BABA AUA MTOTO KWA MAKONDE

Watoto wawili wamefariki dunia katika matukio mawili tofauti likiwamo la mtoto wa miaka mitatu aliyepoteza maisha baada ya baba yake kumchakaza kwa makonde.

Mtoto aliyefariki baada ya kipigo hicho ni Vanesa Njojowa wa Kijiji cha Isisi wilayani Mbarali mkoani hapa.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi alisema tukio hilo lilitokea saa 5:00 usiku wa kuamkia jana baada ya kuzuka kwa vurugu katika familia.


Msangi alisema baba wa marehemu ambaye ana umri wa miaka 23 alizusha vurugu kubwa kwa mkewe na baadaye aliamua kutoa kipigo kwa mtoto na kusababisha kifo.

Baba huyo anashikiliwa polisi wakati mwili wa marehemu ulitarajiwa kuzikwa jana baada ya polisi na madaktari kufanya uchunguzi.


Katika tukio jingine, Msangi alisema mtoto anayekadiriwa kuwa na umriwa kati ya miaka minne na mitano, Festo Mbiga alifariki dunia baada ya kugongwa na lori eneo la Nsalaga Uyole jijini hapa.


Mtoto huyo aligongwa juzi alipokuwa akikatisha barabara na kwamba polisi wanachunguza chanzo cha ajali hiyo.