ALIYEKUWA RAIS WA SIERRA LEONE AFARIKI DUNIA

Bwana Kabbah anasifiwa zaidi duniani kwa kurejesha amani nchini Sierra Leone baada ya mapigano ya wenyewe kwa wenyewe.

Amefariki nyumbani kwake akiwana miaka 82.

Alhaji Ahmad Tejan Kabbah alizaliwa February 16, 1932. Aliongoza Sierra Leone katiya mwaka wa 1996 hadi 1997 na kisha tena mwaka wa 98 hadi mwaka wa 2007.

Katika miaka mingi ya utu uzima wake, alihudumu kama mtaalamu wa uchumi na sheria. Alifanya kazi kwa miaka mingi na shirika la maendeleo la Umoja wa mataifa UNDP. Baada ya kujiuzulu kutoka umoja huo mwaka wa 92, alirudi zake nchini Sierra Leone na kujiingiza katika siasa za nchi hiyo.


*Maisha yake ya siasa

Mnamo mwaka wa tisini na sita, bwana Kabbah alichaguliwa kuwa kiongozi wa chama Sierra Leone's People's Party (SLPP) na kuwania urais kwa tikiti ya chama hicho mwaka wa 96.

Katika kinyanganyiro hicho, alishinda na kuwa rais kwa 59% ya kura na kumpiku mpinzani wake mkuu John Karefa-Smart wachama cha United National People's Party (UNPP) aliyepata 40% tu ya kura.

Waangalizi wa kimataifa walitangaza kuwa uchaguzi huo ulikuwa huru na wa haki.

Kikubwa atakachokumbukwa nacho ni hotuba yake ya kuapishwa mjini Freetown, alipoahidi kumaliza kabisa mapigano ya wenyewe kwa wenyewe, jambo alilotekeleza baada ya kuwa rais.

Bwana Kabbah ni wa kabila la Mandingo kiasilia na ndiye aliyekuwa rais wa kwanza wa kiislamu wa Sierra Leone. Alizaliwa katika kijijji cha Pendembu, wilaya ya Kailahun mashariki mwa Sierra Leone, japo udogoni mwake alikulia mji mkuu wa Free town.


*Utawala wa Kabbah

Sehemu kubwa ya uongozi wa Kabbah ilishawishiwa na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yaliyotokea nchini Sierra Leone kwa muda mrefu, huku akikumbwa na mapinduzi yamuda yaliyofanywa na wanamgambo wa United Front wakiongozwa na Foday Sankoh. Mapinduzi hayo yalim'ngoa madarakani kati ya Mei 97 hadi March 98.

Hata hivyo alirejeshwa madarakani kufuatia usaidizi wa kijeshi kutoka kikosi cha Jumuiya ya Kiuchumi ya Afrika Magharibi (ECOWAS) kilichoongozwa na Nigeria.

Awamu ya pili ya machafuko ya ndani na mauaji ilisababisha kuingiliwa na Umoja wa mataifa pamoja na Uingereza nchini humo mwaka wa 2000.


*Harakati za amani

Katika wadhifa wake kama rais, Kabbah alianzisha mazungumzo na wanamgambo hao wa RUF ili kumaliza mapigano hayo ya ndani. Alisaini mikataba kadhaa ya kusitisha mapigano na kiongozi wa waasi Foday Sankoh, ukiwemo ule mkataba wa mwaka wa 1999 wa mjini Lome' ambapo kwa mara ya kwanza waasi hao walitekeleza na kusitisha kabisa mapigano na mashambulio dhidi ya serikali.

Na pale mkataba huo ulipovunjika baadaye, Kabbah alifanya kampeini kuomba usaidizi kutoka Umoja wa Mataifa, Uingereza, Jumuiya ya ECOWAS na hata Muungano wa Afrika, AU ili kurejesha amani.

Kabbah alitagaza rasmi kumalizika kwa vita vya ndani vya Sierra Leone mwaka wa 2002. Maelfu ya raia wa Sierra Leone walikimbia katika barabara kuu zanchi hiyo kusherehekea hatimaye kupatikana amani.

Miaka michache baadaye Kabbah alipata ushindi wa rahisi sana kuongoza nchi hiyo kwa muhula mwingine wa miaka mitano alipopata 70% ya kura na kumpiku mpinzani wake mkuu Ernest Bai Koroma wa chama cha All People's Congress (APC). Hapopia, waangalizi wa kimataifa walitangaza uchaguzi kuwa huru na wa haki.