MKUU WA MAJESHI ANUSURIKA KIFO SOMALIA

Mkuu wa jeshi la Somalia ameponea chupuchupu kuuawa mjini Mogadishu.

Hili ndilo shambulio la punde zaidi katika msururu wa mashambulio dhidi ya viongozi wa serikali na rasilimali za serikali nchini humo.

Gari lake Jenerali Dahir Aden Elmim lilirushiwa bomu katikabarabara kuu karibu na afisi za wizara ya ulinzi mjini Mogadishu.

Aliponea kwa sababu yeye huendesha mojawepo ya magari machache yaliyo na uwezo wa kudhibiti shambulio la risasi, ambayo yametengewa viongozi wakuu wa serikali hiyo.

Hakuna yeyote aliyedai kuhusika na shambulio hilo kufikia sasa japo inafahamika kuwa kundi la Al shabaab limekuwa likifanya mashambulio ya mara kwa mara mjini Mogadishu.

Mwishoni mwa juma, watu 15waliuawa katika shambulio lililolenga jengo la bunge la Somalia.

Wengine wengi walijeruhiwa wakiwemo wabunge 3.