MASHAMBULIZI YAZIDI PWANI YA KENYA

Watu wasiojulikana wameteketeza nyumba saba katika eneo la kuhifadhi wanyama mjini Lamu , ingawa hakuna vifo vimeripotiwa katika shambulizi la hivi karibuni.

Washambuliaji walifanya uharibifu mkubwa kwa kuteketeza magari na ofisiTakriban familia 500 zinatoroka na kukimbilia usalama wao katika maeneo jirani ambako mashambulizi mengine mawili yalitokea mjini Lamu na katika eneo la Tana Delta na kusababisha vifo vya watu 29 mwishoni mwa wiki.

Chanzo cha familia hizi kuanza kutoroka makwao kabla hata ya kuwazika jamaa zao, ni swala linalowatia wasiwasi maafisa wakuu.

Wengi walilazimika kulala nje ya gereza la Hindi baada ya kutoroka mashamba yao.

Familia nyingi pia zimepiga kambi nje ya lango kuu la Kambi ya jeshi iliyo karibu na eneo hilo.

Wengi wanahisi kuwa salama katika kambi hizi kinyume na hali ilivyo nyumbani kwao.

Msemaji wa shirika la Red Cross,Waita Wariko, aliambia BBC kuwa watu wengi wameshuhudiwa wakihama makwao kutafuta maeneo salama.

Licha ya hali hiyo, watu hao wameombwa kurejea makwao, lakini hawana imanina polisi hususan kuhusu usalama wao.

Makamu wa Rais William Ruto, aliyezuru eneo hilo Jumapili, alitoa makataa ya saa 48 kwa maafisa wakuu wa usalama kuwasaka washambuliaji , wakiwa hai au wafu la sivyo, wafutwe kazi.

Hakuna mshukiwa hata mmoja amekamatwa mpaka sasa.

Mauaji hayo yamesemekana kuchochewa na swala tete la umliki wa mashamba na kunawasiwasi wa kutokea mashambulizi ya kulipiza kisasi kutoka kwa jamii moja ambayo watu wake wengi walishambuliwa hivi karibuni.