MWANASHERIA WA ZANZIBAR ALIA NA TUME YA PAMOJA YA FEDHA

MWANASHERIA Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), Othman Masoud Othman, amesema kushindwa kuanza kazi kwa Tume ya Pamoja ya Fedha ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,ndiyo chanzo kikubwa cha misuguano na kero za Muungano.


Othman alisema hayo katika Baraza la Wawakilishi, wakati alipokuwa akijibu hoja mbali mbaliza wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, waliokuwa wakitaka ufafanuzi wa kero za Muungano na ufumbuzi wake, ikiwemo sababu zakutoanza kazi kwa Tume hiyo.

Akifafanua zaidi, Othman alisema Tume huyo kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ibara ya 133, ndiyo yenyemamlaka ya kutunza fedha za Muungano wa Tanzania katika akauti maalumu.

"Fedha kwa ajili ya shughuli za Muungano zitakuwa zikilindwa na kuhifadhiwa katika akaunti hiyo kwa ajili ya matumizi ya mambo yaMuungano tu," alisema Othman.


Othman ambaye amekuwa mjumbe wa tume hiyo kwa muda mrefu sasa, alisema Sheria ya Kuundwa kwa Tume hiyo ya 1996, bado haijafanya kazi na kutekeleza majukumu yake ya kusimamia mwenendo wa kutunza fedha.

Alisema hajui sababu za tume hiyo kushindwa kutekeleza majukumu yake ya kutunza akaunti ya Muungano kwa matumizi ya taasisi za Muungano kwa mujibu wa Katiba.


Kwa mujibu wa Othman, kama Tume hiyo ingekuwa ikifanya kazi zake za kutunza akaunti ya fedha zaMuungano vizuri, kero za Muungano zinazojitokeza sasa zingekuwa historia.

"Chokochoko zinazotolewa katika Muungano ikiwemo matumizi mabaya ya fedha za Muungano katika upande mwengine, zingeondoka kama akaunti hii ingekuwa ikifanya kazi zake vizuri,"alisema.

Baadhi ya mambo yaliyomo katika orodha ya Muungano ni mambo yanje na ushirikiano wa kimataifa, ulinzi pamoja na mambo ya ndani.


Hivi karibuni akiwasilisha makadirio ya bajeti ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais kwa mwaka wa fedha 2014-2015, Balozi Seif Ali Iddi, alisema miongoni mwa kero za Muungano ambazo hazijapatiwa ufumbuzi hadi sasa ni kuanza kazi Tume hiyo.

Suala la kushindwa kufanya kazi kwa tume hiyo liliibuka katika Bunge Maalumu la Katiba, katika kikao chake kilichofanyika Dodoma miezi miwili iliyopita na kuibua mjadala mkubwa.