IRAQ YAOMBA MSAADA


Majeshi ya angani ya MArekani kutumwa Iraq

Iraq imeomba rasmi usaidizi wa Marekani kushambulia kwa ndege wapiganaji wa kiislamu walioteka miji kadhaa nchini humo wiki hii.
"Tumepokea ombi kutoka kwa serikali ya Iraq kutumia ndege zetu huko,'' alithibitisha kamanda mkuu wa jeshi la Marekani Jenerali Martin Dempsey mbele ya baraza la senate.

ISIS waendeleza harakati zao

wapiganaji wa ISIS wameilemea serikali ya Iraq

Awali wapiganaji hao wa madhehebu ya Sunni walishambulia kiwanda kikubwa zaidi cha kusafishia mafuta nchini Iraq katika mji wa Baiji kaskazini mwa Baghdad.
Katika taarifa yake kwa taifa, waziri mkuu Nouri AL Maliki alitoa wito kwa raia wa Iraq waungane dhidi ya wanamgambo.
Vikosi vya jeshi vinajitahidi kuwakabili na kuwasukuma nje wanamgambo wa ISIS pamoja na washirika wao wa Ki-sunni kutoka mikoa ya Diyala na Salahuddin baada ya waasi hao kuteka mji wa Mosul wiki iliyopita.

Obama ataka kuisaidia Iraq

Na hapo Jumatano, rais Barack Obama alifanya kikao cha dharura na baraza la Congress kujadili mzozo wa Iraq.
Duru za ikulu ya White house zinasema kuwa Bwana Obama ''amependekeza kuongezwa juhudi zetu nchini Iraq na kusaidia majeshi ya serikali hiyo katika kukabiliana na wanamgambo wa ISIS ikiwemo uwezekano wa kuongeza usaidizi wa kiusalama''.

Baadhi wanapinga

Lakini kabla ya kufanyika mkutano huo, kinara wa baraza la Senatae wa Marekani Harry Reid, kutoka chama cha Demokrats alisema kuwa hakubaliani kamwe na wazo la kuihusisha Marekani katika ''vita vya ndani vya Iraq''.
Marekani imekuwa katika ubishi mkubwa katika mabunge ya Senate na Congress juu ya kuondolewa majeshi yao ndani ya Iraq na Afghanistan.