MORAVIAN WAPINGA HUDUMA YA WACHUNGAJI MASHOGA

HALMASHAURI Kuu ya Kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la Misheni Mashariki, limetoa tamko la kutounga mkono maazimio ya Kanisa la Moravian Jimbo la Marekani ya Kaskazini lililoruhusu huduma ya wachungaji mashoga na wasagaji.


Juni 22 mwaka huu, Sinodi ya Kanisala Moravian Jimbo la Amerika ya Kaskazini imeruhusu watu wenye uhusiano wa jinsia moja kubarikiwa katika daraja takatifu la uchungaji pamoja na kuruhusu viapo vya ndoa za jinsia moja kufungwa kanisani.


Katibu Mkuu wa Jimbo hilo, Mchungaji Emmaus Mwamakula alisema kuwa kanisa lake haliungi mkono maazimio hayo kutokana na kuwa vitendo hivyo ni kinyume na misingi, imani na mafundisho ya Kanisa la Moravian."


Kanisa limepata mashangao mkubwa taarifa za Sinodi ya Kanisa Moravian Jimbo la Amerika ya Kasikazini, ya kuruhusu huduma ya wachungaji mashoga na wasagaji na ndoa za jinsia moja kufungwa kanisani.


"Biblia Takatifu inatamka wazi vitendo vya ushoga na usagaji ni chukizo mbele za Mungu na watu wanaotenda hawataurithi ufalme wa Mungu na pia ni kinyume na tamaduni na imani ya kikristu na kuwa mamlaka ya mwisho kuhusu imani ni neno la Mungu (Biblia),"alisema.


Alisema kuwa kutokana na maazimio hayo ambayo ni chukizo mbele za Mungu, kanisa lake linasitisha uhusiano na Jimbo ya Amerika ya Kaskazini na kuwaombea ili viongozi wake wafikie hatua ya kufikiria toba.


Mwamakula alitoa wito kwa wakristo wa Mashariki na majimbo mengine ya kanisa hilo hapa nchini, kukataa kwa namna zote ushoga na usagaji pamoja na kuwakataa viongozi wanaoshikana na watu waliohalalisha ushoga katika majimbo yao.