BUNGE LA KATIBA KUDHIBITIWA KIDIGITALI

BUNGE Maalumu la Katiba, limeanza chini ya mfumo wa kidijitali ambao pamoja na masuala mengine, vipaza sauti vyote viko chini ya udhibiti wa Mwenyekiti hali ambayo haitaruhusu mbunge kuvitumia bila ridhaa ya kiti. Hayo yalifahamika jana bungeni mjini hapa, wakati Sekretarieti ikitoa maelekezo kwa wajumbe kuhusu ukaaji na jiografia ya ukumbi.

Aidha wajumbe wamehakikishiwa kuwepo usalama wa kutosha huku wakiambiwa wakubaliane na upekuzi wa hali ya juu unaofanyika kutokana na mazingira ya sasa ambayo suala la usalama ni tata.

Chini ya usimamizi wa Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah na Katibu wa Baraza la Wawakilishi, Yahya Khamis Hamad, ilielezwa, Mwenyekiti wa Bunge Maalumu sasa anao uwezo wa kuzima kipaza sauti za mjumbe akiwa mezani kwake.

"Sauti ya kaa chini ikisikika, ukitaka kuendelea kuzungumza, sauti haitasikika," alisema Kaimu Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari (IT), Didas Wambura.


Kutokana na mfumo huo, kipaza sauti cha kwanza kikishawashwa, kinaonesha rangi nyekundu. Wengine wakiwasha, wanaoneshwa rangi ya kijani kuashiria kwamba wasubiri. Viashiria hivyo vinakuwa kwenye kiti ambaye anavitumia kuruhusu wazungumzaji.

Mfumo utaweza? Hata hivyo muda mfupi baada ya wataalamu kuwasilisha maelekezo, walipopewa muda wa kuuliza maswali au kupata ufafanuzi, walijitokeza wajumbe wengi waliotaka kuzungumza ambao baadhi, baada ya kudhibitiwa na mfumo, walipaza sauti bila kutumia vipaza sauti wakitaka wapewe nafasi.

Wakati huo huo Wambura alisema kila mjumbe ana kadi inayomwezesha siyo tu kufungulia mlango, bali kutumia katika kuzungumza kupitia vipaza sauti hivyo na pia inamwezesha kupiga kura.

Kaimu Mkuu wa Usalama wa Bunge, Peter Magati alisema wameongeza vituo vya upekuzi na akaomba wajumbe wakubaliane nahali hiyo.

"Mazingira ya sasa hivi ya hali tata ya usalama ndiyo sababu ya upekuzi wa namna hii," alisema.

Aliendelea kusema, "tumejiandaa kuhakikisha mnakaa kwa amani na utulivu ndani na nje ya Bunge." Kuhusu wageni, alisema watakuja kwa taarifa na akataka wajumbe kuhakikisha wageni wao wanakuwa katika mavazi ya staha yasiyo na walakini.

Masuala mengine waliyohakikishiwa wajumbe, ni umeme kutokatika.

Sanjari na hilo, Mkuu wa Wakala waSerikali Mtandao, Dk Jabir Bakar alisema pia ipo Wavuti ya Bunge Maalumu itakayokuwa ikirusha shughuli zote za Bunge moja kwa moja sanjari na Televisheni ya Taifa (TBC).

Huduma za matibabu zinapatikana katika hospitali iliyoko bungeni na ikitokea matibabu yakashindikana, mjumbe anaruhusiwa kwenda hospitali nyingine ya Serikali au binafsi kwa ushauri wa daktari na gharama za matibabu zitarudishwa.

Aidha wajumbe wamepewa orodhaya hoteli huku wakiaswa kutokwenda maeneo yanayohatarisha maisha yao.

Posho Taarifa ya Mhasibu Mkuu waBunge ilieleza kwamba licha ya wajumbe kulipwa posho ya kujikimu kila siku huku posho maalumu ikilipwa kwa wiki, vile vile wenye wasaidizi watalipwa posho ya kujikimu.


Malipo mengine wanayopewa wajumbe ni gharama za usafiri ambazo zitarejeshwa baada ya mhusika kuwasilisha tiketi ya usafiri aliotumia. Pia upo utaratibuwa kurudisha mafuta kwa waliotumia usafiri binafsi. Wajumbe wenye watoto wachanga wameambiwa wawasiliane na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu kwa ajili ya kupewautaratibu juu ya eneo la kutolea huduma.

Ukaaji ndani ya ukumbi huo wenyeviti 676, umezingatia majina, wenye mahitaji maalumu hususaniwenye ulemavu na pia wenye mahitaji maalumu ya kiusalama kama vile Waziri Mkuu.

Wajumbe Baada ya maelekezo kutolewa ukumbini, baadhi ya wajumbe walilalamikia masuala mbalimbali, wakiwemo wenye ulemavu waliotaka mazingira rafikikwao ikiwemo kuwepo wakalimani kwenye televisheni.

Vile vile suala la usawa wa jinsia katika uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu wake, lilijitokeza kutoka miongoni mwa wajumbe.


Mjumbe wa kwanza kusimama alikuwa Tundu Lissu, ambaye alitaka ufafanuzi kutokana na kile alichosema baadhi ya nyaraka muhimu hazimo kwenye makabrasha. Mwingine, Mussa Ali Kombo, alilalamikia posho akisemawapo waliofika Februari 16 mwaka huu lakini hawakujisajili jambo ambalo limewanyima posho ya kujikimu. Alitaka wafikiriwe kupatiwa posho hiyo.

Ernest Kimaya alitaka kufahamu iwapo wenye ulemavu watapatiwa maandishi makubwa. Kwa upande wake, Amon Mpanju alihoji kama kutakuwepo wakalimani wa lugha za alama ili watu walio kundi hilo wafuatilie yanayojadiliwa kwenye Bunge.

Naye Julius Mtatiro alihoji kuhusu stahiki za wajumbe akitaka posho maalumu wanayopewa, viwango vitajwe waelewe. Kwa upande wake, Kangi Lugora alitaka wagawiwe mapema rasimu ya Kanuni za Bunge hilo."Iko tabia ya kuuziwa mbuzi kwenye gunia…tugawiwe haraka.

Lazima tuwe na muda wa kutosha. Mpaka kieleweke mimi sitoki bila kuwa na kanuni," alisema.

Hata hivyo Katibu wa Bunge, Dk Kashililah alisema suala la kanuni inabidi kusubiri apatikane Mwenyekiti wa Muda ambaye ndiye mwenye jukumu la kuandaa kanuni.

Akizungumzia usawa wa kijinsia katika kupata Mwenyekiti na Makamu wake, Kashililah alisema uchaguzi huo ni suala la kisheria."Mnatubebesha mzigo tu, naliacha kwa mtaalamu," aliwaambia wajumbe. Kuhusu maandishi makubwa na wakalimani kwa wenye ulemavu, Katibu wa Bunge alisema huduma hizo zitapatikana mkutano utakapoanza.

Aidha kuhusu hoja ya Lissu, Kashililah alikubaliana naye na akasema nyaraka zinaendelea kuchapishwa na kabla ya kuanza kupitia rasimu ya katiba, zitakuwa zimepatikana.

Akijibu aliyelalamikia posho, Kashililah alisema ambao hawakulipwa posho ya kujikimu lakini walifika DodomaFebruari 16 wawasilishe uthibitisho.