PUTIN AANDA MAJESHI YAKE

Rais Vladimir Putin wa Urusi ameviweka vikosi vyake vilivyoko nchini humo katika hali ya "tahadhari kamili ya vita" na kuwaamuru wanajeshi 65,000 katika eneo hilo kufanya luteka za kijeshi za wiki moja kuwa tayari kwa vita.


Waziri wa Ulinzi wa Urusi, Sergei Shoigu, amesema mazoezi hayo ya kijeshi ya angani na ardhini katika maeneo ya milima ya Volga na Ural yatafanyika kuanzia Jumamosi Juni 21 hadi Juni 28.

Jumuiya ya Kujihami ya NATO imesema mapema wiki hii kwamba Urusi imerudia tena kurundika wanajeshi wake kwenye mpaka na Ukraine ambapo waasi wanaotaka kujitenga wamekuwa wakipambana na vikosi vya serikali kwa wiki kadhaa katika mzozo uliogharimu maisha ya watu 300 na kuwapotezea makaazi wengine 34,000.


*Kusitisha uhasama

Hatua hizo za kijeshi zinakuja siku moja baada ya Rais Petro Poroshenko wa Ukraine kutangaza wiki moja ya usitishaji wa mapigano na waasi wanaoiunga mkono Urusimashariki ya nchi hiyo ikiwa ni sehemu ya mpango wa amani wa vipengele vinne ambao pia unajumuisha msamaha na ahadi ya kufanyika kwa marekebisho ya katiba.

Serikali ya Urusi imeishutumu mpango huo wa Poroshenko kuwa ni "amri" ambao hautopelekea kupatikana kwa ufumbuzi wowote ule na waasi wameukataa wito wake wa kuwataka wasalimishe silaha zao.


Chanzo:DW SWAHILI