24 WAFARIKI AJALI YA TRENI MISRI

Takriban watu 24 wamefariki na wengine 28 kujeruhiwa katika ajali ya treni na basi ndogo iliyohusisha magari mengine Kusini mwa mji mkuu wa Misri Cairo.

Treni iligongana na basi ilipokua inatoka mjini Bani Swaif, na kisha kugonga mahari mengine katika makutano ya njia ya reli umbali wa kilomita 40 kutoka mji mkuu Cairo.

Taarifa za vyombo vya habari nchini humo zilisema kuwa wengi wa waliofariki walikuwa jamaa wa familia moja waliokuwa wanarejea kutoka harusini.

Ajali hiyo ilitokea karibu na kijiji cha Dahshur Jumatatu asubuhi huku taarifa zikisema kuwa ajali hiyo pia ilihusisha basi ndogo na magari mengine.

Maafisa wakuu walisema kuwa milango ya magari kuvukia njia ya reli ilikuwa imefungwa lakini dereva wa treni alishangazwa kuona magari yakipita kwenye njia hiyo.

Magari ya kuwabeba wagonjwa ya Ambulance, yaliwasili katika eneo la tukio kuwabeba waliojeruhiwa.

Taarifa zinasema kuna hofu kuwa idadi ya waliojeruhiwa huenda ikaongezeka.

Mnamo mwezi Januari, treni iliyokuwa imewabeba makurutu wa jeshi, ilianguka na kusababisha vifo vya watu 19 na kuwajeruhi zaidi ya 100.

Novemba mwaka jana watoto 50 walifariki wakati treni ilipogonga basi yao ya shule.

Waziri wa usafiri alijiuzulu baada ya ajali hiyo.

Ajali mbaya zaidi ya gari moshi kuwahi kutokea Misri, ilishuhudiwa mwaka 2002, ambapo treni ilishika moto na kuwaua watu 373