MZEE MANDELA HAWEZI KUZUNGUMZA

Mke wa zamani wa Nelson Mandela, amesema rais huyo wa zamani hawezi kuzungumza, lakini anatumia uso kuwasiliana na watu.

Winnie Madikizela-Mandela alieleza kuwa Bwana Mandela, mwenye umri wa miaka 95, ni mgonjwa kweli lakini alikanusha tetesi kuwa mashini ndio inamsaidia kupumua.

Mwezi wa Septemba Bwana Mandela alirudi nyumbani baada ya kulazwa hospitali mjini Pretoria kwa karibu miezi mitatu akitibiwa ugonjwa wa mapafu.

Serikali ya Afrika Kusini imesema hali yake bado ni ya kutia wasi-wasi na wakati mwengine hubadilika.