NMB YAVUNA BILLION 45

Benki ya NMB imeingiza faida ya Sh134 bilioni mwaka jana na kutoa gawio la Sh45 bilioni kwa wanahisa wake.

Faida hiyo ya mwaka jana ni sawa na ongezeko la asilimia 37 la faida iliyopatikana mwaka 2012.


Mwaka 2012 benki hiyo ilitoa gawiola jumla ya Sh34 bilioni kwa wanahisa huku kila hisa ikipata Sh68 baada ya benki hiyo kupata faida ya Sh97 bilioni.

Akitoa taarifa katika mkutano mkuuwa mwaka wa wanahisa wa benki hiyo, mtendaji mkuu wa NMB, Mark Wiessing alisema mwaka huu gawio la kila hisa litakuwa Sh90.


Huo ulikuwa mkutano wa sita tangubenki hiyo iandikishwe katika Soko la Hisa la Dar es Salaan (DSE),mwaka 2008.

"Tuna furaha kwamba benki yetu imeendelea kuvuna mafanikio mwaka hadi mwaka. Tutaendelea kutoa huduma bora kwa kutumia teknolojia ili kuwavutia wateja zaidi," alisema.


Wiessing alisema mwaka 2013 benki hiyo ililipa kodi ya mapato jumla ya Sh422 bilioni ikiwa ni ongezeko la asilimia 18 ikilinganishwa na mwaka 2012.

Mikopo iliyotolewa kwa mwaka 2013 ilikuwa ni Sh1,614 bilioni sawa na ongezeko la asilimia 20 ya mikopo iliyotolewa mwaka 2012 na benki hiyo.


Alisema mafanikio hayo yanatokana na huduma zinazotolewa na benki hiyo hasa ikizingatiwa kwamba benki hiyo inaongoza kwa kuwa na wateja wengi zaidi.

Mtendaji huyo mkuu alisema asilimia 40 ya Watanzania wenye akaunti benki ni wateja wa NMB, huku asilimia 60 wakiwa ni wateja kutoka katika benki mbalimbali nchini.


Katika taarifa yake, mwenyekiti wa bodi ya NMB, Profesa Joseph Semboja aliwapongeza wateja, wadau na wanahisa wa benki hiyo kwa kuchangia mafanikio yaliyopatikana mwaka uliopita.

" Tunatarajia kuendelea kupata faida mwaka huu kutokana na utendaji uliotukuka," alisema.