MAJESHI YA UGANDA KUPAMBANA WA WAASI S.KUSINI

Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, amesema kuwa jeshi la Uganda linashirikiana na wanajeshi wa Sudan kupambana na waasi nchi Sudan Kusini.

Mapigano hayo ambayo yalizuka mwezi uliopita yanaendelea katika maeneo kadhaa ya Sudan kusini, licha ya kufufuliwa kwa mazungumzo ya amani katika nchi jirani ya Ethiopia.

Baada ya wiki kadhaa za tetesi za wanajeshi wa Uganda kuwa nchini Sudan Kusini, jeshi la Uganda sasa limekiri rasmi kuwa liko katika vita na waasi wa Sudan Kusini.

Kwa mujibu wa msemaji wa jeshi,Luteni Kanali Paddy Ankunda, Uganda ina takriban wanajeshi elfu moja na mia sita nchini humo.

Serikali ya Uganda imekiri kukabiliana na waasi hao tangu mwanzoni mwa wiki hii,wakati wanajeshi hao waliposhambuliwa na waasi wanaoongozwa na makamu wa zamani wa Rais Riek Machar.

Akisimulia kuhusu tukio hilo kwenye mkutano wa kikanda nchini Angola mnamo Jumatano, Rais Yoweri Museveni, alisema kwamba baadhi ya wanajeshi wake waliuawa au kujeruhiwa.

Jeshi la Uganda hata hivyo halijaeleza idadi kamili ya wanajeshi waliouawa.

Luteni Kanali Paddy Ankunda ametetea hatua ya Uganda kupeleka wanajeshi wake Sudan Kusini ikisema lengo lake ni kulinda raia na kufungua njia kwa misaada kuingizwa nchini humo.