawaziri hao wapya hii leo katika tangazo litakalorushwa hewani na runinga ya taifa.

Walioteuliwa

1. George Simbachawene- Waziri Nishati

2. Mary Nagu-Waziri wa Nchi mawasiliano na Uratibu

3. Christopher Chiza-Waziri uwezeshaji na Uwekezaji

4. Harson Mwakyembe-Ushirikiano wa afrika mashariki

5. Lukuvi-Ardhi Nyumba na Makazi

6. Steven Wasira-Kilimo chakula na Ushirika

7. Samwel Sitta -Wizara ya Uchukuzi

8. Jenista Muhagama-Sera na uratibu wa Bunge.

MWANAUME MMOJA AUAWA KINYAMA KISHA VIUNGO VYAKE VYACHEMSHWA

(Tunaomba radhi kwa muonekano wa picha kuwa wakutisha)


Kuna tukio moja la mauaji namba ING/IR/30/2015. Mnamo 22/01/2015 majira ya 23:45 hrs huko kijiji cha songambele wilaya ya Mlele, Richard Madirisha, msukuma(31),mkulima, akiwa amelala na make wake ghafla alivamiwa na watu wasiojulikana karibia watano ambapo walivunja mlango na kuingia ndani na kuanza kumkatakata mapanga, kutenganisha kichwa, sehemu za siri kisha kuchemsha viungo hivyo nje ambapo moto ulikuwa unawaka.

Sufuria za kuchemshia viungo hivyo walivichukua ndani ambapo walimtishia mke wa marehemu aitwaye Mekrina Moses, msukuma(25) asipige kelele.

Baada ya kukamilisha zoezi walinawa mikono kwa kutumia sabuni iliyokuwa nyumbani kwa marehemu na kuondoka na simu ya marehemu yenye namba 0783846414.

Taarifa za awali inaonyesha chanzo kulipiza kisasi kwani marehemu alikuwa akiishi kaliua mkoani Tabora na huyo mwanamke alikuwa ni mke halali wa Shija Manyama wa kaliua hivyo marehem alipora.

Kitendo hicho kilimuudhi Shija na kuamua kukata mapanga ng'ombe 7 wa marehemu na ugomvi ukawa unaendelea hadi July 2014 ambapo marehemu alihamia kijiji cha songambele wilaya mlele, na hata hivyo inasemekana vitisho viliendelea kutolewa na shija dhidi ya marehemu kwa njia ya simu, Jitihada za kuwatafuta watuhumiwa zinaendelea.

POLISI ZANZIBAR WAKAMATA MAJAMBAZI WAWILI

Jeshi la polisi Zanzibar kwa kushirikiana na wafanyabiashara wa machinga walioko darajani Zanzibar wamefankiwa kuwakamata majambazi wawili huku kukiwa na taarifa kuwa mmoja amefariki baada ya kutupiana risasi na kusababisha kizaazaa cha aina yake mjini Zanzibar.

Hali hiyo imetokea baada ya polisi kuanza kuwasaka na kuwafuata majambazi hayo ambayo baada ya kuona wamenaswa wakaamua kukimbia na kuingia maeneo ambayo yanatumiwa na wafanyabishara wadogo wadogo maarufu kwa jina la 'dada njoo' Baada ya kuingia katika maeneo hayo, ndipo wafanyabishara hao wakaanza kuwanasa na kuwabana majambazi hayo yaliyokuwa katika gari aina ya Noah yenye namba za usajili ambazo inasemekana ni za bandia.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Mjini Magharibi Muccadam Khamis amesema polisi bado inawasaka wengine ingawa amesema uchunguzi unaendelea na kuthibitisha kuwepo kwa wananchi wanane ambao walipatwa mshtuko na wako hopitali ya Mnazi Mmoja wakipata huduma za matibabu.

Hata hivyo taarifa zilipatikana mjini Zanzibar zinadai kuwa jambazi mojaambaye anajulikana kwa jina la Khmais Mabunduki na ambaye alikuwa anasakwa na polisi kwa muda mrefu ndiye aliyefariki kutoakna na mapigano hayo, huku bado polisi wakiendelea kuwasaka wengine ambao wako katika mtandao mmoja.

TFDA YAFUNGIA DAWA TANO

Mamlaka ya chakula na dawa nchini TFDA imefuta usajili wa dawa za binadamu aina Tano na kuamuru ziondolewe sokoni na vituo vyote vya kutolea huduma za afya mchini kote mara moja kutokana na kubainika kuwa na viambata vinavyosababisha maradhi sugu ikiwemo kiharusi, na wakati mwingine kusababisha vifo.

Dawa zinazotajwa kufutiwa usajiri na kuzuia uingizwaji kuwa ni pamoja na dawa za kutibu maralia ya maji na vidonge aina ya Amodiaquine, dawa za kutibu mafua na kikohozi zamaji, vidonge na kapsulis zenye kiambata cha Fenil Propanolamine nyingine ni dawa ya sindano aina ya Chrolaphenical inayotengenezwa nakiwanda cha Lincoln cha nchini India, dawa za kutibu fungus ya vidonge na kapsuli.

Akitangaza dawa hizo mkurugenzi mkuu mamlaka ya chakula na dawa TFDA Bw. Hiit Sillo amesema hatua hiyo imefikiwa baada ya uchunguzi wa kitaalam wa muda mrefu kwa kutumia mifumo ya ufuatiliaji wa usalama na ubora wa dawa ambao pia unafanya kazi kwa kutumia mtandao wa kimataifa kwa ushirikiano wa shirika la afya duniani WHO.

Aidha TFDA imefanya mabadiliko yamatumizi ya dawa ya maralia ya SP kutumika kama kinga ya maralia kwa wanawake wajawazito tu na kuagiza watengenezaji kubadili machapisho na vifungashio vyake mara moja ambapo mkurugenzi wa dawa TFDA Bw. Mitanga Fimbo pamoja na kufafanua athari anawataka watoa huduma nchini kote kuondoa dawa hizo na kuziteketeza mara moja kabla ya kuanza kwa msako.

Dawa aina Tano zilizofungiwa ni:-Dawa ya kutibu Fungus ya vidonge na Kasuli aina ya Ketoconazole Dawa ya kutibu Malaria ya maji na vidonge aina ya Amodiaquine (Monotherapy)Dawa za kutibu mafua na kikohozi za maji, vidonge na Kapsuli zenye kiambato hai aina ya Phenylpropanlo Amine Dawa ya kuua bakteria ya sindano aina ya Chloramphenicol Sodium Succinate inayotengenezwa na kiwanda cha Lincoln Pharmaceuticals Ltd, India Dawa ya Kuua bakteria ya maji na kapsuli aina ya Cloxacillin.

KAMATI YA ZITTO YAMJIA JUU MBUNGE

KAMATI ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imeiagiza Bodi ya Korosho Tanzania, kuandika barua inayoeleza hatua walizochukua katika kurudisha nyumba iliyouzwakwa Mbunge wa Kibaha Mjini, Silvestry Koka (CCM).

Akitoa agizo hilo, Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe alisema kamati yake haijaridhishwa na namna nyumba hiyo ilivyouzwa.

Zitto aliitaka Bodi hiyo kuhakikisha inapeleka barua yenye taarifa na lazima iifikie kamati leo saa 6, ikieleza mchakato, taratibu na hatua waliyofikia katika kushughulikia suala hilo.

Taarifa ya CAG inaonesha nyumba ya Bodi ya Korosho iliyopo katikati ya jiji la Dar es Salaam, iliuzwa kwaKoka kwa thamani ya Sh milioni 300 na iliyokuwa Bodi ya Kilimo, ambayo kwa sasa haipo.

Pia, Zitto aliiagiza Bodi hiyo kuhakikisha wanatafuta hati za nyumba na viwanja vyake na kila hatua wanayofuatilia watoe taarifa kwa kamati.

Aidha, PAC imeitaka Bodi ya Korosho kuhakikisha mapato ya njeyanayopatikana kutokana na kuuza korosho, wayatumie kuongeza thamani ya zao hilo ikiwamo kufufua viwanda.

KING ABDULLAH WA SAUDI AFARIKI

Taarifa zilizotufikia zinaeleza kuwa mfalme wa Saudi Abdullah bin Abdulaziz amefariki dunia akiwa hospitalini.

Tamko la kifo cha mfalme huyo zilitolewa na kaka wa mfalme huyo aitwaye , Salman,ambaye naye aliwahi kuwa mfalme.

Kabla ya tamko hilo television ya taifa la Saudi lilikatiza matangazo yake na kuweka nyimbo za quraan ,kama ishara ya kifo cha kiongozi wa juu wa ufalme.

King Abdullah, amefariki dunia akiwa na miaka 90, alilazwa hospitalini kwa wiki kadhaa tangu December mwaka wa jana kutokana na maambukizi kwenye njia ya hewa.

Mfalme huyo aliingia madarakanimwaka 2005 lakini alikuwa ni dhaifu mwenye kushambuliwa namaradhi mara kwa mara.

SERIKALI YAJIUZULU NCHINI YEMEN

Mgogoro nchini Yemen umechukua mkondo mwengine alhamisi baada ya ripoti za maafisa kusema kuwa Rais na waziri mkuu pamoja na serikali yao wamejiuzulu.

Hatua hiyo inajiri baada ya serikali hiyo kutoa ombi la kujiuzulu huku kukiwa na sitofahamu kati yake na waasi wa Houthi maafisa wamesema.

Serikali hiyo ilibuniwa mnamo mwezi Novemba kufuatia makubaliano yalioafikiwa na umoja wa mataifa.

Wapiganaji wa Houthi bado wanaendelea kudhibiti mji mkuu wa sanaa mbali na kumteka msadizi mmoja wa rais wiki iliopita.

Walikuwa wamekubali kuondoka katika maeneo muhimu katika kasri ya ikulu ya rais na nyumba ya rais Abdrabbuh Mansour Hadi.

BANGI HALALI KWA MATIBABU JAMAICA

Baraza la mawaziri la Jamaica, limeidhinisha mswada ambao unahalalisha watu kumiliki kiwango kidogo cha Marijuana.

Ina maana kwamba hii ni mara yakwanza kwa jamii ya 'Warastafarian' wanaotumia Bangi kwa sababu za kidini kuweza kuivuta hadharani bila ya kupatikana na hatia.

Mswada huo,pia unatawezesha kuwepo halmashauri itakayokua ikitoa leseni za kupandwa , kuuzwa na kusambazwa kwa Marijuana kwa sababu za kimatibabu.

Lakini uvutaji wa Bangi katika maeneo ya umma haitaruhusiwa.

Mswada huo huenda ukaidhinishwa na baraza la Senate wiki ijayo.

SOMALIA YAPIGA MARUFUKU LUGHA ZA KIGENI

Rais wa Somalia amepiga marufuku ya matumizi ya lugha za kigeni katika ofisi za serikali na kusema kuwa lugha pekee ya mawasiliano katika ofisi hizo ni kisomali.

Rais Hassan Shaykh Mahmud alikuwa akizungumza hayo katika sherehe za maadhimisho ya kutimiza miaka 42 tangu kuanza kutumika kwa lugha ya Kisomali nchini humo ,maadhimisho yaliyofanywa mjini Mogadishu kwa lengo la kutaka kuiimarisha lugha hiyo.

Hata hivyo maadhimisho hayo yalihudhuriwana mamabalozi wanaowakilisha nchi zao nchini humo.

Matumizi ya lugha ya kisomali katika ofisi za serikali yametakiwa kuanza January mosi mwaka huu na kuendelea.

Shughuli zote za kiserikali nchini humo zimetakiwa kuendeshwa katika lugha ya kisomali na si lugha ingine yoyote.

Ruhusa ya matumizi ya lugha za kigeni imetolewa tu wakati wageni kutoka nje ya somalia watakapo kuwa wakihudumiwa.

Hata hivyo waziri wa habari wa taifa hilo,ametilia mkazo kauli hiyo na kudai kwamba January 21 ni siku muhimu sana kwa taifa hilo,na siku hiyo ni kumbu kumbu kwa gazeti la kisomali la kwanza kuchapishwa.

Naye spika wa bunge la Somalia,Muhammad Shaykh Usman Jawari, ambaye pia alitoa kauli yake kwenye maadhimisho hayo,na kusema kwamba ni jambo muhimu kwa jamii ya wasomali kuelewa umuhimu wa lugha yao na kuitaka jamii kuiimarisha lugha hiyo.

Rais Mahmud aliongeza kusema kwamba tarehe 21 January ni siku muhimu kwa wasomali na serikali yao.

BASI LA TAQWA LADAKWA NA MAGENDO

Abiria zaidi ya 60 ambao walikuwa wakisafiri kutoka harare nchini zimbwe kwenda jijini Dar es salaam wamekwama jijini mbeya kwa zaidi ya saa sita,baada ya basi lenye namba za usajili T776 CRNmali ya kampuni ya TAQWA walilokuwa wakisafiria kukamatwa likiwa limebeba bidhaa mbalimbali za magendo zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 39.
Msako wa kushtukiza katika vyombo vya usafiri ambao umefanywa na mamlaka ya chakula na Dawa,TFDA, na mamlaka ya mapato tanzania,TRA, kwa kushirikiana na jeshi la polisi ndio ambao umelinasa basi hilo likiwa limesheheni bidhaa za aina mbalimbali yakiwemo maziwa ya watoto aina ya LACTOGE Nambayo hayajasajiliwa nchini na hivyo kuhatarisha afya na maisha ya watanzania.

Afisa wa forodha wa TRA mbeya, Edward Male, akatumia fursa hiyo kutoa onyo kwa wafanyabiashara na watu wengine wenye tabia ya kufanya biashara ya magendo.

Baada ya basi hilo kushikiliwa kwa muda mrefu, abiria wake wengi wao wakiwa ni raia wa nchi za zambia na zimbabwe ambao walionesha kuwa wachovu wa safari na wenye njaa, nao wakaanza kutoa kilio chao, wakihitaji msaada ili waendelee na safari yao.

Malalamiko hayo yakatua kwenye sikio la mamlaka ya udhibiti wa usafiri wa majini na nchi kavu SUMATRA, ambao ikawabidi kuingilia kati na kuhakikisha abiria wanaendelea na safari yao.

MAKASISI WAPEWA KICHAPO

Makasisi watatu wa kanisa la Baptist nchini Guinea wamechapwa na kisha kutekwa nyara baada ya wenyeji kuwashuku kuwa maafisa wanaohamasisha jamii dhidi ya ugonjwa hatari wa Ebola.

Makasisi hao, walikuwa wametembelea kijiji cha Kabac eneo la Forecariah wakilenga kufukiza dawa ya wadudu kwenye kuta za vyoo za umma na katika sehemu za kuteka maji.

Mwandishi wa BBC anasema kwamba wanakijiji hao punde tu walipowaona, waliwashuku kutaka kueneza ugonjwa wa Ebola katika eneo hilo.

Zaidi ya watu 8,600 wamefariki katika kanda ya Afrika Magharibi kutokana na ugonjwa wa Ebola.

Mapema mwezi huu, wakazi katika eneo la Forecariah walishambulia na kuwaua polisi wawili walioshukiwa kuwa na njama ya kueneza Ebola katika eneo hilo.

Makasisi hao walipewa kichapo cha Mbwa huku magari yao yakiteketezwa.

Baada ya kuwavamia makasisi hao, wakazi walikwenda katika makao ya baraza la mji na kuanza kuyashambulia.

Pia waliteketeza jumba hilo na kuwalazimisha wafanyakazi kukimbilia usalama wao.

Duru zinasema kwamba mfanyakazi mmoja wa baraza la jiji aliuawa ingawa taarifa hii haingeweza kuthibitishwa.

Watu hao walizua vurugu zaidi pale polisi walipowakamata washukiwa wa vurugu hizo.

WAKULIMA WAZIDI VAMIWA NA MADEREVA BODABODA

Hofu imeendelea kutanda kwa wafungaji mkoani Morogoro kufuatia bodaboda kuendelea kuwavamia na kuwapora wafugaji kila wanapoonekana katika mji wa Morogoro kwa madai ya kulipiza kisasi baada ya mkulima mmoja kuuwawa katika bonde la mgongola ambapo wafanyabiashara wafugaji na wanaofanya shughuli za ulinzi wamelazimika kuukimbia mji wa Morogoro na baadhi ya wanafunzi wa vyuo na kurudi majumbani.
Wakizungumza wakiwa porini kujadili hatma ya usalama wa wafugaji hao wakiwemo wanaume kwa wanawake kutoka wilaya za Kilosa na Mvomero wamesema hawakuusika na mgogoro uliosababisha mauaji ya mkulima katika bonde la mgongola na hivyo kuomba serikali kupitia vyombo vya ulinzi na usalama wawasaidie kwani hivi sasa wagonjwa wanalazimika kutibiwa majumbani wanafunzi hawaendi shule kwa kuhofia madereva wa bodaboda.

Nao baadhi ya wafugaji waliojeruhiwa na kuporwa fedha wameeleza jinsi walivyovamiwa na kupigwa kisha kunyanganywa simu na fedha na hivi sasa wanaugulia majumbani na wanashindwa kwenda hospitali kupata matibabu kwa hofu ya kuvamiwa na madereva wa bodaboda huku baadhi ya wanafunzi wafugaji wanaosoma chuo cha St Josefu Morogoro nao wameelezwa kurudi majumbani.

Wakati haya yakitokea jeshi la polisi mkoa wa Morogoro limewafikisha mahakamani madereva wa boda boda 11 waliobainika kuhusika na matukio ya kuvamia wafugaji ambapo wamesomewa mashataka mawili ya kuvamia wafugaji kwanyakati tofauti mbele ya hakimu mkazi Maua Hamduni ambapo washtakiwa wamenyimwa dhamana kwa hofu ya usalama wao na kurudishwa rumande.

MBWANA SAMATTA AFANYA MAJARIBIO CSKA MOSCOW

MSHAMBULIAJI wa kimataifa waTanzania, Mbwana Samatta, amezidi kugeuka lulu kwa timu za Ulaya baada ya matajiri wa Urusi, CSKA Moscow nao kuonyesha nia ya kumsajili katika dirisha dogo linalomalizia usajili.

Samatta aliyeondoka nchini mwishoni mwa wiki kuelekea Hispania kufanya mazungumzo na moja ya timu ya huko inayoshiriki Ligi Kuu ya Hispania'La Liga', sasa amekutana na zali jingine nchini humo baada ya CSKA nayo kumfukuzia.

Mtoa habari wetu aliyekaribu na Samatta amelipasha MTANZANIA kuwa CSKA imeridhishwa na kiwango cha Samatta na inataka kumsajili kwa ajili ya kuimarisha kikosi chao kwenye mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Urusi.

"CSKA kwa sasa ipo Hispania kwa ajili ya kambi ya mazoezi kujiandaa na mzunguko wa pili wa ligi yao. Walikuwa wanamfuatilia kwa muda mrefu hivyo wanaona hivi sasa ni muda sahihi kwao wa kumsajili,"alieleza.

Mbali na timu kutoka Hispania na Urusi zinazomwania, chanzo hicho kilieleza kuwa Samatta anatakiwa na timu nyingine za Italia na Uswisi, huku timu mbili kati ya hizo nne kutoka mataifa hayo zikiwa ni washiriki wakubwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kila mwaka.

"Watanzania wasiwe na wasiwasi, taarifa njema ya Samatta inakuja muda si mrefu na itajulikana anakwenda Urusi, Hispania, Uswisi au Italia," alieleza.

"Kwa sasa yupo Hispania na janaalitarajia kuanza mazoezi na moja ya timu hizo, watamuangalia mara ya mwisho kabla ya mazungumzo ya pande zote kuanza kisha kufanyiwa vipimo vya afya na kusajiliwa rasmi."

CSKA iliyotolewa kwenye hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu huu ikiwa na Bayern Munich, AS Roma na Manchester City (Kundi E), kwa sasa inashika nafasi ya pili katikaLigi Kuu Urusi kwa pointi 34, huku Zenit yenye pointi 41 ikiwa kileleni.

Kama Samatta atafanikiwa kujiunga na matajiri hao wa Urusi, anaweza kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao na kuwafikia wachezaji wengine wa Afrika Mashariki kutoka Kenya, Mackdonald Mariga (wakati akiwa Inter Milan) na Victor Wanyama (wakati akiwa Celtic).
Samatta alijiunga na TP Mazembe akitokea Simba mwaka 2011, kwa sasa amebakisha mkataba wa mwaka mmoja ndani ya timu hiyo inayomilikiwa na mfanyabiashara Moise Katumbi.

Chanzo: Mtanzania

WINGU ZITO KURA YA MAONI YA KATIBA

Mchakato wa Katiba Mpya, hatua ya Kura ya Maoni umegubikwa na wingu zito kutokana na kuibuka utata na ukiukwaji wa sheria.

Wakati hali ikiwa hivyo, jana Ofisi ya Rais, Ikulu iliibuka na kutoa ufafanuzi kuwa Rais Jakaya Kikwete hajakiuka Sheriaya Kura ya Maoni kama ilivyodaiwa na baadhi ya vyombo vya habari hivi karibuni.

Juzi, Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba alisema kuna mwingiliano unaoleta mkanganyiko katika mchakato wa kuboresha Daftari la Wapiga kura na Sheria ya Kura ya Maoni.

Jaji Warioba alisema sheria inaweka utaratibu maalumu wa mchakato wa kura ya maoni ambao hautaendana na ratiba ya uandikishwaji katika daftari hilo.

Alisema Sheria Kura ya Maoni Na. 3 ya mwaka 2014 inasema wananchi wanatakiwa kupewa elimu ya kura ya maoni kwa miezi miwili na mwezi mmoja wa kampeni lakini hadi sasa, hakuna ratiba inayoeleweka, jambo ambalo alisema linaleta mwingiliano.

"Hii ni Januari, kama watafuata sheria na kuanza kutoa elimu kwa kipindi cha miezi miwili, ina maana itakuwa ni Aprili na Mei, ukijumlisha mwezi mmoja wa kampeni ambao ni Juni ina maana kura itapigwa Julai. Ikumbukwe kuwa mwezi huo mbio za uchaguzi zitakuwa zimepamba moto," alisema.

Mkanganyiko huo umeibua maswali kutoka kwa wanasiasa, wanasheria na wanaharakati wakisema hali hiyo inaweza kuathiri kura ya maoni ambayo imepangwa kufanyika Aprili 30.

Kwa upande mwingine, Mbungewa Ubungo (Chadema), John Mnyika amewasilisha hoja binafsi bungeni kuhusu udhaifu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ili ijadiliwe na kutoa maazimio kutokana na kutokuwapo uwezekano wa kufanyika kura ya maoni Aprili 30.


Kauli ya Ikulu

Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salvatory Rweyemamu alisema katika mchakato huo, Rais Kikwete alifuata taratibu zote zilizopo katika sheria hiyo, ikiwa ni pamoja na kutangaza katika Gazeti la Serikali tarehe ya kuanza kwa upigaji wa kura hiyo.

"Sheria inasema Rais atatangaza tarehe hiyo wiki mbili baada ya kupokea Katiba Inayopendekezwa na alitekeleza hilo na baadaye alieleza jinsi ambavyo Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) itakavyosimamia suala hilo," alisema.

Katika hotuba yake kwa wazee wa Dodoma Novemba mwaka jana, Rais Kikwete alisema, "Ninaomba Watanzania wenzangu tuzingatie mamlaka ya Sheria ya Kura ya Maoni ambayo imeelekeza vizuri lini kura ya maoni itapigwa, lini kampeni zitafanyika na lini wadau watatoa elimu, naomba tuwe na subira. Tukizingatia sheria hii hakuna ugomvi," alisema Rais Kikwete.

Alisema licha ya sheria kuruhusu kampeni kufanyika ndani ya siku 60 kabla ya kura za maoni, kwa mamlaka yake yakiuongozi, kura na kampeni vitafanyika ndani ya siku 30 tu.

"Kampeni zitaanza Machi 30 na kumalizika Aprili 29 ikiwa ni siku moja kabla ya kupiga kura ya maoni. Muda huo ndiyo utakuwa wa kufanya hivyo," alisema Rais Kikwete.


Hoja ya Mnyika

Mbunge huyo wa Ubungo alisema mpaka sasa Nec ilitakiwa iwe imetangaza ratiba ya uboreshaji wa daftari la kudumu la wapigakura lakini haijafanya hivyo, pia Sheria ya Kura ya Maoni inasema kabla yakufanyika kwa kura hiyo kutakuwa na miezi miwili ya kutoa elimu ambayo haitatosha.

"Hakuna haja ya kuuharakisha mchakato huu kwani unaweza kufanyika baada ya Uchaguzi Mkuu, unajua baada ya mjadala,Bunge litakuja na maazimio ambayo yatakuwa suluhisho la mchakato huu unaoharakishwa na chama tawala."

Mnyika ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema (Bara) alisema; "Hata Rais Kikwete anatakiwa kutengua kauli yake kuwa kura ya maoni itafanyika Aprili 30 kwani hali ilivyo hakuna uwezekano wa kufanyika."

Akifafanua baadaye, Mnyika alisema anazo taarifa za ndani ya Nec kuwa vifaa vinavyotakiwa havijakamilika na Serikali haijatoa fedha za kutosha na ndiyo sababu haijatangaza ratiba ya uboreshaji daftari.

Alisema kwa muda uliotangazwa kati ya Februari 15 na Machi 15 kufanya uboreshaji huo, hauwezekani kwa kuwa hakutakuwa na muda wa kuhakiki daftari hilo kabla ya kura ya maoni.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Nec, Julius Malaba alipoulizwa alisema atazungumzia suala hilo leo.


Msimamo wa Makamba

Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba akizungumzia suala hilo alisema; "Kama tukijipanga vizuri kwa Tume na Serikali tunaweza kufanikiwa na hakuna sababu ya kuharakisha kitu.Katiba itapata uhalali kama mchakato wa kuipitisha utakuwahalali."


Wanasheria waponda

Wanasheria mbalimbali wamesema Sheria ya Kura ya Maoni 2013, ina upungufu mkubwa na inaweza kuathiri Wazanzibari wengi kutoshiriki katika upigaji kura ya maoni.

Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu alisema miongoni mwa udhaifu wa sheria ni pamoja na mwingiliano wa Sheria ya Kura ya Maoni ya 2013 na Sheria ya Kura ya Maoni ya 2010 ya Zanzibar.

Alisema katika utaratibu wa kupatikana wapiga kura, kila upande wa Muungano utatumia daftari lake kuwasajili.

"Kwa upande wa Bara kuna daftari linaloandaliwa lakini kwa upande wa sheria ya kura ya Zanzibar ya 2010, ili Mzanzibari atambuliwe na kusajiliwa kwenye daftari la wapigakura ni lazima awe ni mkazi aliyeishi Zanzibar kwa miaka isiyopungua mitatu," alisema na kuongeza:
"Kutokana na sheria hiyo, kuna Wazanzibari wengi ambao wanaishi Bara kwa muda mrefu ambao hawatakuwa na sifa za kuandikishwa kwenye daftari hilo. Nilitoa hoja hiyo bungeni lakini wabunge wa CCM walikataa kwa kuhofia Wazanzibari wakipata nafasi ya kuandikishwa, wataikataa Katiba hiyo.

"Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), Deus Kibamba alisema mbali ya udhaifu huo alioutaja Lissu, mpaka sasa hakuna dalili zozote za kufanyika kura ya maoni kutokana na muda uliobakia.

Alisema katika tathmini yake, hatua zote za maandalizi ya tukio hilo zitakamilika Mei, kinyume na tarehe iliyopangwa na Serikali.

"Mpaka sasa haijulikani daftari kama litakamilika kutokana na muda uliopangwa na ukosefu wa fedha kwa Tume, Pili hatua ya kampeni na maandalizi mengine yanaweza kukamilika Mei," alisema Kibamba.

Awali, Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema Nec haitaweza kukamilisha uandikishaji kabla ya Aprili 30.

"Tulikutana kwenye kikao cha TDC ambacho kilihusisha viongozi wote wa vyama na Jaji Lubuva alikuwapo, aliahidi kutimiza ahadi hiyo lakini mpaka sasa hajapata fedha za kununulia vifaa vingine vilivyobakia," alisema Nyambabe.

Mashine za BVR zinazohitajika ni 7,750 na zilizopatikana ni 250 tu, vituo vya kuandikishia viko 40,500 nchi nzima na Watanzania wanaotarajiwa ni milioni 23, kwa hivyo hakuna uwezekano wa kufanikiwa shughuli hiyo kwa mwaka huu."

Chanzo: Mwananchi

OBAMA ATAKA MGAO SAWA WA RASILIMALI

Rais wa Marekani Barak Obama, amesema Marekani inafanya mabadiliko ya kiuchumi na kijamii baada ya miaka mingi ya kujirudia kwa mdororo wa uchumi na vita, huku uchumi ukiongeza ajira kwa kasi kubwa kuliko wakati wowote tangu mwaka 1999.

Pia amesema Wamarekani wengi zaidi wana bima za afya kuliko wakati wowote kabla ya hapo.

Akihutubia taifa kupitia baraza la Congress lenye wajumbe wengi kutoka chama cha Republican, Rais Obama ametumia hotuba hiyo kutangaza mpango wa kujenga uchumi wa kati kwa wananchi wote wa Marekani, ambapo wananchi wa kipato cha chini watapata huduma za afya na elimu kwa gharama nafuu.

Rais Obama ametangaza hatua za kusaidia familia za wafanyakazi kunufaika kutokana na kukua kwa uchumi.

Mkakati wa Bwana Obama anaouelezea kama uchumi wa daraja la kati, unahusisha kupandisha kodi kwa matajiri.

Hotuba ya Rais Obama ilibeba mapendekezo kuhusu kodi, vyuo vya jamii, huduma za internet, usalama katika mtandao wa komputa na likizo ya ugonjwa.

Bwana Obama amesema hali ya kutoka katika mdororo wa uchumi imetoa fursa ya kuongezeka kwa kipato na fursa kwa kila mtu.

Amesema uchumi wa daraja la kati ni wazo kwamba nchi hiyo inafanya vizuri kabisa wakati kila mtu anapata haki katika mapato na kila mtu anatendewa haki kama ilivyoanishwa katika sheria za nchi hiyo.

Mpango wake wa kuongeza kodi kufikia dola bilioni 320 katika kipindi cha zaidi ya miaka kumi nipamoja na kuziba mianya ya kukwepa kodi kwa wenye vipato vikubwa, ambapo matajiri wakubwa watalipa kodi ya kukua kwa mtaji kutoka asilimia 23.8% hadi asilimia 28%.

MZUNGUKO WA KWANZA WA AFCON WATAWALIWA NA SARE, MZUNGUKO WA PILI KUANZA LEO

Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, Afcon zinazoendelea nchini Equatorial Guinea zilikamilisha mzunguko wa kwanza kwa timu zote 16 ambapoza kundi D zilicheza Jumanne usiku.

Ambroise Oyongo aliifungia goli lake la kwanza timu yake ya Cameroon katika dakika ya 84 ilipopambana na Mali katika mchezo wao wa kundi D uliomalizika kwa sare ya bao 1-1.

Oyongo mlinzi wa kulia aliingia katika eneo la penalti na kupokea pasi kutoka kwa Raoul Loe kabla ya kutumbukiza mpira kimiani kwa umakini mkubwa akiwa karibu na lango la Mali.

Naye Sambou Yatabare aliiwezesha Mali kuongoza mpambano huo alipopachika goli katika dakika ya 71 ya mchezo baada ya kufunga kwa kiki ya karibu akiwa ndani ya eneo la hatari.

Yatabare alifikiria kuwa ameshinda katika dakika za mwisho wakati alipotumbukiza mpira kwa kichwa langoni mwa Cameroon, lakini kibendera kilikuwa juu kuashiria kuwa tayari alikuwa ameotea.

Mali ilicheza vizuri kipindi cha kwanza kwa kupata nafasi kadha za kufunga magoli kwa kiungo wake Bakary Sako kujaribu mara mbili kutumbukiza mpira kimiani, huku akikataliwa na mlinda mlango wa Cameroon Fabrice Ondoa.

Katika mchezo wa awali wa kundi D, Ivory Coast iliambulia sare ya goli 1-1 dhidi ya Guinea. Ivory Coast ilipigana ili kupata sare hiyo, licha ya mshambuliaji wake hatari Gervinho kutolewa nje kwakadi nyekundu, mapema kipindi cha pili.

Iliwachukua Guinea dakika 36 kuongoza mtanange huo wakati Mohamed Yattara alipofunga kutokana na makosa ya mawasiliano ya walinzi wa Ivory Coast.

Gervinho, mshambuliaji wa zamani wa timu ya Arsenal, ambaye aling'ara katika mchezo huo huku moja ya mikwaju yake ikigonga mwamba wa goli la wapinzani wao, alitolewa nje ya dimba kwa kadi nyekundu katika dakika ya 58 baada ya kumpiga usoni Naby Keita. Gervinho kwa hakika alikuwa ndiye mchezaji bora kuliko wote katika mchezo huo, huku wachezaji wenzake wa timu ya Ivory Coast wakishindwa kuonyesha uwezo wao uliowapa majina makubwa katika timu zao za Ulaya kama vile Yaya Toure, ambaye alibadilishwa dakika ya 86 akitoa nafasi kwa Doukoure.

Ivory Coast ndio waliokuwa wakipewa nafasi kubwa ya kushinda mechi hiyo kutokana nakusheheni wachezaji wenye vipaji kama vile Wilfried Bony, ambaye amejiunga na Manchester City kwa kitita cha pauni milioni 28(£28).
Bony alitarajiwa kushirikiana na Yaya Toure na Gervinho katika kuipatia ushindi timu yao, lakini haikuwa hivyo.

Kwa upande wake Guinea ilionyesha uwezo ulioiwezesha kufika fainali hizi za kombe la mataifa ya Afrika, licha ya kucheza mechi zao za kufuzu nje ya uwanja wao wa nyumbani kutokana na ugonjwa wa Ebola kuikumba nchi yao.

Michezo ya mzunguko wa pili inaanza leo kwa timu za kundi A. Wenyeji Equatorial Guinea yenyepointi moja itavaana na Burkina Faso isiyo na pointi katika mchezo wa kwanza kabla ya Gabon inayoongoza kundi hilo kwa kujikusanyia pointi tatu kupepetana na Congo katika mchezo wa pili wa kundi A.

KIJANA APEWA URAIA KWA USHUJAA

Mwanamume mmoja mwenye asili ya nchini Mali ambaye aliwaficha wauza maduka katika duka kubwa maarufu kama supermarket mjini Paris wakati wa shambulio la kigaidi lililotekelezwa na watu wanaodhaniwa wapiganaji wa kiislamu amepewa hati halali ya ukaazi na kuwa raia halali wa Ufaransa.

Kwa pamoja waziri mkuu wa Ufaransa Manuel Valls na waziri wa mambo ya ndani Bernard Cazeneuve walizungumza katika karamu ya kumpongeza na kumshukuru Lassana Bathily kwa ushujaa wake kwa niaba ya taifa lake.

Kijana huyo ana umri wa miaka ishirini na minne, na kazi aifanyayo ni muuzaji msaidizi katika supermarket hiyo,ambaye alifanya kazi kubwa ya kuwaongoza na kuwaficha katika eneo la juu la chumba baridi cha kuhifadhia bidhaa na kisha akazima taa za duka hilo kubwa,kisha akawapigia polisi simu kwa msaada wakati walipovamiwa.

Baada ya tukio hilo, likapitishwa azimio aitwe apewe uraia wa nchihiyo ya Ufaransa ,hata hivyo inaelezwa kwamba Bathily ameishi nchini humo kwa miaka tisa sasa na alikuwa ameshaomba ridhaa ya kuwa raia halali wa nchi hiyo mwaka wa jana.

Wakati wa uvamizi huo, Amedy Coulibaly,aliwaua watu wane wenye asili ya Uyahudi katika duka hilo kubwa kabla hajapigwa risasi na polisi na kufa.

HALI MBAYA YA HEWA YAIKABILI ZAMBIA

Matokeo ya uchaguzi mkuu wa Zambia uliofanyika jana yatatangazwa kama ilivyopangwa awali.

Hata hivyo kutangazwa kwa matokeo hayo kunakabiliwa na changamoto mbalimbali kutokana na baadhi ya vituo vya kupigia kura kushindwa kupiga kura jana, na hivyo kufanyika leo.

Vituo hamsini na moja vitapiga kura hii leo na sababu kubwa ni mvua kubwa iliyo nyesha nchi yote ya Zambia ,hali mbaya ya hewa na kucheleweshwa kwa karatasi za kupigia kura ni sababu zilizotajwa kusababisha wananchi wa Zambia kutopiga kura na leo wapewe haki hiyo.

Hali mbaya ya hewa pia huenda ikasababisha hata matokeo ya uchaguzi kutolewa kama ilivyosemwa awali,naye Rafael Phiri, msemaji wa tume ya uchaguzi ya Zambia amethibitisha kuwa endapo yatachelewa sana haitazidi tarehe ishirini na nne mwezi huu.

ATUPWA JELA MAISHA KWA KULAWITI

Kijana mmoja aitwaye Michael Edward (25) mkazi wa Mtaa wa Mji wa Zamani, Mkoa wa Katavi amehukumiwa kifungo cha maisha jela baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka na kumlawiti mtoto wa kiume mwenye umri wa miaka saba.

Hukumu hiyo iliyovuta hisia za watu wengi mjini Mpanda, ilitolewa na Hakimu mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mpanda, Chiganga Ntengwa baada ya Mahakama kuridhika na ushahidi uliotolewa mahakamani hapo wa pande zote mbili.

Awali, akisoma maelezo ya upande wa mashtaka Mwendesha Mashtaka, Kulwa Sikwesa alidai mahakamani hapo kuwa, mshtakiwa alitenda kosa hilo Oktoba 9, 2014, saa 12 jioni katika eneo la Mji wa Zamani.

Alisema siku hiyo ya tukio mshtakiwa alikutana na mtoto huyo njiani akielekea nyumbani kwaondipo alipomshika mkonona kwenda naye kwenye pagala la nyumba katika mtaa huo.

Mwendesha mashtaka huyo aliieleza Mahakama hiyo kuwa, baada ya kuingia naye ndani mshtakiwa alitoa kisu na kuchoma kwenye ubao aliokuwa amemshikisha mtoto huyo ikiwa ni ishara ya kumtishia kisha alimwambia endapo atakataa kulawitiwa au akipiga kelele atamuua.

Sikwesa alidai baada ya vitisho hivyo ndipo mshtakiwa alipomvua nguo mtoto huyo na yeye suruali na kutoa sehemu zake za siri na kuupaka mate na kisha kuanza kumlawiti mtoto huyo kwa nguvu.

Alidai baada ya kumlawiti alimtishia kutotoa siri hiyo lakini mtoto huyo baada ya kufika kwa wazazi wake alilazimika kuwaambia kutokana na maumivu aliyokuwa nayo na ndipo walipotoa taarifa Polisi kabla ya kukamatwa.

WAFUKUA NA KUBEBA MWILI WA MAREHEMU NA KUTOKOMEA NAO

Watu wasiofahamika wamefukua kabuli na kubeba mwili wa marehemu aliyekuwa amezikwa kwenye makaburi ya Isanjandugu Tarafa ya Nsimbo Wilaya ya Mlele Mkoani Katavi kwa kile kinachodaiwa kuwa ni imani za kishirikina Kwa mujibu wa Diwani wa Kata ya Nsimbo Michael Kasanga(CCM) alisema tukio hilo la imani za kishilikina lilitokea hapo juzi kwenye makaburi ya Isanjandugu Tarafa ya Nsimbo.

Alisema kabuli la marehemu huyo ambalo lilifukuliwa na watu wasiojulikana liligunduliwa hapo juzi na wananchi wawili waliokuwa wanakwenda shambani ambao walipita jirani na makabuli hayo na kuona kabuli hilo limefukuliwa.

Diwani Kasanga alieleza baada ya wananchi hao wawili kuona kabuli hilo limefukuliwa walishitushwa na hari hiyo na iliwalazimu kurudi kijijini na kutoa taarifa kwa uongozi wa serikali ya kijiji.

Alisema baada ya viongozi wa Kijiji hicho kupata taarifa hiyo waliongozana na baadhi ya wananchi kwenda kwenye maeneo hayo ya makaburi ya Kijiji hicho.

Baada ya kufika kwenye eneo hilo la kabuli hilo walikuta limefukuliwa na watu ambao hawajafamika huku mabaki ya mwili wa marehemu huyo yakiwa yamebebwa kwa kile kinachoonekana ni imani za kishirikina.

Alisema kabuli hilo lilishindwa kufahamika jina la marehemu aliyekuwa amezikwa kwenye kabuli hilo kutona na kile kilichoonekana kuwa kabuli hilo lilikuwa ni la muda mrefu.

Diwani Kasanga alifafanua kuwa imekuwa ni tabia ya muda mrefu kwa wananchi wa Kijiji hicho kuwa na tabia ya kwenda kwenye makabuli hayo mida ya usiku na kuoga dawa za kienyeji juu ya makabuli kwa imani za kishilikina

Alisema anatowa wito kwa wananchi wa Kijiji hicho kuacha tabia hiyo ya kuchezea kwenye makabuli na kuogea dawa kwani tabia hiyo ya imani potofu sio nzuri kwenye jamii.

WATU WATANO WAJERUHIWA NA BOMU

WAKAZI watano wa kitongoji cha Mafuriko Amboni kilichopo jijini Tanga wamejeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za mwili baada ya kurushiwa bomu la kutupwa kwa mkono na mtu asiyejulikana wakati walipokuwa wakitazama mpira kwenye banda la wazi.

Majeruhi hao ni Hassani Abdallah (72) ambaye amevunjika mguu wa kulia na kupata madhara makubwa kifuani na sasa amelazwa katika hospitali ya mkoa ya Bombo.

Wengine ni Rashid Ally (45), Mrisho Abdi (29), Juma Mtoo (15) na Abdul Ismail (19) ambao waliumia sehemu mbalimbali za mwili lakini baada ya kufikishwa Bombo wamepatiwa matibabu na kuruhusiwa kurudi nyumbani.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Frasser Kashai amethibitisha tukio hilo na kusema limetokea Januari 15 mwaka huu saa 3:00 usiku huko Mafuriko wakati waathirika hao walipokuwa ndani ya banda moja la kuonesha video.

"Ni kweli jana usiku huko Amboni Mafuriko katika kata ya Chumbageni kulitokea mlipuko wa kitu kinachodhaniwa kuwa ni bomu", alisema.

Aidha aliongeza, "Bomu hilo lilirushwa majira ya saa 3:00 usiku kwenye banda la wazi la kuonyesha video ambalo ni mali ya Evarist Kingazi (82) na kusababisha majeruhi watano", alisema.

Alisema uchunguzi wao wa awali umebaini kwamba bomu hilo ni la kutengenezwa kienyeji kwa sababu askari waliofika eneo la tukio walifanikiwa kuokota mabaki yake ambayo yamejumuisha vipande kadhaa vya nondo na vibati vidogo vidogo.

Kamanda Kashai alisema mkazi mmoja wa eneo hilo, Ally Rashid (25) anashikiliwa na Polisi kwa mahojiano maalumu kuhusiana na tukio hilo.

Chanzo: Habari leo

WATUHUMIWA WATATU WA MAUAJI WAUAWA NA WANANCHI

WAKAZI wa kijiji cha Burunde kata ya Karitu wilayani Nzega mkoani Tabora, wamewapiga, kuwaua na kuwachoma moto watu watatu kwa tuhuma za kushiriki kumuua Helena Abel na kumjeruhi mume wake, Said Msoma.

Akizungumza na waandishi wa habari Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Tabora, Juma Bwile alisematukio hilo limetokea Januari 15 mwaka huu.

Alisema kuwa Januari 12 mwaka huu Helena Abel na mume wake Said Msoma walivamiwa katika tukio hilo Helena aliuawa na Said Msoma alifanikiwa kumjeruhi mmoja wa wahalifu hao ambaye alikimbia.

Kamanda Juma alisema kuwa wananchi hao walifanya doria na kumkamata mhalifu huyo aliyejeruhiwa ambaye anaitwa Mainda Mahila na kuanza kumhoji kuhusika na mauaji hayo na kukiri kufanya hivyo.

Bwile alisema kuwa mtuhumiwa huyo aliwaeleza wananchi hao kuwa mauaji hayo alifanya kwa kuagizwa na Mama Zainabu Hamis pamoja namtoto wake aliyefahamika kwa jina la Zena Yasoda.

Wananchi hao waliwapata watuhumiwa hao wawili kisha kuanza kuwapiga hadi kufa na baadaye kuwachoma moto.

Wakati huo huo mkazi mmoja wa kijiji cha Muhugi kata ya Muhugi wilayani hapa Chenge Kasinki (75) aliuawa na watu wasiofahamika baada ya kuvamiwa nyumbani kwake.

WATANZANIA WANYONGWA KWA MIHADARATI

Kasisi mmoja raia wa Australia amefichua na kuthibitisha kuwa kuna idadi kubwa ya wafungwa wenye asili ya Afrika katika magereza yaHong Kong, wengi wao wakiwa ni kutoka Tanzania.

Kasisi huyo John Wortherspoon ambaye kwa sasa anafanya ziara maalum Tanzania, amesema yeye ndiye ambaye amekuwa akisambaza barua zinazodaiwa kuandikwa na wafungwa wanaoshikiliwa kwenye magerezahayo ambapo baadhi yao wametaja majina ya watu wanaodaiwa kuwa wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya waliowatuma kusafirisha dawa hizo.

Padre Wotherspoon amefika kuonana na familia za wafungwa hao pamoja na idara za serikali zinazohusika na mapambano dhidi ya biashara hiyo hatari ya dawa za kulevya.

Mwandishi wa BBC mjini Dar es Salaam alifuatialia habari na kugundua kwamba kwa muda sasa barua zimekuwa zikichapishwa kwenye mtandao zikielezea maisha ya wafungwa walionaswa na mamlaka za Hong Kong.

Sasa Padre Wotherspoon amejitokeza hapa Tanzania na kusimulia zaidi maisha aliyowakuta nao wafungwa hao ambao amekuwa akiwatembelea gerezani na kuwaunganisha kwa mawasiliano na ndugu zao.


'Padre anayejitolea'

Akizungumza na BBC, Padre Wotherspoon, ambaye anajitolea kazi ya kuelimisha vijana kuhusu madhara ya biashara hiyo haramu na hatari, amesema zaidiya Watanzania mia moja wanashikiliwa katika magereza za mamlaka ya Hong Kong kwa makosa ya kuingiza dawa za kulevya katika eneo hilo licha ya adhabu ya kifungo cha maisha au kifo kwa watu wanaokamatwa, lakini ni kwa nini aliamua kubeba jukumu hilo?

"Waafrika wengi walinyongwa katika kipindi cha miaka miaka mitatu iliyopita.
Ni idadi kubwa ya vifo vinavyotokana na kunyongwa. Kwa hiyo niliogopa sana. Nilijaribu kuwapata wahusika wenyewe wawambie watu kwamba wasijaribu kupeleka dawa za kulevya Hong Kong, Macau, China. Lakini waliendelea kuja.

Wiki moja mwezi Julai 2013, saba walikamatwa uwanja wa ndege wa Hong Kong katika wiki moja. Katika hali hiyo nilipata ruhusa kutoka mamlaka ya magereza kuwawezesha baadhi ya wafungwa kuandika barua katika mtandao wetu kuwaonya watu nchini Tanzania na sehemu nyingine barani Afrika kuhusu hatari ya kusafirisha dawa za Kulevya kwenda Hong Kong, '' alisema padri huyo.

Baada ya kubaini hali hiyo Father John aliwatembelea magerezani huko Hong Kong na kuwaonya juu ya hatari inayowakabili vijana wengi barani Afrika. Lakini huwa anawaambia nini vijana hao mara anapowatembelea.'

"Ninawaambia andikeni kwa marafiki zenu, familia zenu, makanisa yenu, wanasiasa wenu vyombo vyenu vya habari waambieni watu waache kuleta dawa za kulevya Hong Kong kwa sababu wengi walidanganywa, waliambiwa kuwa ni rahisi kuingiza dawa za kulevya Hong Kong. Lakini ukweli ni kwamba ni vigumu sana na waliambiwa ukikamatwa utafungwa kifungo cha miaka miwili lakini ukweli ni kwamba kifungo cha chini ni miaka saba au nane."


''Vijana wanavyorubuniwa"

Hata hivyo Father Wotherspoon anasema alichobaini ni kwamba licha ya tamaa ya utajiri wa haraka haraka, wengi wa vijana hao au wote walirubuniwa na vigogo wa biashara hiyo kwa kuwabebesha dawa za kulevya ili tu wakidhi mahitaji yao ya lazima kama kutunza familia zao.

Amesema baada ya kuanza kampeni hiyo mwaka 2013 idadi ya vijana wanaokamatwa imepungua kwa kiasi kikubwa kutokana na baadhi ya vyombo vya habari nchini Tanzania kunasa habari kutoka tovuti ya Father John ya v2catholic.com na habari hizo kusambaa haraka, ambapo amesema badala ya kuwakamata watu watatu wanne, watano kwa wiki, kwa kuanzia miezi minane 2013, ni mtu mmoja tu alikamatwa kwa karibu miezi minane katika uwanja wa ndege wa Hong Kong.

Father John anasema vigogo wa biashara ya dawa za kulevya wamekuwa wakibuni mbinu mpya kwa kuwatumia watu kutoka vijijini badala ya mijini kwa sababu watu wa vijijini hawajui hatari ya biashara hiyo au waliambiwa dakika za mwisho wakiwa uwanja wa ndege kuwa ni nchi gani walitaiwa kwenda na dawa hizo.

Baada ya kuwasili Tanzania amekutana na familia mbalimbali za wafungwa magereza ya Hong Kong.

Saleh ni ndugu wa mmoja wa wafungwa na anaeleza hisia walizopata kama familia mara baada ya kukutana na Father Wotherspoon.

BBC imekutana na Kamishna wa kikosi cha kudhibiti dawa za kulevya nchini Tanzania, Godfrey Nzowa ambaye amesema jitihada zinazochukuliwa na makundi mbalimbali pamoja na watu binafsi katika kuwaelimisha watu hatari ya dawa hizo ambapo mwaka jana pekee walikamata kilo mia nne za dawa za kulevya aina ya heroin na kuokoa maisha ya watumiaji karibu milioni saba ili wasiweze kuzipata na kutumia.

Na kuhusu namna wanavyokabiliana na watu wanaodaiwa kuwa vigogo wa dawa za kulevya Kamishna Nzowa anaeleza namna wanavyopambana nao pindi wanapopata majina ya watu hao.

ESCROW YABURUZA WAWILI MAHAKAMANI

WATUMISHI wawili waandamizi wa Serikali wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka ya kupokea zaidi ya Shmilioni 485 ambazo ni sehemu ya fedha zilizokuwa kwenye akaunti ya Tegeta Escrow.

Washitakiwa hao ni Mkurugenzi wa Masuala ya Kisheria wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rugonzibwa Mujunangoma na Mhandisi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Theophil Bwakea.

Washitakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo jana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na kusomewa mashitaka mbele ya mahakimu wawili tofauti.

Awali, Bwakea alifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi, Frank Moshi akidaiwa kupokea rushwa ya Sh milioni 161,700,000 kutoka kwa mmiliki wa kampuni ya kufua umeme ya VIP Engineering and Marketing ambaye pia alikuwa Mkurugenzi wa kampuni ya IPTL, James Rugemalira.

Wakili kutoka Takukuru, Leonard Swai alidai, Februari 12, 2014 katikajengo la Benki ya Mkombozi Ilala, alijipatia fedha hizo kupitia akaunti namba 00410102643901 akiwa kama mjumbe aliyeandaa sera kuruhusu sekta binafsi kuzalisha na kuliuzia umeme Shirika la Umeme (Tanesco).

Mujunangoma alifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Emilius Mchauru na kusomewa mashitaka ya kupokea Shmilioni 323,400,000 baada ya kushughulikia masuala ya kampuni ya IPTL kama mfilisi jambo ambalo linahusiana na kazi yake.

Wakili Swai alidai Februari 5, 2014 katika jengo la Benki ya Mkombozi alipokea rushwa ya fedha hizo kupitia akaunti namba 00120102602001 kutoka kwa Rugemalira. Inadaiwa fedha hizo ni sehemu ya zilizokuwa kwenye akaunti ya Tegeta Escrow.

Washitakiwa walikana mashitaka na upande wa Jamhuri ulidai upelelezi wa kesi hizo umekamilika na kuomba terehe nyingine kwa ajili yawashitakiwa kusomewa maelezo ya awali.

Washitakiwa wote wameachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza masharti yaliyotolewa, ambapo Bwakea alitakiwa kuwa na wadhamini wawili wanaofanya kazi serikalini waliotoa Sh milioni 25 kilammoja. Aidha, Mahakama imeamuru fedha zilizo katika akaunti ya Bwakea zisitumike hadi kesi hiyo itakapokwisha.

Mujunangoma aliwasilisha hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya nusu ya fedha anazodaiwa kupokea, alikuwa na wadhamini wawili watumishi wa umma waliosaini hati ya Sh milioni 10 kila mmoja, aidha upande wa Jamhuri umetakiwa kuwasilisha ombi la kuzuia matumizi ya akaunti yenye fedha anazodaiwa kupokea.

Kesi zitatajwa Januari 29 mwaka huukwa ajili ya kuwasomea washitakiwa maelezo ya awali. Mujunangoma atafika mahakamani kesho kwa ajili ya kuwasilisha tathmini ya hati alizotoa mahakamani kama dhamana pamoja na baadhi ya nyaraka za wadhamini wake.

WanaCCM kikaangoni

Katika hatua nyingine, sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow limechukua sura mpya ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), baada ya Kamati Kuu ya chama hicho kuagiza hatua za kimaadili zichukuliwe dhidi ya wote waliohusika na ukiukwaji wa maadili katika sakata hilo.

Wanaobanwa zaidi ni wale ambao nisehemu ya vikao vya maamuzi katika chama hicho tawala. Hayo yalisemwa jana na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye alipozungumza na waandishi wa habari mjini humo kuzungumzia yaliyojadiliwa katika kikao cha Kamati Kuu ya CCM kilichokutana juzi.

Alisema Kikao cha Kamati Ndogo ya Maadili kitafanyika Januari 19, kwa ajili ya utekelezaji wa agizo hilo.

Aliongeza kuwa, CCM imesikitishwa sana na sakata hilo linalohusishwa na uchotaji fedha zaidi ya Sh milioni 306 katika akaunti ya Tegeta Escrow katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) iliyofunguliwa baada ya kuibuka kwa mgogoro wa kibiashara baina ya kampuni ya kufua umeme ya IPTL na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO).

"Baada ya kulijadili kwa muda mrefu na kwa kina Kamati Kuu imeamua pamoja na yale ambayo yameshatekelezwa na serikali, Kamati Kuu imeitaka serikali na vyombo vinavyohusika kuendelea kutekeleza maazimio ya bunge juu ya swala hilo."

Aidha, Kamati Kuu imewataka wote wanaopewa dhamana wajenge utamaduni wa kuwajibika kwa dhamana zao, na wasipowajibika waliowapa dhamana wachukue hatua za kuwawajibisha. "Na Tatu, Kamati Kuu imeiagiza Kamati Ndogoya Maadili kuchukua hatua za kimaadili kwa wale wote waliohusika na ukiukwaji wa maadili kwenye sakata la Escrow na wako kwenye vikao vya maamuzi vya Chama."

Sakata la Escrow, baada ya kuibua mjadala mzito bungeni, wabunge walitoka na maazimio kadhaa yaliyowasilishwa kwa Rais Jakaya Kikwete, ikiwa ni pamoja na kutaka kuwajibishwa kwa wahusika wa sakata hilo, wakiwemo mawaziri na watendaji wengine serikalini.

Tayari Rais Kikwete ameshachukua hatua kadhaa, ikiwa ni pamoja na kutengua uteuzi wa aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Eliakim Maswi amesimamishwa kwamuda usiojulikana ili kupisha uchunguzi wakati Jaji Frederick Werema amejiuzulu wadhifa wake wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, akisema anawajibika, ingawa amekuwa akisisitiza haoni kama alifanya kosa lolote katika kushauri juu ya suala la akaunti ya Escrow.

Chanzo: Habari leo

UDOM WACHAPWA MABOMU ALFAJIRI

Jeshi la Polisi jana lilifyatua mabomu kuwatawanya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) waliokuwa wanaandamana kushinikiza kulipwa madai yao.

Katika vurugu hizo, polisi wealiwatia mbaroni wanafunzi 86 wanaosoma programu maalum ya Stashahada ya Ualimu kwa tuhuma za kuhamasisha uvunjifu wa amani na kufanya maandamano.

Wanafunzi hao ni wa programu maalumu katika masomo ya Sayansi, Hisabati na Teknohama iliyoanza mwaka jana.

Wanafunzi hao waligoma kuingia madarasani jana na kufanya maandamano ya amani kuelekea ofisi ya Waziri Mkuu kwa lengo la kuwasilisha madai yao.

Wakati wakiandamana kwa kupitia njia za pembezoni kuelekea kwa Waziri Mkuu katika eneo la Makulu, polisi walifika ghafla Jeshi la polisi liliwatawanya kwa mabomu ya machozi na hivyo kushindwa kufika katika ofisi hiyo.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoani hapa, David Misime, wanafunzi hao walifanya maandamano hayo majira ya saa 11:30 alfajiri jana.

Alisema wanafunzi hao walikuwa na malengo ya kuelekea katika ofisi mbalimbali za viongozi wa serikali zilizopo mjini Dodoma.

Alisema chanzo cha wanafunzi kugoma ni kutokana na maamuzi waliyokubaliana katika kikao chao walichofanya cha tarehe juzi wakidai kuongezewa posho ya chakula na kwamba hata kiasi ambacho wanapewa wamechelewa kupewa.

"Hata hivyo uongozi wa chuo uliwaeleza kuwa wenye mamlaka ya kuzungumzia sualala kuongezewa posho ni Bodi ya Mikopo na siyo chuo, hivyo walitakiwa kufuata taratibu za kuwasilisha madai yao pia walielezwa kuwa hundi kwa ajiliya fedha za posho zao zimeshasainiwa na kuwasilishwa benki ili waweze kuanza kupewa posho zao," alisema Misime.

Alisema hata hivyo, wanafunzi hao hawakuridhika na usiku wakaanza kuhamasishana kufanya maandamano, jambo ambalo ni kosa.

Alisema ushahidi wa awali wa meseji, vipeperushi na vikao visivyo halali mahakamani kwa kosa la Kufanya maandamano yasiyo na kibali.

"Endapo wataendelea kufanya hivyo, wasije wakalilaumu Jeshila Polisi kwani hatua zitachukuliwa bila kujali wao ni wanafunzi wa vyuo vikuu kulingana na sheria inavyoelekeza ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani," alisema Misime.

Wakizungumza jana na NIPASHE kwa nyakati tofauti, wanafunzi hao walidai sababu zilizowafanya kugoma na kuandamana ni hali ngumu ya maisha chuoni hapo kutokana na uongozi wa chuo kutowalipa fedha zao za malazi, chakula, vitabu na viandikwa ambazo walitakiwa kupatiwa Januari 6, mwaka huu.

"Tumeamua kugoma na kuandamana kwa lengo la kwenda Ofisi ya Waziri Mkuu kupeleka malalamiko yetu, kama Serikali ilikuwa haijajipanga kwa ajili ya kutusomesha ni bora waturuhusu turudi kwanza nyumbani kuliko kuendelea kuteseka na njaa hapa chuoni," alisema mmoja wa wanafunzi ambaye hakutaka kutaja jina lake.

Wakifanunua madai yao walisema kwa mujibu wa barua zao za kuitwa kujiunga naUdom, waliambiwa kuwa Serikali itagharamimia gharama zote ikiwa ni pamoja na ada, chakula, malazi, vitabu na viandikwa.

Hata hivyo, walisema walikuwa wanayapeleka madai yao Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuchelewesha malipo yao, kukatwa malipo bila kupewa risiti, kupewa ufafanuzi juu ya tamko la Rais wa Jamhuri ya Muungano kuwa watapatiwa mkopo asilimia 100 kwa kozi hiyo maalum.

Walisema kutokana na tamko hilo, kila mwanafunzi anapaswakulipwa Sh. 10,000 kwa siku.

Walitaja madai mengine kuwa ni malipo wanayosainishwa na chuo ya Sh. 6,000 kwa siku nayo kuendelea kukatwa badala ya kulipwa Sh. 367,500 kwa miezi miwili, lakini wanalipwa Sh. 226,500.

"Kutokana na barua hizi tulijua Serikali itatusaidia kutupatia elimu bila matatizo, hivyo tulifika chuoni hapo tukiwa na akiba kidogo tulizopewa kutokakwa wazazi wetu, lakini kwa sasa tumeishiwa kabisa," alieleza mwanafunzi mwingine bila kutaka jina lake kutajwa.

Walibainisha kuwa walishapeleka malalamiko yao kwa uongozi wa chuo, lakini wameshindwa kuwasaidia na kadri siku zinavyozidi wanakumbana na hali ngumu ya maisha.

Walisema uongozi wa chuo baada ya kusikia kuwa jana watagoma na kufanya maandamano, waliingiza malipo kwa wanafunzi 392 kati ya 2,000.

NIPASHE ilimtafuta Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Idrisa Kikula, ili kuzungumzia madai hao, lakini simu yake ilipokelewa na msaidizi wake ambaye alijibu kuwa alikuwa katika kikao, hivyo atafutwe baadaye. Hadi tunakwenda mitamboni, Prof. Kikula hakupatikana kutoa ufafanuzi huo.

Chanzo: NIPASHE

WAJUMBE WA ARSENAL KUFIKA TANZANIA

*Kukutana na wafanya biashara
*Wanaondoka London Jumamosi hii
* Kukutana na baadhi ya wapenzi na mashabiki wa Arsenal


Klabu ya Arsenal imepanga kutuma maofisa biashara wake jijini Dar es Salaam, Tanzania kwa ajili ya kujadili fursa za ushirikiano na wafanyabiashara kadhaa wakubwa nchini Tanzania.

Huu utakuwa ujumbe wa kwanza kabisa wa Arsenal nchini Tanzania, ambapo klabu hii kubwa ya England inataka kujenga ushirika mkubwa kabisa katika maeneo ya masoko nachapa zake, ili kutanua mafanikio yaliyofikiwa kwenye nchi nyingine za Afrika kama Kenya, Uganda na Nigeria.

Washika Bunduki hao wa London wanataka kutoa fursa kwa benki za Tanzania pamoja na kampuni za simu na taasisi nyingine kuweza kupata rasilimali zihusianazo na Arsenal, kama vile bidhaa zilizosainiwa kwa majina ya wachezaji, tiketi za mechi.

Safari hii kwa kiasi kikubwa imefanikishwa na Ubalozi wa Tanzania katika Uingereza, Kupitia kwa Mhe Balozi Peter Kallaghe, ambaye binafsi ameshiriki kuwaarifu maafisa hao, mazingira ya nyumbani, na ukuaji wa sekta za binafsi katika kukuza uchumi wa Tanzania.

Arsenal wanasema kwamba wanaweza kuwapatia washirika wao hao uwanja mpana wa masoko kwa ajili ya kuwasaidia kutimiza malengo mbalimbali ya kibiashara.

Ofisa Biashara Mkuu wa Arsenal, Vinai Venkatesham amesema kwamba wameichagua Tanzania kwa sababu wana washabiki wengi, na kwa kushirikiana na taasisi za Tanzania, watakuwa karibu zaidi na washabiki wao kuliko ilivyokuwa awali.

"Katika bara lenye nchi zaidi ya 50, tumechagua kuzuru Tanzania kimkakati kwa sababu tunaiamini nchi hiyo. Arsenal ina mamilioni ya Watanzania ambao ni washabiki waaminifu na wenye mapenzi makubwa nayo.

"Kwa kushirikiana na taasisi za huko,tutaweza kuisogeza klabu karibu zaidi na washabiki hao kuliko ilivyokuwa awali, huku tukizipatia taasisi husika fursa pekee za kuifikia klabu yetu," akasema Venkatesham.

Wajumbe hao wa jopo la Maendeleo ya Ushirikiano ya Arsenal wanatarajia kuwasili nchini Tanzania Januari 18 mwaka huu, ambapo watakaa kwa wiki moja jijini Dar es Salaam, kuitisha mikutano kadhaa ya awali ya kibiaashara na kuzindua rasmi mchakato wa kutafuta washirika wa kwanza kabisa nchini Tanzania.

ELIMU SEKONDARI NA MSINGI KUTOLEWA BURE

Rais Jakaya Kikwete ametangaza habari njema kwa Watanzania kwamba kuanzia mwaka kesho, elimu ya msingi na sekondari itatolewa bure.

Alitangaza azma hiyo ya serikali juzi, wakati akizungumza katika karamu aliyowaandalia mabalozi ya kuukaribisha mwaka 2015 iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.

Alisema hatua hiyo inakuja baada ya serikali kukamilisha sera mpya ya elimu na ufundi ili kuboresha sekta hiyo ambayo imepitishwa na Baraza la Mawaziri.

Hatua hiyo inachukuliwa katika kuhakikisha kuwa kila Mtanzania anapata kiwango hicho cha elimu kwa gharama inayobebwa na serikali.

"Kwenye sera mpya, imeainisha jinsi ya utoaji wa elimu bora na viwango vinavyokubalika katika ufundi, hii itawezesha elimu hizi mbili kukidhi matakwa katika soko la ajira pamoja na kujiajiri," alisema.

"Wazo hili la kufanya elimu hii kuwafikia kila mmoja sasa ndilo jukumu lililo mbele yetu tukianza na maandalizi ya kuhakikisha tunalitimiza lengo hili kuu kwa ufanisi mkubwa,"alisema.

Hatua ya Rais ya kutangaza azma ya kutoa elimu bure, imekuja miaka 10 baada ya wapinzani hasa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kueleza kuwa, moja ya mikakati yao ni kutoa elimu bure kwa kila Mtanzania iwapo watachaguliwa kuongoza taifa.

Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willibrod Slaa, aliwahi kutamka katika moja ya mikutano ya hadhara kuwa chama hicho kimejiwekea ajenda nne na kuwa ifikapo 2015 kikishika dola, kazi yao ni kutoa elimu bure na bora kwa Watanzania.

Kwa upande wa kutoa elimu bure barani Afrika, Kenya ni moja wapo ambapo imeanza kuwapa wananchi wake elimu hiyo baada ya Rais Uhuru Kenyatta kuingia madarakani.

Kuhusu walimu, Rais Kikwete alisema mwaka uliopita katika kuhakikisha elimu ya sekondari inaboreshwa, walimu 36,339 waliajiriwa na kubakisha upungufu wa walimu 45,233 wa shule za msingi na sekondari ambao wataendelea kuajiriwa.

Alisema katika mkakati wa kuimarisha shule za kata katika masomo ya sayansi, ujenzi wa maabara umekamilika kwa asilimia 40.5 na ujenzi unaendelea.

Kwa upande wa ukuaji wa uchumi, Rais Kikwete alisema unatazamiwa kukua kwa asilimia 7.4 mwaka jana ikilinganisha na asilima 7.3 mwaka jana.

Alisema kutokana na ukuaji huo, Tanzania imekuwa miongoni mwa nchi zenye uchumi unaokua kwa kasi duniani.

Hata hivyo, alisema mfumko wa bei umepungua kufikia asilimia 4.8 mwezi uliopita kutoka asilimia sita iliyorekodiwa siku za nyuma.

Aliwaambia waalikwa kuwa hali hiyo imetokana na kuongezeka kwa uzalishaji chakula, ambapo mpaka mwezi uliopita ziada ya nafaka ilifikia tani milioni 3.25.

"Mafanikio haya yamekuja baada ya kutekeleza mipango yetu ya Kilimo Kwanza na mradi wa Ukanda wa Kusini waKilimo, Sagcot," alisema Rais Kikwete.

Rais Kikwete, aliwaambia mabalozi hao kwamba pato la taifa (GDP) limefikia shilingi trilioni 70 mwaka 2013 kutoka shilingi bilioni 53.7 mwaka 2001.

Chanzo: NIPASHE

MWANABLOG ACHAPWA VIBOKO HADHARANI

Mwanablogu nchini Saudia amechapwa viboko hadharani kwa madai ya kutusi dini ya kiislamu.

Raif Badawi ambaye alianzisha mtandao kwa jina ''Liberal Saudi Network'' alihukumiwa kifungo cha miaka 10 msimu wa joto uliopita.

Mahakama pia iliagiza acharazwe viboko 1000.

Amechapwa viboko hivyo katika mji wa Jeddah.

Ilieleweka kwamba angetandikwa viboko hamsini na kwamba alitarajiwa kuchapwa viboko zaidi wiki zilizofuatia.

Mwanablogu huyo alichapwa viboko licha ya wizara ya maswalaya kigeni nchini Marekani kutaka kuondolewa kwa adhabu hiyo walioitaja kama ya kikatili.

RADI YAUA MAMA NA MWANAFUNZI

MKAZI wa kijiji cha Nkana, kata ya Sintali wilayani Nkasi Restuta Dickson (37) na mwanawe Simon Sungura (14) mwanafunzi wa darasa la Saba , shule ya msingi Nkana wamekufa papo hapo baada ya kupigwa na kujeruhiwa na radi walipokuwa shambani mwao.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Rukwa, Jacob Mwaruanda alieleza kuwa mkasa huo ulitokea juzi saa 7:00 mchana baada ya mvua kubwa iliyoambatana na ngurumo na radi hiyo kuwapiga na kuwasababishia mauti papo hapo.

Kamanda alibainisha kuwa mchana huo wa tukio, watu hao walikuwa shambani mwao wakilima na mvua ikaanza kunyesha hivyo wakalazimika kusitisha shughuli ya kilimo na kurejea nyumbani, lakini kabla hawajafika walikumbwa na dhahama hiyo.

Katika tukio jingine, Jeshi la Polisi mkoani hapa linamshikilia mkazi wakijiji cha Mpembano wilayani Sumbawanga akituhumiwa kumtupamtoto wake wa kiume muda mfupi baada ya kujifungua na kumsababishia mauti.Inadaiwa alifanya uamuzi huo kutokana na fedheha ya kupewa ujauzito na shemeji yake.
Kamanda Mwaruanda alisema tukio hilo lilitokea juzi mchana wakati mtuhumiwa huyo ambaye ni bubu kumtelekeza mtoto wake huyo mchanga kwenye mtaro barabarani kijijini humo kisha akarejea nyumbani kwao.

"Uchunguzi wa awali umebainisha kuwa mtuhumiwa huyu alikuwa ameolewa na kuzaa naye watoto wanne lakini waliachana na mumewe kutokana na ugomvi wa kifamilia, ndipo mama huyo alianza mahusiano ya kimapenzi na shemeji yake yaani mdogo wa mumewe wa awali ambaye alimpatia ujauzito na alipobaini alikimbilia kusikojulikana," alibainisha.

Aliongeza kuwa mtuhumiwa huyo atafikishwa mahakamani mara baada ya uchunguzi wa awali utakapokamilika.

UN YAKEMEA MASHAMBULIZI DHIDI YA ALBINO

Umoja wa Mataifa umekemea wimbi la mashambulizi dhidi ya Watu wenye ulemavu wa ngozi, Albino, baada ya tukio la kutekwakwa mtoto wa miaka minne mjini Mwanza.

Mwakilishi wa UN nchini humo Alvaro Rodriguez ameitaka Serikali ya Tanzania kuzidisha juhudi za kupambana na vitendo vya unyanyapaa dhidi ya albino.

Akiwa katika ziara kanda ya ziwa, Mjumbe huyo wa UN amekemea kutekwa kwa binti mdogo na kutoa wito kwa serikali kufanya kila iwezalo kumuokoa na kumkutanisha na Familia yake.

Mtoto Pendo Emmanuel alitekwa akiwa nyumbani kwake Kijiji cha Ndami baada ya Watu kadhaa wakiwa na mapanga kuvamia makazi yao tarehe 27 mwezi Disemba mwaka jana.

Polisi wamesema Watu 15 akiwemo Baba yake wamekamatwa wakihusishwa na tukio la kutekwakwa mtoto huyo.

MTOTO WA JACKIE CHAN ATUPWA JELA KWA KUKAMATWA NA BANGI

Jacee Chan mwana wa mwana nyota wa filamu Jackie Chan amehukumiwa kifungo cha miezi sita jela kwa kutumia mihadarati.

Chan mwenye umri wa miaka 32 alikiri kufanya makosa hayo katika mahakama ya wiliaya ya mjini Beijing Dongcheng kwa kuwaficha wengine ili kutumia dawa za kulevya.

Polisi walivamisa nyumba yake mnamo mwezi Agosti na kupata gramu 100 za marijuana.

Alikabiliwa na hukumu ya miaka mitatu.

Kukamatwa kwake kunajiri kufuatia msako wa dawa za kulevya nchini Uchina ambapo watu kadhaa mashuhuri walikamatwa.

Mnamo mwezi Juni mwaka 2014,rais Xi Jinping aliwaagiza polisi kutumia mikakati mikali ili kusitisha utumizi wa mihadarati.

Kukiri kwa mwana wa mcheza filamu mashuhuri nchini Uchina kunatoa ujumbe muhimu kutoka kwa serikali ya Uchina.

Hakuna aliye na kinga nchini Uchina katika msako huo wa dawa za kulevya.

Chan na nyota wa filamu kutoka Taiwan Kai Ko mwenye umri wa miaka 23 walikamatwa pamoja katika nyumba ya Beijing mnamo mwezi Agosti huku polisi wakisema kuwa walipatikana wametumia bangi.

TRAFIKI KUVAA NEPI WAKATI WA ZIARA YA PAPA FRANCIS

Wakati Papa Francis atakapoitembelea Ufilipino wiki ijayo, askari wa barabarani(trafiki) hawatokubali mitaa ya mji mkuu kufungwa na kuwa na msongamano mkubwa endapo watatakiwa kufanya hivyo.

Askari zaidi ya 2,000 ambao watakuwa na zamu siku za Januari 15-19 kwenye ziara ya Papa watatakiwa kuvaa nepi za watoto (diapes), alisema Francis Tolentino, mwenyekiti wa Uongozi wa Maendeleo ya Metropolitan jijini Manila.

Tolentino pia aliwahamasisha watu ambao watamsubiria kwa masaa kumuona Papa pia wavae nepi.

Zoezi la kuvaa nepi siku ya zamu lilipokelewa vema na watu wake, alisema siku ya Jumatano.

Itakuwa mara ya kwanza kwa askari wa barabarani nchini Ufilipino kuvaa nepi wakiwa kazini mitaani, alisema.

Alipouliza kuwa naye atavaa, Tolentino alisema, "Nitajaribu, ila kwa upande wangu, nina tatizo la kuharisha kidogo."

YANGA YANG'OLEWA KOMBE LA MAPINDUZI

Yanga imeng'oka katika michuano ya Kombe la Mapinduzi baada ya kufungwa bao 1-0 na JKU.

JKU inayomilikiwa na Jeshi la Zanzibar imefanikiwa kuing'oa Yanga katika mechi kali na ya kuvutia kwenye Uwanja wa Amaan, huko Zanzibar.

Muuaji wa Yanga alikuwa Amour Mohammed ambaye alifunga bao hilo adhimu kabisa katika dakika ya 72 na kupeleka simanzi Jangwani,kitendo kilichoivuruga Yanga wasionane na kushindwa kusawazisha, ingawa watoto hao wa Jangwani watajilaumu wenyewe kwa kupoteza nafasi kadhaa za kufumania nyavu bila mafanikio katika kipindi cha kwanza.

Kutokana na ushindi huo, sasa JKU itacheza nusu fainali dhidi ya Mtibwa Sugar ambayo iliing'oa Azam FC.

YAYA TOURE ATWAA TUZO YA MCHEZAJI BORA AFRIKA

Yaya Toure akiwa na tuzo yake ya CAF aliyoshida jana jijini Lagos, Nigeria. Hiyo ni tuzo yake ya nne mfululizo.

Kiungo wa kati wa klabu ya Manchester city Yaya Toure ametangazwa kuwa mchezaji bora wa mwaka 2014 kutoka Afrika kwenye sherehe iliyofanyika huko jijini Lagos nchini Nigeria hapo jana.

Mchezaji huyo amechukua tuzohiyo kwa kuwashinda wachezaji Vicent Enyeama pamoja na Pierre Emerick Aubameyang.

Sherehe hizo zilihusisha na utoaji wa tuzo nyingine kwa washindi kama Mchezaji bora wa kike, Mchezaji bora mdogo wa mwaka,Timu bora ya taifa ya mwaka.

Hata hivyo mchezaji huyo ameweka rekodi ya kuchukua tuzo hiyo kwa vipindi mfululizo ambapo alichukua tuzo hiyo mwaka 2011,2012,2013,2014.


Tuzo zilizotolewa kwa ujumla

Mchezaji bora wa Afrika
Yaya Toure (Cote d'Ivoire and Manchester City)

Mchezaji bora wa Afrika wa ligi za ndani
Firmin Mubele Ndombe (DR Congo and AS Vita)

Mchezaji bora wa kike wa mwaka
Asisat Oshoala (Nigeria and River Angels)

Mchezaji bora mwenye umri mdogo wa mwaka
Asisat Oshoala (Nigeria and River Angels)

Mchezaji bora chipukizi
Yacine Brahimi (Algeria and Porto)

Kocha bora wa mwaka
Kheireddine Madoui (ES Setif)

Timu bora ya taifa ya mwaka:
Algeria

Timu bora ya wanawake ya mwaka
Nigeria

Klabu bora ya mwakaES Setif (Algeria)
Mwamuzi bora wa mwaka
Papa Bakary Gassama (Gambia)

Kiongozi bora wa mpira wa mwaka
Moise Katumbi Chapwe – President of TP Mazembe (DR Congo)

Tuzo kwa klabu kongwe

Oryx Club (Cameroon) – winners of the maiden edition of CAF Champions League 1964 Stade Malien (Mali) – runner up of the maiden edition of CAF Champion's League 1964


Tuzo za heshima

Dr Kwame Nkrumah (First President of Ghana)His Excellency Goodluck Jonthan (President of Nigeria)Kikosi bora cha Afrika cha mwaka

Mlinda mlango: Vincent Enyeama (Nigeria)

Mabeki: Jean Kasulula (DR Congo), Mehdi Benatia (Morocco), Stephane Mbia (Cameroon), Kwadwo Asamoah (Ghana)

Viungo: Yaya Toure (Cote d'Ivoire), Yacine Brahimi (Algeria), Fakhreddine Ben Youssef (Tunisia), Ahmed Musa (Nigeria)

Washambuliaji: Asamoah Gyan(Ghana), Pierre-Emerick Aubameyang (Gabon)


Wachezaji wa akiba

Raïs M'Bolhi (Algeria), Firmin Mubele Ndombe (DR Congo), Ferdjani Sassi (Tunisia), Yao Kouasi Gervais 'Gervinho (Cote d'Ivoire), Abdelrahman Fetori (Libya), Akram Djahnit (Algeria), Roger Assalé (Cote d'Ivoire).

WANALENGA KUNICHAFUA KISIASA - MH. PINDA

Mh. Pinda ameyasema hayo jana wakati akiwahutubia wananchi wa Mkoa wa Katavi katika Hlamshauri ya mpanda katika mkutano wa hadhara ulifanyika mkoani humu nakuongeza kuwa kama angekuwa fisadi basi angekua mmoja wa matajiri wakubwa nchini.

Mh. Pinda amesema kuwa kama kuna mtu mwenye ushahidi wa yeye kufisadi apeleke kwenye vyombo vya dola ili ashughulikiwe kwa mujibu wa sheria na yupo tayari kufungwa endapo ikithibitika kuwa ni fisadi.

Waziri mkuu ameongeza kuwa hatua hyio ya kumchafua inakuja wakti ambapo ametangaza nia ya Urais na kuongeza kuwa kama kuna mtu alikua na ushahidi wa kutosha dhidi ya upataji wake wa pesa amripoti takukuru ili achukuliwe hatua kwani yupo tayari kufungwa.

Aidha Waziri mkuu amepuuza kauli za baadhi ya watu wanaosema kuwa hana maamuzi katika serikali zaidi ya kulialia na kusisitiza kuwa kazi anayoifanya ni kubwa na inayozingatia msingi ya utawala bora na yenye maadili kiutendaji nakama kuna mapungufu wananchi ndio watakaopima na kutoa maamuzi.

MAPACHA WALIOZALIWA WAKIWA WAMEUNGANA WAFARIKI

Watoto mapacha wa kike waliozaliwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Mara iliyopo mjini Musoma wakiwa wameungana sehemu ya kifua na tumbo wamefariki dunia siku ya jumatano majira ya saa 9.10 Alasiri wakiwa katika hospitali ya rufaa ya Bugando jijini Mwanza kabla ya kufanyiwa upasuaji.

Watoto hao pacha walizaliwa Januari 4 mwaka huu na mama mmoja mkazi wa manispaa ya Musoma Helena Paulo wakiwa na uzito wa kilo 4.6 na kisha kusafirishwa hadi katika hospitali ya rufaa Bugando kwa ajili ya uchunguzi zaidi ikiwa ni pamoja na kuangalia uwezekano wa kufanyiwa upasuaji wa kuwatenganisha.

Dk. Shukuru Kibwana ambaye ni daktari katika wodi ya watoto ya hospitali ya rufaa Bugando, amesema timu ya madaktari wa upasuaji na wataalamu wengine wamefanya kila lililowezekana kuokoa maisha ya pacha hao walioungana lakini haikuwezekana.

Ameongeza kuwa kabla ya upasuaji, mapacha hao walitakiwa kupitia tomografia ( CT ) na kufanya kipimo cha Ultra Sound ili kujua kama watoto hao wameungana baadhi ya maeneo na viungo muhimu.

Dkt. Kibwana amesema watoto hao licha ya kuungana, madaktari bingwa wa hospitali hiyo wamegundua kuwa viungo vyao vingi vya mwili vilikuwa vikijitegemea, kila mmoja alikuwa na figo yake, ini na moyo wake.

Muuguzi wa zamu katika wodi ya watoto Sembosah Hiza akieleza kuwa hali ya pacha hao ilianza kubadilika jana mchana jambo lililokwamisha rufaa yao ya kwenda hospitali ya taifa Muhimbili kwa ajili ya vipimo zaidi na uchunguzi.

Agosti 6 mwaka jana mkazi wa Katoro wilayani Geita Neema Luswetura alijifungua watoto wakiwa wameungana sehemu ya kifua na tumbo wakiwa na uzito wa kilo 5.1 hata hivyo walifariki muda mfupi baadaye.

Mwishoni mwa mwaka jana hospitali ya Apollo nchini India ilitangaza kufanikiwa kutenganisha mapacha waliokuwa wameungana kutoka Tanzania katika upasuaji uliochukua saa 11 na wataalamu 50.

ASKARI AJIUA KWA KUJIPIGA RISASI

Askari wa jeshi la polisi, Sajenti Patrick Kondwa amejiua kwa kujipiga risasi akiwa katika ofisi yake kwenye ghala la kuhifadhia silaha katika kituo cha polisi cha wilaya ya mbozi mkoani mbeya.

Akizungumza na ITV kwa njia ya simu, kamanda wa polisi mkoa wa mbeya amekiri kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa chanzo cha kifo hicho bado hakijafahamika na kwamba jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo.

Sajenti Patrick mwenye umri wamiaka 54 ,akiwa katika ofisi yake kwenye chumba cha kuhifadhia silaha katika kituo cha polisi cha wilaya ya mbozi amejipiga risasi mdomoni ambayo imetokea kisogoni na kuondoka na uhai wake, tukio ambalo limetokea majira ya saa tisa usiku na kuthibitishwa na kaimu mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo, ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya ileje, Rosemary Staki Senyamule.

Baadhi ya waombolezaji ambao wamezungumza na ITV wamesema kuwa wamepokea msiba huo kwa masikitiko makubwa hasa kwa kuzingatia kuwa Sajenti Patrick alikuwani askari mwadilifu na anayeipenda kazi yake.


Chanzo: ITV

MWANAUME MWENYE JINSI MBILI ASIMULIA MAISHA YAKE

Mwanamume mwenye jinsi mbili, amezungumza na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) na kusema kama wazazi wake wangemshauri kuhusu hali hiyo, asingeogopa kujitambulisha ulimwenguni.

Mwanamume huyo anayejitambulisha kwa jina la Triple D (25) kutoka Mashariki mwa pwani ya Marekani alisema kutokana na hali hiyo amekuwa na uhusiano wa kimapenzi na wanawake 1,000, kutokana na kutodumu nao muda mrefu.

Alisema sehemu zake hizo zinafanya kazi vyema na kwamba hajabahatika kuwa na uhusiano wa kimapenzi uliodumu.

Mwanamume huyu pia anaugua ugonjwa unaoitwa 'diphallia.'

Kwa mujibu wa Jarida la Afya la BMJ, mwanamume mmoja kati ya milioni tano, duniani huzaliwa na hali hiyo.

"Maisha yangu hayatakuwa sawatena ikiwa nitajitambulisha duniani," alisema Triple D. Hata hivyo, Triple D alisema BBC ilikubali kuhifadhi jina la kijana huyo na hata kutoonyesha sura yake.

Alisema hataki kuwa kichekesho kwa jamii hasa anakoishi.

Alisema alipokuwa mdogo, wazazi wake walimwambia kuwa kutokana na maumbile yake, yeye ni mtoto mwenye jinsi za kipekee.

Alisimulia kuwa wazazi wake walimkalisha chini na kuanza kumwelezea kwamba asithubutu kucheza mchezo ya kitoto na wala asivue nguo za ndani mbele ya watu.

Kutokana na mawaidha ya wazazi wake, alisema kwamba aliweza kuwa msiri, lakini alipokuwa shule ya sekondari wanafunzi wenzake waligundua na ndipo alipopata masaibu mengi.

"Mwanzoni, sikutaka wanafunzi wengine shuleni wajue hali yangu, kwa kuwa sikupenda kumuudhi yeyote," alisema.

Triple D alisema anatamani wazazi wake wangemwambia kwamba watu wakimwona katika hali hiyo watamcheka.

"Sikutaka wanamume wenzangu kuhisi vibaya kutokana na hali niliyonayo mimi na kuanza kuniona kama mimi siyo mtu wa kawaida," alisema Triple D.

Alisema alipokuwa na miaka 16,alitaka kufanyiwa upasuaji ili kuondolewa jinsi moja kwa sababu wasichana walikuwa wakimtazama sana katika maeneo hayo.

"Natamani sana wazazi wangu wangenishauri kuhusu hali yangu kwani nisingeogopa kujitangaza hata kidogo ," alisema.

Triple D alisema changamoto kubwa ni kununua nguo za ndani zinazolingana na maumbile yake.

VIONGOZI WA SIASA WAMTAKA RAIS KIKWETE KUTEKELEZA AHADI YA KUMNG'OA MUHONGO

Viongozi wa vyama vya siasa nchini wamemtaka rais Jakaya Kikwete kutekeleza ahadi yake aliyoahidi wakati wa mkutano na wazee wa Dar es Salaam ya kufanya maamuzi ya kumwajibisha waziri wa nishati na madini ambaye alimweka kiporo na kudai kuwa atatoa maamuzi ndani ya siku mbili lakini hadi leo amekaa kimya.
Mwenyekiti wa chama cha wananchi CUF Prof Iibrahim Lipumba amesema suala la viongozi wakiwemo mawaziri kuwajibika halikuanza leo hasa anaposhindwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu na kuisababishia serikali hasara au kushusha heshima ya taifa hivyo ni vyema uwajibikaji ukawa ni kwa kila mtumishi wa umma bila kubagua ili kuleta tija kwa taifa.

Kwa upande wake mjumbe wa halmashauri kuu taifa ya chama cha mapinduzi CCM Bw Najim Msenga amesema niimani ya chama chake kuwa rais atafanya maamuzi sahihi kwa maslahi ya taifa kama alivyoahidi na kwamba suala hilo haliwezi kuathiri uhai wa CCM kwani bado iko imara baada ya baadhi ya watuhumiwa kuchukuliwa hatua.

Akizungumzia suala hilo katibu mkuu wa chama cha demokrasia na maendeleo Chadema Dk Willbroad Silaa amesema hata hao waliojiuzulu na kuenguliwa uteuzi wao maadam uchunguzi ulifanywa na vyombo sahihi hadi kufikia hatua ya kupelekwa bungeni na kujadiliwa na wao kutoa maazimio watuhumiwa wote hadi sasa walipaswa wawe wamefikishwa mahakamani.

Katika mkutano wake na wazee wa Dar es Salaam uliofanyika ukumbi wa Diamond Jublee desemba 22 mwaka jana rais Kikwete alitengua uteuzi wa aliyekuwa waziri wa ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi Mh Anna Tibaijuka na kutangaza kumweka kiporo waziri wa nishati na madini Prof Muhongo.

BEI YA MAFUTA YASHUKA

BEI ya mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa, imeshuka kuanzia leo, huku watumiaji wa petroli wakipata nafuu zaidi kutokana na kuuzwa chini ya Sh 2,000 baada ya kipindi cha muda mrefu.

Kutokana na kushuka kwa bei ambako pia kunachangiwa na kushuka kwa bei katika soko la dunia, sasa petroli itauzwa lita moja kwa Sh 1,955, dizeli itakuwa Sh 1,846 kwa kila lita moja na mafuta ya taa yatakuwa yanauzwa kwa Sh 1,833 kwa kila lita moja.

Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), Felix Ngamlagosi alipokuwa akizungumzia mwenendo wa bei za mafuta nchini pamoja na utangazaji wa bei mpya za mafuta.

Alisema kuanzia leo kutakuwa na punguzo la Sh 74 kwa petroli, Sh 62 kwa dizeli na Sh 54 kwa mafuta ya taa.

"Kwa bei ya kesho (leo) katika soko la Dar es Salaam hakutakuwa na mafuta ya zaidi ya Sh 2000. Kutakuwa na punguzo la Sh 74 kwa petroli, Sh 62 kwa dizeli na Sh 54 kwa mafuta ya taa," alisema.

Alisema gharama za mafuta yatakayokwenda mikoani zitaongezeka kutokana na usafiri. Alisisitiza kuwa, Ewura itahakikisha kuwa gharama zilizotangazwa ndizo zitakazotumika kwa wananchi.

Mkurugenzi huyo alisema bei ya mafuta ya mwezi Januari nchini, ni bei katika soko la dunia iliyotumika mwezi mmoja uliopita.

"Kwa Tanzania bei ya Desemba ni ya mafuta ya Oktoba hapa nchini na bei za Novemba ndizo zitatumika kesho (leo) hapa nchini," alisema.

Alisema katika kipindi cha robo ya mwisho wa mwaka kuanzia Septemba hadi Desemba mwaka jana, bei za mafuta ghafi zimekuwa zikishuka kwa kasi ikilinganishwa na kipindi cha nyuma, bei zimeshuka kutoka dola 100 (Sh 170,000) kwa pipa hadi kufikia wastani wa dola 60 (Sh 102,000) kwa pipa moja ambayo ni sawa na kushuka kwa bei kwa asilimia 40.

Kwa maelezo yake, asilimia ya kushuka kwa bei katika soko la ndani ni tofauti na kushuka katika soko la dunia kwa sababu mchangowa bei za soko la dunia katika bei za soko la ndani ni takribani asilimia 60.

"Gharama nyingine kodi za serikali, gharama za usafirishaji, gharama za usambazaji na gharama za upokeaji mafuta ambazo huchangia katika bei hazikushuka kwa sababu hazitegemei kushuka kwa bei za soko la dunia," alisema.

BLATTER APATA MPINZANI MBIO ZA URAIS

Makamu wa Rais wa shirikisho la soka duniani, Mwanamfalme Ali Bin Al Hussein wa Jordan, amesema kuwa atamenyana na Sepp Blatter kuwania urais wa shirikisho hilo.

Ali Bin Al Hussein amesema atagombea urais wa shirikisho hilo katika uchaguzi utakaofanyika mwezi Mei.

Sepp Blatter anawania urais wa shirikisho hilo kwa muhula wa tano.

Kwa upande wake, Ali Bin Hussein, huenda akapokea uungwaji mkono wa mashirikisho ya soka Ulaya ingawa haijabainika ikiwa ataungwa mkono na shirikisho lenye nguvu sana la soka ya Bara Asia.

Mwanamfalme huyo, amesema ni wakati sasa wa kubadilisha mambo katika shirikisho hilo hasa kutokana na kashfa nyingi ambazo zimekumba soka duniani.

Alikuwa akigusia madai ya rushwa ambayo amehusishwa nayo, bwana Blatter na kutikisa uongozi wake wa shirikisho hilo kwa miaka 17 iliyopita.

Mwanadiplomasia wa Ufaransa Jerome Champagne, pia anajiandaa kuwania uongozi huo dhidi ya wawili hao.

DAR ES SALAAM JIJI GHALI KUISHI

Wakazi wa jiji la Dar es Salaam hutumia gharama kubwa zaidi, kulipia mahitaji yao ya muhimu kuliko wenzao wengine wa Afrika mashariki, jijini Nairobi na Kampala,utafiti uliofanywa na Shirika linalotathimini gharama za maisha, Numbeo umeeleza.

Utafiti huu ulifanywa ukihusisha miji mikubwa 22 ukiangalia uwezo wa kununua bidhaa, biashara za migahawani, hali kadhalika utafiti huu ulijikita kwenye gharama za juu na urahisi wa maisha ya mijini Kwa mujibu wa Ripoti ya Numbeo, takwimu za gharama za watumiaji kwa wakazi wa Dar es Salaam kwenye bidhaa na huduma mbalimbali ni asilimia 62.83 ambayo imezidi Kampala na Nairobi zenye asilimia 54.34.

Kwa sasa Kenya ni nchi inayoongoza kwa kuwa na uchumi mkubwa Afrika Mashariki na iko nafasi ya sita barani Afrika, hata hivyo kwa mujibu wa matazamio ya Benki ya Standard Charterd , Tanzania inaelekea kuipiku Kenya na kuwa nchi yenye uchumi mkubwa ifikapo mwaka 2030 iwapo pato la taifa halitabadilika.

DIWANI KUMLIPIA PINDA FOMU YA URAIS

Diwani wa Kata ya Makanyagio (CHADEMA) katika Halmashauri ya Mjiwa Mpanda Idd Nzguye amemwahidi Waziri Mkuu Mizengo kuwa atamlipia pesa za gharama za kuchukulia fomu za kugombea Urais Nzguye alitowa ahadi hiyo mbele ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda wakati wa sherehe za kuuwaga mwaka 2014 na kuukaribisha mwaka 2015 zilizofanyika katika Hotel ya Lyamba lyamfipa mjini hapa.

Alisema kuwa ameridhishwa na utendaji wake wa kazi hivyo utakapofikia kipindi cha kuchukua fomu za kugombea Urais gharama ya fomu za kugombea Urais atalipa yeye Diwani Nzguye Alieleza mbele ya umati wa watu waliohudhuria sherehe hizo kuwa Mizigo Pinda anaishi kwenye Kata yakeya Makanyagio hivyo yeye kama Diwani wa Kata hiyo ameamua kutoa ahadi ya kulimpia gharama za pesa za kuchukilia fomu za kugombea Urais Alisema ni jambo la kujivunia kwake kuona mgombea Urais anatoka kwenye kata yake anayoiongoza hivyo ni wajibu wake kumsaidia wananchi wake huyo ambae ni Pinda.

Alisema sababu nyingine iliyomvutia mpaka afikie uamuzi huo wa kumwahidi kulipia fomu ya kugombea Urais ni jinsi ambavyo Pinda hakuusika kabisa na tuhuma za kuchota fedha za IPTL.

Nzguye alisema haoni sababu yoyote ya kutomlipia fomu za kugombea Urais kutokana najitihada zinazofanywa na Pinda za kusimamia shughuli za Serikali.

AUA, AJIUA NA KUACHA UJUMBE

Mfanyabiashara wa mbao Manispaa ya Songea, Emmanuel Moshi (40), mkazi wa Marangu, mkoani Kilimanjaro amemuua mfanyabiashara mwenzake aliyetambuliwa kwa jina la Didas Alphonce (64), mkazi wa Kilema Kilimanjaro kwa kumpasua kichwa kwa shoka, kisha yeye mwenyewe kujinyonga kwa kutumia kamba ya katani katika stoo ya nyumba waliyokuwa wakiishi.

Inadaiwa kuwa Moshi alichukua uamuzi huo baada ya Alphonce kumdhulumu zaidi ya Sh87.4 milioni.

Wakizungumza na gazeti hili jana, watu wa karibu na wafanyabiashara hao ambao hawakupenda majina yao kuandi kwa kwenye gazeti, walidai kuwa wafanyabiashara hao walikuwa wakiishi nyumba ya ndugu yake, Didas na kufanya biashara za kuuza mbao pamoja.

Walidai kuwa, Desemba 30 mwaka jana, wafanyabiashara hao walikuwa wakinywa pombe kwenye Bwalo la Magereza na Moshi alikuwa akilalamika kudhulumiwa na Didas.

Mashuhuda hao waliongeza kuwa tangu siku hiyo, wafanyabiashara hao hawakuonekana tena hadi jana.

Ilidaiwa kuwa, mwenye nyumbahuyo alitumia funguo zake za akiba kufungua nyumba hiyo nakukuta mwili wa mjomba wake ukiwa umepigwa na shoka na tayari umeanza kuharibika.

Mtu mmoja ambaye jina lake tunalihifadhi alitoa taarifa kituocha polisi na walipofika waliubaini pia mwili wa Moshi aliyejinyonga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kudai uchunguzi wa awali unaonyesha wafanyabiashara hao walikuwa wanadaiana pesa.

Alisema Mosha ameacha ujumbe mrefu wa karatasi nne aliouandika kuhusiana na mauaji hayo.

Ujumbe huo: "Kataeni wadhulumaji kati ya matajiri na maskini, nimeondoa dhambi kubwa ya dhuluma iliyokuwa ikinitesa ulimwenguni, wadhulumaji wasifumbiwe macho jamii iniunge mkono kuondoa watu hawa. "Dhuluma aliyonifanyia mtu huyu imekatisha maisha yangu."

Chanzo: Mwananchi

SIGARA YAMPONZA SZCZESNY

Kipa wa kikosi cha kwanza cha Arsenal, Wojciech Szczesny amepigwa faini ya pauni 20,000 Szczesny amepewa adhabu hiyo baada ya kukuta na kosa la kuvuta sigara muda mchache baada ya kupoteza mchezo dhidi ya Southampton.

Kitendo cha kipa huyo kilisabaisha hasira kwa kocha wake Arsene Wenger na kuamua kumpa adhabu hiyo.

Jack Wilshere pamoja na nahodha wa zamani wa klabu hiyo William Gallas waliwahi kumbwa na tatizo kama hili la uvutaji wa sigara.

PANYA ROAD 510 MBARONI

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linawashikilia watu 510 wakiwemo viongozi watatu wa kundi linalojihusisha na uhalifu la 'Panya Road'.

Watu hao wamekamatwa katika operesheni inayoendeshwa na jeshi hilo, kupambana na uhalifu.

Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo, Suleiman Kova alisema jana kuwa watuhumiwa hao, ni pamoja na watuhumiwa 36 waliokamatwa juzi,kufuatia vurugu iliyotokea Ijumaa iliyopita.

Alisema chimbuko la Operesheni hiyo, inayoendeshwa na wakuu wa Polisi wa Mikoa ya Kipolisi ya Temeke, Kinondoni na Ilala, wapelelezi na askari wa kiintelijensia ni matukio yaliyowahusisha vijana hao na kusababisha tafrani kwa wananchi mbalimbali wa jiji la Dar es Salaam.

Alitaja viongozi wa kundi hilo wanaoshikiliwa kuwa ni Khalfani Said (24) na Said Mohammed (22), wakazi wa Tandale Sokoni katika Manispaa ya Kinondoni na Mohammed Nangula (19), mkazi wa Mburahati kwa Jongo, pia Kinondoni.

Alisema kwamba kazi yao kubwa ni kuwaunganisha na kuratibu uporaji katika maeneo mbalimbali.

Alisema mbali na 'Panya Road', operesheni hiyo ambayo itakuwa ya kudumu kuanzia sasa, imewakamata wapigadebe, wacheza kamari na watuhumiwa wengine waliokamatwa katika vijiwe na katika msako wa nyumba kwa nyumba.

"Imegundulika kwamba kila inapotokea kijana ameuawa, wakatiwa maziko viongozi hawa wanakuwepo na kuwachochea vijana wenzao kufanya vurugu, kama ilivyotokea Januari 2 katika eneo la Magomeni Kagera ambapovijana walipambana na polisi baadaya maziko ya kijana mwenzao aliyefariki kutokana na matukio ya wananchi kujichukulia sheria mkononi Januari Mosi eneo la Mwananyamala.

"Tunashukuru kwa kuwa baadhi ya wananchi waliweza kutupa ushirikiano wa moja kwa moja kuwabaini wahalifu tunaowashikilia, ni ukweli usiopingika kuwa vijana hawa wanaojihusisha na vitendo viovu wanafahamika kwa wananchi hivyo ni jukumu la wazazi, walezi katika mitaa yote ya Dar es Salaam kujihusisha kikamilifu katika kuwabaini vijana hao ili tuweze kukomesha maovu yao ambayo piani kero kwa wananchi," alisema Kamanda Kova.

Aidha, alisema katika operesheni hiyo, pia watuhumiwa hao walikamatwa na vilevi mbalimbali zikiwemo bangi, lita 150 ya pombe kali aina ya gongo na mabunda matatu ya dawa za kulevya aina ya mirungi.

Alisema katika kuhakikisha msako huo unazaa matunda, jeshi hilo limeweka mpango maalumu wa kuwahusisha moja kwa moja watendaji kuanzia ngazi ya Mitaa, Kata na Tarafa ili waweze kushirikiana na polisi kuweza kuwabaini wahalifu au makundi ya uhalifu wa aina hiyo.

Alisema mpango huo utafanikiwa kutokana na semina elekezi iliyotoa mafunzo hayo, iliyofanyika hivi karibuni kwa watendaji hao katika kukabiliana na matukio hayo.

Aliwataka vijana ambao hawana kazi za kufanya, kutafuta njia nyingine za kuendesha maisha yao na siyo kujiingiza katika matumizi ya dawa za kulevya na kufanya makosa ya jinai, yanayowafanya baadhi kujiingiza katika makundi hayo.

Chanzo: Habari Leo

PANYA ROAD 36 WATIWA MBARONI

Jeshi la polisi nchini linawashikilia vijana 36 wa kundi maarufu Panya Road wanaodaiwa kufanya vurugu na kupora mali za watu na kusababisha taharuki katika jiji la Dar es salaam huku baadhi ya wananchi wakitoa maoni tofauti kuhusiana na tukio hilo.

Akitoa ufafanuzi wa taharuki hiyo msemaji wa jeshi la polisi SSP ADVERA BULIMBA ambaye mbali nakuwatoa hofu wananchi kuwa hali hiyo haitajitokeza tena amesema jeshi hilo limejipanga vizuri kukabiliana na vikundi vyovyote vinavyotaka kuvuruga amani ya nchi.

Pia amesema kwamba endapo polisi wasingewadhibiti vijana hao mapema tangu wakiwa makaburini baada ya kumzika mwenzao aliyeuawa na wananchi baada ya kuiba hali ingekuwa mbaya zadi.

Kufuatia tukio hilo baadhi ya wananchi wa maeneo ya Magomeni ambako vurugu zilianzia wameelezea namna zilivyoanza hadi kusababisha watu kuanza kukimbia hovyo na wengine kuacha maduka yao wazi na taarifa kusambaa maeneo mengine.

Katika maeneo ya Mwananyamala na Ubungo baadhi ya waliozungumzia sakata hilo wameitaka serikali kuangalia makundi ya vijana na ikiwezekana wapatiwe elimu ya ujasiriamali bure ili waweze kuendesha maisha.

Wananchi wengine wameshauri vijana wasiokuwa na kazi mitaani wapelekwe jeshini wakafundishwe stadi za kazi pamoja na uzalendo ili kuepuka vitendo hivyo.

Taharuki hiyo ilitokea usiku wa tarehe 2 Januari, 2014 chanzo kikiwa ni kijana mmoja aliyejulikana kwa jina la MOHAMED AYUB kuuawa na wananchi tarehe mosi mwaka huu katika maeneo ya Tandale kwa Mtogole kwa tuhuma za wizi ambapo tarehe 2 maziko yalifanyika na taarifa zilizolifikia jeshi la polisi zilidai kuwa baada ya maziko vijana wenzake walijipanga kufanya fujo ili kulipiza kisasi.