MWASISI WA CHADEMA MZEE MTEI ANENA JUU YA YANAYOENDELEA NDANI YA CHADEMA

Mwasisi wa Chadema, Edwin Mtei amesema kuna baadhi ya watu nchini wanakesha usiku na mchana kuhakikisha wanafanya njama za kukidhoofisha na hata kukipoteza kabisa chama hicho kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Mtei,alitoa kauli hiyo wakati chama hicho kikiwa katika wakati mgumu baada ya baadhi ya viongozi wake kushambuliana kupitia mitandao ya kijamii, huku aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema mkoani Arusha, Samson Mwigamba akisimamishwa kwa madai ya kukiuka kanuni za chama hicho.

Mtei alisema kuna baadhi ya watu kutoka Chama Tawala cha CCM wanahakikisha wanatengeneza mifarakano kila kukicha ili kukivuruga Chadema.

Alisema mara baada ya Rais Jakaya Kikwete kutoa kauli kuwa huenda CCM ikang'oka mwaka 2015, baadhi ya makada na viongozi wameanza kukesha wakifanya mbinu ya kukivuruga ili Chadema kisishike dola.

"Kuna watu wa CCM wanakesha usiku na mchana kuhakikisha wanatuvuruga, ili tusishike dola mimi nasema hawatuwezi" alisema Mtei Hata hivyo, alisema kitendo cha kusimamishwa na hata kufukuzwa baadhi ya makada wa Chadema kimetokana na usaliti ndani ya chama hicho huku wengine wakikubali kutumiwa na CCM.