KOCHA MKUU WA ITALIA CESARE PRANDELI KUSHUHUDIA UFUNGUZI WA MAPINDUZI CUP

KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Taifa ya Italia, Cesare Prandeli anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa michuano ya soka ya Kombe la Mapinduzi inayotarajiwa kutimua vumbi Januari mosi.

Mechi ya ufunguzi itakayoshuhudiwa na kocha Prandelini kati ya Simba na FC Leopard ya Kenya itakayochezwa saa mbili usiku kwenye Uwanja wa Amaan.

Kabla ya mechi hiyo, jioni ya siku hiyo kutakuwa na mechi kati ya wenyeji KMKM na KCC ya Uganda. Hayo yamebainishwa na Msemaji wa Kamati ya michuano hiyo, Farouk Kareem alipozungumza na waandishi wa habari jana.

Alisema kuwa uamuzi wa kumualikakocha huyo kuwa mgeni rasmi, umefikiwa kwa pamoja na viongozi wa kamati hiyo waliokutana juzi visiwani Zanzibar.

Alisema maandalizi kwa ajili ya michuano hiyo yamekamilika na timu zote kutoka nje ya Zanzibar zinatarajiwa kuwasili Desemba 30.

Alisema kuwa Kamati imeamua kumuita kocha huyo kuwa mgeni rasmi kutokana na mafanikio yake makubwa katika soka nchini kwake ambayo yanaonekana ulimwenguni kote.

Aidha alisema kuwa pamoja na kumteua kocha huyo kuwa mgeni rasmi pia kamati hiyo imefanya marekebisho ya michezo ya uwanja wa Gombani ambayo yalionekana kuzibana sana timu katika michezo yao.

Alisema kuwa katika marekebisho hayo michezo yote ya Pemba itachezwa mmoja kwa siku ambapo siku ya kwanza kutakuwa na mchezokati ya Clove Stars na Mbeya City nasiku itakayofuata Chuoni atacheza na URA ya Uganda.

Jumla ya timu 12 zinatarajiwa kushiriki katika michuano hiyo ambayo itachezwa katika vituo viwili, huku bingwa mtetezi ni AzamFC ya Dar es Salaam.