CHEKA APANDISHWA KIZIMBANI

Baada ya tuhuma zakumdunda meneja wake, hatimaye bondia wa ngumi za kulipwa anayeshikilia mkanda wa WBF, Francis Cheka, amepandishwa kizimbani katika mahakama ya hakimu mkazi mkoa wa Morogoro, akikabiliwa na shtaka la shambulio la kudhuru mwili na kujeruhi.

Cheka amefikishwa kwa mara ya kwanza katika mahakama ya hakimu mkazi mkoa wa Morogoro, na kusomewa shtaka, na mwendesha mashtaka wa polisi, Aminata Mazengo, mbele ya hakimu wa mahakama hiyo Said Msuya, akidaiwa mnamo julai 02 mwaka huu, bila halali na akijua kufanya hivyo ni kosa kisheria, amempiga kwa ngumi maeneo ya kichwani na tumboni, Bahati Kabanda maarufu kama Masika, na kumsababishia maumivu makali.

Cheka anadaiwa kutenda kosa hilo kwa kabanda ambaye alikuwa ni meneja wa baa yake ya Vijana Social iliyopo sabasaba katika manispaa ya Morogoro baada ya kudaiwa kutoridhishwa na mahesabu ya mauzo, ambapo mahakama ilitoa masharti ya dhamana, ikimtaka kuwa na wadhamini wawili kwa kila mmoja kuweka dhamana ya maandishi ya shilingi milioni moja, ama aende rumande, taratibu za dhamana zilikuwa zikiendelea.