MAJAMBAZI WAWILI WAUAWA NA WANANCHI

Watu wawili wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wakiwa katika jaribio la kutaka kupora fedha kwa mmoja wa wateja aliyekuwa ndani ya benki ya NMB tawi la uwanja wa ndege,wakiwa na pikipiki aina ya Boxer wameuawa na wananchi wenye hasira kali,huku jeshi la polisi kanda maalumu ya Dar-es-Salaam likiwashikilia watu watatu mmoja akiwa ni mganga aliyekuwa akiwatibu kwa nguvu za giza na kudai kuwapa nguvu.


Kamanda wa polisi kanda ya maalumu ya Dar-es-salaam, kamishana wa polisi Selemani Kova amesema kuwa, majambazi hao walipoteza maisha mara baada ya kipigo na kupoteza maisha wakiwa njiani kupelekwa hosipitalini, ambapo amesema katika tukio hilo majambazi hao walikutwa na bastola waliyotumia kurushiana risasi na polisi.


Jeshi la polisi limezitaka taasisi za kifedha kama mabenki na taasisi na watu binafsi kuacha mtindo wa kubebeba fedha kwa njia ya mifuko ya plastiki maarufu kama rambo, kubebea kwenye pikipiki na aina nyingine za usafirishaji fedha ambazo zinatoa vishawaisi kwa watu wasio na nia njema kuleta hujuma.


Baadhi ya wananchi walioshuhudia wameiambia ITV kuwa majambazi hao walikuwa wakikimbia hovyo huku wakirusha risasi hewani, ambapo wamerishukuru jeshi la polisi kwa kudumisha doria na kulitaka jeshi hilo kushirikiana na wananchi ili kuhakikisha kuwa vitendo vya uporaji hasa kwenye mabenki vinakomeshwa.


Chanzo:ITV