KUPATA URAIA MPAKA MIAKA 15 YA NDOA

KAMATI Namba Tatu ya Bunge Maalumu la Katiba imependekeza mtuyeyote anayetaka uraia wa kuandikishwa baada ya kufunga ndoa na Mtanzania, asipewe uraia huo mpaka adumu katika ndoa husika kwa miaka 15.

Akisoma maoni ya wengi kutoka kwenye Kamati Namba Tatu bungeni jana, Dk Francis Michael alisema kamati hiyo imependekeza kuwa Ibara ya 58 inayozungumzia uraia wa kuandikishwa ni vyema mmoja wa wanandoa awe na sifa ya kuomba uraia baada ya kukaa kwenye ndoa kwa muda huo.Dk Michael alisema Ibara ya 58 inayozungumzia uraia wa kuandikishwa, ni vyema mmoja wawanandoa kuwa na sifa ya kuomba uraia baada ya kukaa kwenye ndoa kwa muda huo.

Lengo la hatua hiyo ni kuondoa udanganyifu wa watu kutumia mwanya wa ndoa, kupata uraia na kisha kupata haki za kumiliki ardhi na rasilimali zingine.

Kamati Namba 10 pia ilitoa pendekezo katika ibara hiyo, ambapo Mwenyekiti wake Anna Abdallah, alisema kamati hiyo imependekeza haki ya mwanandoa kupewa uraia, itekelezwe baada ya kudumu katika ndoa miaka saba.

Rasimu ya Pili ya Katiba, iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilitambua wakazi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wenye sifa za kisheria kuomba uraia wa kuandikishwa, ikiwemo mtu aliyefunga ndoa awe amedumu katika ndoa kwa kipindi cha miaka mitano mfululizo.

Aidha, kamati nyingi zimeonesha kuunga mkono pendekezo kumpa hadhi maalumu, Mtanzania aliyekana uraia wake mara anaporejea nchini, ingawa zimepinga kuwepo kwa uraia pacha.

Rasimu inampa hadhi maalumu mtu wenye asili au na saba ya Tanzania na ambaye ameacha kuwaraia wa Tanzania kwa kupata uraia wa nchi nyingine, wanapokuja Tanzania kwa masharti yatakayo ainishwa na sheria za nchi.

Licha ya kutoa maelezo kuwa kamati yake inatambua uraia pacha, Abdallah alisema wanapendekeza sheria inayoainisha sifa na masharti ya mtu huyo anaporejea nchini.

Masharti hayo ni suala zima la umiliki wa rasilimali, ambapo pia kamati hiyo imependekeza watu hao kutoshiriki mchakato wa uchaguzi kwa kuchagua au kuchaguliwa.

Akiwakilisha maoni ya wachache katika Kamati Namba 10, Said Arfi alisema wachache pia waliunga mkono kifungu hicho, ili kuimarisha umoja, amani, uzalendo na usuala zima la usalama wa nchi.