POLISI WANNE WAFUKUZWA KAZI

ASKARI polisi wanne jijini Dar es Salaam wamefukuzwa kazi, kutokana na kile kilichodaiwa ni kujihusisha na vitendo vya uhalifu.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema kufukuzwa kwao kumetokana na uchunguzi uliofanyika na kubaini ushiriki wao katika matukio ya uhalifu, likiwemo la wizi la Machi 9, mwakahuu eneo la Mbezi Beach, Dar es Salaam.

Kova alitaja polisi hao, ambao kwa mujibu wake walifikishwa kwenye Mahakama ya Kijeshi kuwa ni Koplo Rajabu Mkwenda maarufu kama Ugoro, aliyekuwa Makao Makuu ya Polisi.

Wengine ni Konstebo Simon wa Kituo cha Kikuu cha Polisi, Konstebo Albernus Koosa wa Bendiya Polisi, Dar es Salaam na Konstebo Seleman wa Kituo cha Polisi Kigamboni. Kamanda alisema kabla ya kufukuzwa askari hao, walishitakiwa katika Mahakama ya Kijeshi na kupatikanana hatia.

Alisema jalada la kesi hiyo na majalada ya watuhumiwa wengine ambao ni raia, yatapelekwa kwa mwanasheria wa serikali, kabla ya kuwafikisha mahakamani kwa makosa ya jinai.

"Uchunguzi wa kina umefanyika na watuhumiwa 11 (wakiwemo polisi hao wanne) wamepatikana ndipo ilipobainika kwamba askari polisi hao walishiriki katika tukio hilo," alisema Kamanda Kova. Kwa mujibu wa kamanda, katika tukio hilo, raia wengine wanaotuhumiwa kwa ujambazi walikamatwa wakati wakitoroka baada ya gari lao kugonga mti.

Watuhumiwa hao ni Gerald Mtutu (36), Charles Mbelwa (37), Adam Mohamed (40), Ally Salum (38), Salum Mussa (22), Juma Hamis (29)na Juma Ngwele (50).

Inadaiwa siku hiyo Machi 9, walifika katika ofisi za kampuni ya Wachina ijulikanayo kama Hong Yang, inayojishughulisha na ujenzi na useremala.

Kamanda Kova alisema watuhumiwa walitambuliwa na mashahidi mbalimbali.

Kamanda alisema polisi haitavumilia vitendo vya ukiukwaji wa maadili ya utumishi wake.

Alisema hatua hizo ni fundisho kwa askari yeyote, atakaye jaribu kwenda kinyume na maadili ya kazi.

"Wamefukuzwa kwa fedheha na kawaida ukifukuzwa kwa fedheha huna stahili yoyote. Ikumbukwe kuwa tuko katika mpango wa maboresho kwa jeshi la Polisi kwa maana hiyo hatuwezi kuwa na watuambao ni wachafu ndani yetu," alisema.