JOHN MNYIKA AKUSUDIA KUMSHITAKI WAZIRI MKUU MIZENGO PINDA

Mh. John Mnyika anakusudia kumshtaki mahakamani Waziri Mkuu Mh. Mizengo Pinda kwa kosa la ofisi yake kushindwa kutangaza tarehe pamoja na maadalizi ya uchaguzi wa serikali za mitaa.

Akizungumza Jijini Dar es Salaam huku akiwa ameambatana na mwanasheria wake, Mh. Mnyika amesema moja ya hoja zilizomo katika shauri watakalofungua kuwa ni kutaka mahakama imlazimishe waziri mkuu Mh. Pinda, atoe kanuni pamoja na kutangaza ni lini uchaguzi huo utafanyika baada ya kile alichodai kuwa ni kuwepo kwa kimya kirefu kuhusu kufanyika kwa uchaguzi huo.

Mh. Mnyika amesema kuwa kwa mujibu wa sheria, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali zaMitaa inatakiwa itangaze pamoja na kutoa kanuni za uchaguzi huo miezi miwili kabla ya mwezi Oktoba na kwamba kitendo cha ofisi hiyo kukaa kimya hakileti tafsiri sahihi juu ya hatma ya uchaguzi huo.

Mbali ya kutaka waziri mkuu atangaze kanuni na siku ya kufanyika kwa uchaguzi wa serikali za mitaa, Mnyika amesema katika hoja zake ataiomba mahakama iitake serikali ibadilishe taratibu na sheria zinazosimamia uchaguzi huo ili uwe huru na wa haki.