UTEKELEZAJI HUKUMU YA MGOMBEA BINAFSI UTATA

Utata wa kisheria umeibuka kuhusu utekelezaji wa amri ya Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu kuhusu nafasi ya mgombea binafsi nchini.

Juni 14, 2013, Mahakama hiyo ilitoa amri ya kuitaka Serikali ya Tanzania kutoa taarifa ndani ya miezi sita kuhusu hatua ilizochukua kulingana na hukumu hiyo.
Wakati wanasheria wakieleza kuwa kitendo cha Serikali kushindwa kutekeleza amri hiyo kunaweza kuifanya nchi iwekewe vikwazo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alisema amri hiyo haiwezi kutekelezeka mpaka mchakato wa Katiba Mpya utakapokamilika.
Akizungumza jana, Jaji Werema alisema nchi haiwezi kuwekewa vikwazo vyovyote kwa kuwa tayari suala hilo lipo kwenye mchakato wa Katiba Mpya na kama ikishindikana iliyopo itafanyiwa marekebisho.
“Hakuna cha vikwazo wala nini… hilo suala kwa sasa liko kwenye mchakato wa Katiba unaoendelea, hatuwezi kurekebisha Katiba tena kwa hilo. Mnapaswa kuelewa hizi Mahakama za kimataifa, utekelezaji wa hukumu unategemea pia uwezo wa nchi husika. Sisi tuko kwenye mchakato wa Katiba, hadi ipatikane, isipopatikana ndipo tutaleta marekebisho. Mbona kuna marekebisho mengi tu yaliletwa lakini yanasubiri?”
Hata hivyo, Kaimu Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Harold Sungusia alisema: “Nchi haiwezi kutumia sababu zake za ndani ya nchi kama kisingizio cha kutotekeleza masharti ya mkataba iliyoridhia yenyewe kwa hiari na kwa nia njema.”
Mwanasheria kutoka Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Steven Msechu alisema japo Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu haina jeshi la kuilazimisha Serikali kutekeleza hukumu hiyo, bado itabanwa katika vikao vya nchi za Umoja wa Afrika... “Mahakama hiyo itapeleka ripoti kwenye Baraza la Marais wa Umoja wa Afrika kuonyesha kuwa Tanzania imeidharau... Baraza la Mawaziri wa Afrika nalo litapewa taarifa kama hiyo, hivyo marais na mawaziri husika watahojiwa kwa nini wameshindwa kutekeleza.”
Hata hivyo alisema Serikali inaweza kujitetea kuwa imeshaliweka suala hilo kwenye Rasimu ya Katiba hivyo liko kwenye mchakato.
Mchungaji Mtikila, TLS na LHRC walishinda kesi hiyo waliyofungua katika Mahakama hiyo baada ya kushindwa katika rufaa iliyofunguliwa na upande wa Serikali kupinga suala la mgombea binafsi.
Katika hukumu iliyosomwa na Rais wa Majaji wa mahakama hiyo, Sophia Akuffor Arusha hivi karibuni, Serikali italazimika kutekeleza kwa vitendo hukumu hiyo.