WALIOIBA NMB WAHUKUMIWA MIAKA 37 JELA NA VIBOKO 24

WATU watano wamehukumiwa kifungo cha miaka 37 jela na kuchapwa viboko 24 kila mmoja baada ya kupatikana na hatia ya kuvamia na kupora fedha benki ya NMB tawi la Maswa kwa kutumia silaha.

Hukumu hiyo ilitolewa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Shinyanga na kusikilizwa na Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Neema Gasabile ambapo alitoa hukumu hiyo.

Aliwahukumu kifungo cha miaka 37 na viboko 24 kila mmoja viboko 12 wakati wa kuingia na 12 wakati wa kutoka baada ya kuridhika na ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashitaka kuwa kwa pamoja walitenda kosa hilo kinyume cha sheria.

Washitakiwa hao ni Kapama Hamis Ramadhan (37), Mussa Athuman Buberwa (38), Amos Mathayo, LucasVincent Mabela (40) na Zainabu Mchau (60) wote kwa pamoja walipatikana na hatia ya makosa tisaya jinai.

Mbele ya Hakimu mkazi wa mahakama hiyo, Mwendesha Mashitaka Mwanasheria wa Serikali Edith Tuka aliieleza mahakama hiyo kuwa washitakiwa wote kwa pamoja walitenda kosa hilo majira ya saa 6:00 mchana Julai 5, mwaka 2010 mjini Maswa.