POLISI WAWILI WAUAWA KWA BOMU KARIBU NA IKULU

Mabomu mawili yamelipuka karibu na Ikulu ya Rais mjini Cairo, nchini Misri na kuwaua maafisa wawili wa polisi.

Bomu la kwanza lilimuua afisa wa polisi na kuwajeruhi wengine watatu.


Bomu la pili lililipuka maafisa wa polisi walipokuwa wanajaribu kulitegua na kumuua polisi mwingine.

Wapiganaji wa kiisilamu wanadaiwa kutega mabomu hayo katika eneo hilo wiki jana.


Shambulizi hili limetokea katika siku ya maadhimisho ya maandamano ambayo yalisababisha jeshi kumpindua aliyekuwa Rais Muhammad Morsi.


Mkuu wa ulinzi wa mjini Cairo ameambia BBC kuwa mkuu wa idara ya kutegua mabomu Generali, Alaa Abdel Zaher, alikuwa miongoni mwa wale waliojeruhiwa.


Wakati huo huo, naibu mkuu wa ulinzi amesema kuwa wataalamu wa kutegua mabomu walitegua mabomu mengine mawili yaliyopatikana nje ya ikulu yaRais. Abdul Fattah al-Sisi.


Hata hivyo ratiba ya Rais Abdul Fattah al-Sisi haikubadilishwa kutokana na mashambulizi hayo.


Mashambulizi ya mara kwa mara yamesababisha vifo vyamamia ya watu wakiwemo maafisa wa usalama tangu Morsi kuondolewa mamlakani tarehe 3 mwezi Julai.


Wapiganaji wa kiisilamu wameongeza mashambulizi katika kujibu operesheni ya kijeshi dhidi ya wanachama wa vuguvugu la Muslim Brotherhood, ambapo zaidi ya watu 1,400 wameuawa na wengine 16,000 kujeruhiwa.