HOTEL YA BLUE PEARL YAFUNGWA, YADAIWA TSH MIL 639

KAMPUNI ya Udalali ya Majembe Auction Mart, imeifunga Hoteli ya Blue Pearl ya jijini Dar es Salaam na kutoa vitu vyote nje kwa madai kwamba mmiliki wake anadaiwa kodi Dola za Marekani 380,000 ambazo ni  sawa na Sh milioni 635.9.

Tukio  hilo, limetokea jana ambapo wafanyakazi wa Majembe waliingia hotelini hapo wakiwa na gari la fuso lenye namba za usajili T389 AGG kwa ajili ya kubeba vifaa vyote.

Baadhi ya Wafanyakazi wa majembe Auction Mart wakichukua viti Hoteli ya Blue Pearl
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Saalam jana, Mkurugenzi wa Bule Pearl Hoteli, Rustam Meran alisema ameendesha hoteli hiyo kwa miaka 15, lakini kwa miaka saba aliweza kulipa kodi pango kwa mmiliki wa jengo hilo ambaye ni Ubungo Plaza Investment kwa wakati.

Meran alipewa ruhusa ya kuzungumzia sakata hilo na Wakili wa Hoteli ya Blue Pearl, Joseph Tadayo ambaye aliombwa awali kulizungumzia hilo akasema hawezi kusema wakati mteja wake yupo anaweza kufanya hivyo.

“Miaka saba ya mwanzo nililipa pango kwa wakati,  miaka saba ya mwisho niliomba baadhi ya vyumba ambavyo havijamalizika vimaliziwe kwani vimenisababishia hasara ya Dola za Marekani milioni 3.5.

“Hatukuweza kukubaliana, nilipeleka suala hilo katika Baraza la Usuluhishi, baada ya kusikilizwa nikatakiwa kulipwa kiasi hiki cha fedha, sikuweza kulipwa, kwani Blue Pearl Investment walikata rufaa Mahakama Kuu wakidai kwamba mmoja wa wasuluhishi alikuwa ni mpangaji wangu.

“Uamuzi ule ulibatilishwa, nilibakia na fedha zao kwa sababu sisi tunadai Dola za Marekani milioni 3.5, hata hivyo kabla hatujachukua hatua zozote za kukata rufaa wamekuja kutuondoa bila ya kuwa hata na amri ya mahakama.

“Mpaka sasa tumeshalipa Dola za Marekani 120,000 na tuko tayari kuendelea kuwalipa, huu uharibifu wanaofanya Blue Pearl Investment wanajiharibia mali zao wenyewe,”alidai.


Chanzo: Mtanzania