KIJANA MMOJA AMEKUFA BAADA YA KULIPUKIWA NA SIMU

ALI Bakari Ali (20) mkazi wa Kisima Majongoo mjini Unguja amekufa baada ya simu yake aliyokuwa akitumia ambayo ilikuwa imeunganishwa na chaja ya umeme kupata hitilafu.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Mkadam Khamis Mkadam alithibitisha kutokea kwa tukio hilo ambapo alisema Ali alikufa baada ya kupata mshtuko wa umeme unaotokana na simu yake iliyokuwa imewekwa katika chaja ya umeme huku akifanya mawasiliano.

"Ni kweli tumepata taarifa ya kifo cha kijana Bakari Ali ambaye alikuwa akisikiliza simu yake iliyokuwa imewekwa katika chaja ya umeme na kusababisha mshtuko mkubwa," alisema.

Kamanda Mkadam alitoa wito kwa wananchi na kuwataka wakati wanaposikiliza simu zao kwanza kuziondoa katika umeme ili kuepusha ajali.