MBUNGE MWANAMUZIKI AUAWA KWA KUPIGWA RISASI

Mwanamuziki mashuhuri ambaye pia mbunge katika bunge la Somalia Saado Ali Warsame ameuawa kwa kupigwa risasi.


Msemaji wa kundi la wanamgambo wa kiislamu al-Shabab Abdulaziz Abu Musab aliiambia BBC kuwa mbunge huyo aliauawa kutokana na siasa zake wala sio muziki.

Mwandishi wa bbc mjini Mogadishi Mohammed Moalimu anasema kuwa mbunge huyo ni wa nne kuawa mwaka huu.


Bi Warsame alipata umaarufuwakati wa uongozi wa rais Siad Barre ambaye alipinduliwa mwaka 1991 kupitia nyimbo zake zilizokuwa zikiiushutumu uongozi wake.

Mbunge huyo aliishi kwa kipindi kirefu nchini Marekani wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe kabla ya kurejea nyumbani mwaka 2012 ili kuwakilisha ukoo wake kwenye bunge jipya nchini Somalia.

Mapema mwezi huu mbunge mwengine Ahmed Mohamud Hayd aliuawa baada ya kutoka hotelini ambapo katika tukio hilo, mlinzi wake pia aliuawa na katibu wa Bunge pia alijeruhiwa.


Kundi la Al-Shabab, ambalo lina uhusiano na al-Qaeda, limeapa kuendelea na mashambulizi zaidi katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Wanamgambo hao walipoteza ngome yao mjini Mogadishu na kuchukuliwa na Vikosi vya Umoja wa Afrika mwaka 2011,lakini wameendelea kutekeleza mashambulizi ya mabomu namauaji mjini humo.


Msemaji wa kundi hilo Abdulaziz Abu Musab amesema kuwa kundi lake limetekeleza mauaji kama ilivyopangwa na kuwa wataendelea kuwafuatilia Wabunge wengine ikiwa hawataachana na Bunge.

Al-Shabab imekua ikipigania kuunda taifa la kiislamu nchini Somalia.