Taifa Stars Kuelekea Ethiopia Leo

Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inatarajia kuondoka leo (Mei 26
mwaka huu) usiku kwenda Addis Ababa, Ethiopia ambapo itaweka kambi na
kucheza mechi moja ya kirafiki kabla ya kwenda Morocco.

Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itaondoka saa 5 usiku kwa
ndege ya EgyptAir ikiwa na kikosi cha wachezaji 21 chini ya nahodha wake
kipa Juma Kaseja.

Timu hiyo ikiwa Ethiopia, Juni 2 mwaka huu itacheza mechi ya kirafiki dhidi
ya Sudan ambapo siku inayofuata itaondoka kwenda Marrakech, Morocco kwa
kupitia Cairo, Misri. Mechi hiyo ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya
wenyeji Morocco itachezwa Juni 8 mwaka huu jijini Marrakech.

Mbali ya nahodha Kaseja, wachezaji wengine wanaoondoka katika kikosi hicho
ambacho kina wiki sasa tangu kingie kambini jijini Dar es Salaam ni Mwadini
Ally na Ally Mustafa ambao wote ni makipa.

Wengine ni Shomari Kapombe, Kevin Yondani, Aggrey Morris, Haroub Nadir,
Mwinyi Kazimoto, Frank Domayo, Mrisho Ngasa, Khamis Mchana, Amri Kiemba,
Salum Abubakar, Simon Msuva, John Bocco, Vicent Barnabas, Mudathiri Yahya,
Athuman Idd na Haruni Chanongo.

Wachezaji Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu ambao wako na timu yao ya TP
Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo watajiunga moja kwa moja na
Stars jijini Marrakech, Juni 4 mwaka huu wakitokea Maputo, Msumbiji mara
baada ya mechi yao ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Liga Muculumana ya huko.

Katika msafara huo wa Ethiopia benchi la ufundi la Stars linaundwa na Kim
Poulsen (Kocha Mkuu), Sylvester Marsh (Kocha Msaidizi),Juma Pondamali
(Kocha wa makipa), Leopold Tasso (Meneja wa timu), Dk. Mwanandi Mwankemwa
(Daktari), Frank Mhonda (Mtaalamu wa tibamaungo) na Alfred Chimela (Mtunza
vifaa).