DADA AMSAIDIA KAKA KUMNAJISI MSICHANA WA MIAKA 12

MKAZI wa mtaa wa Tambukareli wilayani Mpanda, Helen Simon (20)anashikiliwa Polisi na kaka yake, Afred Mnyonge (24) kwa tuhuma za kumsaidia kaka huyo kumnajisi msichana jirani yao, mwenye umri wa miaka 12.

Akizungumza kwa njia ya simu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi, Kamishina wa Polisi, Dhahiri Kidavashari, alidai msichana huyo alinajisiwa juzi saa tatu usiku.

Akisimulia mkasa huo, Kamanda Kidavashari alisema usiku huo wa tukio, mtuhumiwa Helen alifika nyumbani kwa msichana huyo aliyekuwa akiishi na shangazi yake, Kibena Hussen na kumtaka msichana huyo amsindikize sehemu ambayo hakuitaja.

Inadaiwa kuwa msichana huyo huyo pasipokuwa na shaka wala wasiwasi wowote, alimsindikiza Helen hadi nyumbani kwa kaka yake huyo na wote wakaingia ndani ya nyumba hiyo."Muda mfupi baadaye Helen alimtaka msichana huyo asiondoke bali amsubiri kidogo kwa kuwa alikuwa anaenda wuani kujisaidia ndipo alipotoka na kufunga mlango wa nyumba hiyo kwa nje".

Msichana huyo baada ya kugundua kuwa mlango wa nyumba hiyo umefungwa kwa nje alianza kupiga mayowe ya kuomba msaada lakini hakuna jirani aliyejitokeza kumsaidia, alibainisha Kidavashari.

Kwa mujibu wa kamanda Kidavashari mtuhumiwa Alfred alimkamata kwa nguvu na kumbaka huku akiwa ameuziba mdomo wa msichana huyo kwa kipande cha nguo.

Inadaiwa baada ya kumfanyia msichana huyo unyama huo alimwamuru aondoke nyumbani kwake ndipo alitoka na kurejea nyumbani kwa shangazi yake ambapo alimkuta akiwa bado macho, hajalala ambapo alimsimulia mkasa mzima uliomkumba.

Inadaiwa shangazi ya msichana huyo aliongozana na binti huyo hadi Kituo cha Polisi mjini Mpanda ambapo alipewa fomu PF 3 ambapo msichana huyo alipata matibabu kwenye Hospitali ya Wilaya ya Mpanda na baadae akaruhusiwa kurejea nyumbani.

Kwa mujibu wa Kamanda wanandugu hao wanatarajiwa kufikishwa mahakamani wakati wowote mara tu uchunguzi wa awali wa shauri lao litakapo kamilika.