ZANZIBAR WATEKETEZA BIDHAA ZA CHAKULA TANI 25

Bodi ya Chakula, Dawa na Vipodozi imeangamiza bidhaa mbalimbali za chakula zipatazo tani 25 baada ya kubainika kuwa hazifai kwa matumizi ya Binadamu.


Bidhaa hizo ni pamoja na maziwa ya kopo aina ya NAN tani 7.4 soda za kopo, chama tani tano, tende tani 10, mchele tani 1.1 na vyakula mchanganyiko tani moja ambapo uangamizaji huo ulifanyika katika Maeneo ya Kibele Mkoa wa Kusini Unguja.

Mkuu wa ukaguzi wa Bodi hiyo,Aisha Suleiman alisema kuwa Bidhaa zote hizo zilizoangamizwa ni kufuatia ukaguzi unaofanyika kila siku kupitia Bandarini, Madukani pamoja na maghala yanayohifadhia bidhaa hizo.


Alifahamisha kuwa soda hizo zimeingizwa nchini zikiwa na tarehe iliyotengenezwa na hazina tarehe ya kumaliza muda wa matumzi jambo ambalo linaweza kuhatarisha afya za watumiaji.

Alisema kwa upande wa mchele ulioangamizwa umebaki kutokana kwa mchele huo kurejeshwa ulikotoka nchini Pakistan ambao ulikua tani 26 na uliobaki kuangamizwa.


Alisema gharama zote za uangamizaji wa vyakula hivyo kwa mujibu wa sheria ya Bodi ya chakula Dawa na Vipodozi mwenye mali yake ndio anaegharamia uangamizaji huo.

Amewataka wananchi kutoa taarifa kwa bodi hiyo endapo watatilia shaka bidhaa za aina yoyote ile kama vile za chakula, Dawa pamoja na vipodozi kwa lengo la kufanyiwa uchunguzi na kuepuka madhara kwa watumiaji.


Kwa upande wa wafanya biashara wametakiwa kuleta bidhaa zenye ubora kwa wananchi na kuepuka udanganyifu ambao unaweza kuleta madhara yanayopelekea kuleta athari kubwa kwa jamii.