AFARIKI AKICHEZA NGOMA ZA MATAMBIKO

MKAZI wa Kijiji cha Ifukutwa wilayani Mpanda , mkoani Katavi, Zainabu Mbaruku (70) amekufa ghafla huku akiwa anacheza ngoma ya matambiko na vikongwe wenzake wa kike kijijini humo.

Akithibitisha kutokea kwa mkasa huo Kamanda wa Polisi wa Mkoa Katavi, Dhahiri Kidavashari alisema ulitokea jana saa 12 jioni kijijini Ifukutwa , Kata ya Mpandandogo wilayani hapa ambapo kikongwe huyo alikuwa miongoni mwa vikongwe wengine waliolikwa na kikongwe mwenzao aitwaye Mwamini Luholi (70) kucheza ngoma hiyo ya matambiko nyumbani kwake.

Alisema jioni hiyo ya tukio, Mwamini alitengeneza pombe ya kienyeji kwa ajili ya matambiko ya mila na desturi za kabila la Kebende ambapo pia aliwataarifu na kuwaalika Mwenyekiti wa Kijiji hicho Steven Ismail (51), na pia ndugu, jamaa na majirani zake.

Inadaiwa ilipofika saa 11 jioni Mwamini alifika kwenye shughuli hiyo na kujumuika na wageni wengine kwa kucheza ngoma ya pamoja ambapo baada ya muda mfupi hali yake ilibadilika na kuanza kijisikia vibaya huku akitetemeka ambapo alidondoka chini.

Kwa mujibu wa Kamanda Kidavashari ilipofika saa 12 jioni kikongwe huyo alifariki dunia kutokana na hali yake kuzidi kuwa mbaya bila kupatiwa huduma yoyote ya kiafya.

"Hadi sasa chanzo kilichopelekea umauti wa kikongwe huyo hakijafahamika na uchunguzi wa kitabibu unaendelea ili kubaini sababu zilizopelekea Mwamini kufariki katika mazingira hayo," alisema Kamanda Kidavashari.

Alisema hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo na kuongeza kuwa kama itabainika kuna aliyehusika atakamatwa na kuchukulia hatua za kisheria.