CAR YAPATA RAIS MPYA WA MPITO

Wabunge katika Jamhuri ya Afrikaya Kati, wamemchagua Meya wa mji mkuu Bangui, Catherine Samba-Panza, kama Rais wa mpito.

Samba-Panza, ndie mwanamke wa kwanza kuwahi kushikili wadhifa huo.

Wagombea wanane waliwania wadhifa huo ambao ulikuwa unaushikiliwa na Michael Djotodia, aliyeng'atuka mapema mwezi huu kufuatia shinikizo kutoka kwa viongozi wa mataifa jirani.

Panza alimpiku mshindani wake wa karibu Desire Kolingba katika duru ya pili ya kura hiyo.

Wakati huohuo mawaziri wa mambo ya nje wa Muungano wa Ulaya wamekubaliana kukutana Jumatatu kupeleka wanajeshi zaidi nchini CAR.

Shirika la msalaba mwekundu linasema kuwa takriban watu hamsini wameuawa Kaskazini Magharibi mwa nchi hiyo mwishoni mwa wiki.

Mapigano yalianza wakati Djotodia alipochukua mamlaka mwaka jana kwa njia ya mapinduzi akiungwa mkono na waasi wa kiisilamu katika taifa hilo lenye idadi kubwa ya waumini wa kikristo.

Waisilamu wawili waliteketezwa katika mji mkuu Bangui siku ya Jumapili.

Karibu watu milioni moja wameachwa bila makao kutokana na mgogoro huo.