MOSHI WALETA TAFRANI KATIKATI YA JIJI

Taharuki na hofu ya moto imewakumba wakazi wa jiji la Dar es Salaam maeneo ya katikati ya jiji kufuatia Moshi mkubwa uliokuwa ukitoka katika mojawapo ya majengo ya benki kuu ya Tanzania na kusababisha baadhi ya wakazi hao pamoja na jeshi la polisi akiwemo kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa kipolisi wa Ilala kufika haraka katika eneo la tukio kutokana na hofu ya kuungua kwa benki hiyo.

Taarifa za awali ambazo zilianza kusambaa zilikuwa zikidai kuwa ni hoteli ya Kilimanjaro Kempisk ndio iliyokuwa ikiungua na kusababisha waandishi wa habari pamoja na baadhi ya wakazi wa jiji kufika katika eneo hilo na baadae kubaini moshi mkubwa ukifuka kutoka katika mojawapo ya majengo ya benki kuu ya Tanzania ambapo baadhi ya askari wa jeshi la polisi pamoja na wananchi wamekusanyika kuishuhudia hali hiyo.
Kitambo kidogo baada ya wananchi kukusabyika baadae kikosi cha zimamoto nacho kikawasili katika eneo la tukio tayari kabisa kukabiliana na hatari ya moto ambapo hata hivyo walilazimika kuondoka katika eneo la tukio huku kiongozi wa msafara huo aliyejitambulisha kwa jina la sifuri simba akidai kuwa wamepata taarifa ya uwepo wa tukio la moto katika benki kuu.

Kamanda wa polisi mkoa wa kipolisi wa Ilala Marietha Minangi ameviambia vyombo vya habari kuwa hakuna tukio lolote la ajali ya moto bali ni jenereta la benki hiyo lilikuwa likijiwasha mara baada ya kukatika kwa umeme wa Tanesco.

Hata hivyo maelezo ya kamanda huyo yanatofautiana na maelezo ya mmoja wa walinzi wa benki hiyo ambaye hakutaka kupigwa picha wala kutaja jina lake kuwa moshi huo umesababishwa na zoezi la kawaida la kusafisha mtambo ambao hata hivyo alikataa kuutaja mtambo huo uliokuwa ukisafishwa ni wa shughuli gani.