JAMAA ANUSURIKA KIFO BAADA YA KUJITOSA MAJINI KUTAFUTA BAISKELI

Mtu mmoja amenusurika kifo kwa kujinusuru katika kichaka katikati ya maji yanayo kwenda kasi akisubiri kuokolewa katika eneo la ruvu mkoani Pwani baada ya kuzidiwa nguvu na maji alipojitosa kwenye maji kwa nia ya kutafuta baiskeli yake huku hali ya usafiri ikitarajiwa kurejea katika hali yake ya kawaida baada ya maji kupungua huku wakandarasi kutoka Tanroad wakihangaika kutengeneza maeneo yaliyoharibiwa na mvua.

Wakisimulia tukio hilo mashuhuda wamesema kuwa mtu huyo alijitosa mwenyewe kwenye maji kwa nia ya kutafuta baiskeli yake aliyodai imesombwa na maji na kisha kuzidiwa nguvu na kasi ya maji katika eneo hilo na kisha kunasa katika kichaka akisubiri kuokolewa huku baadhi ya mashuhuda wakiwa kando wasijue la kufanya kumnusuru.

Katika tukio jingine limeshuhudiwa msururu mkubwa wa magari ukisubiri kupita katika eneo la mto ruvu ambapo baadhi ya wasafiri waliokwama katika eneo hilo wakielezea tabu wanayoipata pamoja na kuwa na hofu ya kuibuka maradhi kutokana na wingi wa watu wanaojisaidia hovyo katika vichaka.

Aidha maji yaliyokuwa yamefunika barabara katika eneo la daraja la mto Ruvu yamepungua huku magari nayo yakiruhusiwa kupita moja moja wakati makandarasi kutoka tanroads wakiendelea kukarabati eneo ambalo lilimong`onyolewa na maji huku eneo zima linalozunguka mto ruvu likiwa limezungukwa na maji na baadhi ya wakazi wa eneo hilo wakioneka kutega nyavu bila kujali hatari inayoweza kuwapata.

Akizungumza katika eneo la tukio kamanda wa polisi mkoani Pwani Ulrich Matei amesema licha ya msongamano mkubwa wa magari hali ya usala katika eneo hilo ni kubwa kutokana na kupata msaada kutoka kwa vijana wa JKT Ruvu na kwamba katika kipindi kifupi kijacho hali ya usafiri itarejea katika hali yake ya kawaida.