MISHAHARA YA RAIS, MAKAMU NA MAWAZIRI KUPUNGUZWA KWA 20%

Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta, ameamuru maafisa wakuu watendaji wa mashirika ya serikali kukubali mishahara yao kukatwa kwa asilimia 20, la sivyo waachishwe kazi.

Akiongea kwenye kongamano la kitaifa kuhusu gharama kubwa ya matumizi ya serikali, Rais Kenyatta alisema kuwa hatua yake na naibu wake pamoja na baraza la mawaziri kupunguza mishahara yao kwa asilimia 20 haikuwa kwa sababu ya kufurahisha watu.Kadhalika Kenyatta ameongeza kusema kuwa uchumi wa nchi hauwezi kuwa mzuri ikiwa kila mtu anataka nyongeza ya mishahara badala ya kuzingatia kupunguza gharama ya maisha nauzalishaji wa bidhaa.

''Wakuu wa mashirika ya serikali watatakiwa kukubali mishahara yao kupunguzwa kwa asilimia 20. Kuna wakenya ambao wanaweza kushikilia nyadhifa hizo kwa pesa ndogo ikilinganishwa na zile wanazopata wakuu hao,'' aliongeza kusema Kenyatta.

Kenyatta amesema matumizi ya pesa za serikali ni ya juu mno na kwamba hayawezi kudhibitiwa ikiwa baadhi ya wafanyakazi wa sekta ya umma wataendelea kupata mishahara mikubwa.Rais alisema lazima safari za kwenda nje ambazo zinafanywa na baadhi ya wafanyakazi wa serikali, kupunguzwa. Wakati huohuo, Rais aliwataka wabunge kukubali mishahara yao kukatwa kwani ni baadhi ya wabunge anaopokea mishahara mikubwa duniani.

Swala la mishahara ya wabunge ni swala tete sana nchini Kenya.

Rais Kenyatta, alisema kuwa serikali inatumia kati ya dola dilioni 4.6 kwa mishahara ya wafanyakazi wa umma na kutumia dola bilioni 2.3 kwa maendeleo.