CHADEMA WAMKALIA KOONI SILAA

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimempa siku 21 Diwani wa Ukonga, Jerry Silaa, kutoa maelezo ziliko fedha za ujenzi wa ofisi ya kata zaidi ya sh. milioni 175.

Chama hicho kimesema endapo Silaa ambaye pia ni Meya wa Manispaa yaIlala hatafanya hivyo, kitaungana na wananchi na kufanya maandamano kuelekea Ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Ilala kudai haki yao.


Kauli hiyo ilitolewa jijini Dar es Salaam jana na Katibu wa CHADEMA Jimbo la Ukonga, Juma Mwipopo, wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Stendi, Gongolamboto.

Alisema wamefikia hatua hiyo baada ya kubaini kuwa katika kipindi cha miaka miwili haijulikani fedha hizo zimepelekwa wapi huku kata hiyo ikiendelea kupanga kwenye nyumba ya watu.


"Ni jambo la kushangaza kusikia ofisi inajengwa, lakinisisi tunajua hata kiwanja kwa ajili ya ujenzi huo hakipo, ndiyo maana tunamtaka Silaa atuambie unafanyika katika kiwanja kipi au fedha hizo wamezipeleka wapi," alisema.

Mwipopo, alisema akiwa Mwenyekiti wa Maendeleo wa Kata, meya huyo, amekuwa mstari wa mbele katika uvunjaji wa kanuni ya majukumu ya udiwani inayomtaka kutoa taarifa kwa wapiga kura kuhusu fedha zinazotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo.