CHINA NA MAREKANI WALAANI MAUWAJI S.KUSINI

China na Marekani zimelaani ghasia zinazoendelea nchini Sudan, kufuatia shutuma kwamba wapiganaji waasi waliwauwa mamia ya raia katika mji wenye utajiri wa mafuta wa Bentiu.


Waziri wa mambo ya nchi za nje wa China amezitaka pande zote husika kwenye mzozo huo kufanya mazungumzo ya kisiasa na kuwataka maafisa wa Sudan Kusini kulinda maslahi ya Uchina.

Uchina ni muwekezaji mkuu katika sekta ya mafuta Sudan kusini.

Ikulu ya White house imeelezea ghasia nchini Sudan kama zisizokubalika nakwamba zinakiuka imani ya raia wa Sudan Kusini waliyokua nayo kwa viongozi wao.


Kadhalika Marekani imesemakuwa imeshangazwa na mauaji ya kinyama ya mamia ya raia Sudan Kusini na kutoa wito wa kusitishwa kwa msururu wa vurugu zinazoendelea nchini humo.

Umoja wa mataifa ulisema siku ya Jumatatu kwamba waasi waliwauwa mamia ya raia katika mji wa Bentiu na wengi walikufa katika msikiti mmoja, hosipitali na kanisa ambako walikuwa wamekimbilia kutafuta usalama.


Msemaji wa ikulu ya White House, Jay Carney, amesema kuwa rais, Salva Kiir, na kiongozi wa waasi ni sharti watangaze hadharani kuwa mashambulizi dhidi ya raia haya kubaliki.

Maelfu ya watu wamefariki dunia tangu mapigano ya kikabila yazuke mwezi Disemba mwaka uliopita.