WANAJESHI WA JWTZ WALIOKUWA LIKIZO WAITWA MAKAMBINI

Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limesitisha wapiganaji wake kwenda likizo na kuwaita waliokuwa likizo kurudi makambini. Kwa mujibu wa vyanzo vya ndani kabisa vya kiinteligensia vijulikanavyo kama'KAINZI'uamuzi huo umeenda sambamba na kuweka hali ya utayari wa kijeshi (military readiness) kufikia asilimia 50; katika hali ya utulivu na amani nchini hali ya utayari wa kijeshi inakuwa kwenye asilimia 25 hivi.

Kwa mujibu wa chanzo changu hicho ambacho kimekuwa kikifuatilia mwitikio wa vyombo vyetu vya usalama kufuatia kuongezeka kwa hali ya utete katika eneo la maziwa mazuri vikosi vya jeshi nchini kufikia jana vilikuwa vimesomewa taarifa hiyo ya kusitisha likizo na hata pasi za kutoka makambani huku maafisa wake ambao walikuwa nje ya vituo vyao vya kazi wakitakiwa kurudi makambini. Uamuzi huu hata hivyo haijawa wazi kama unahusu wapiganaji wote nchini au wa Brigedia za Tabora au Brigedia za vikosi maalum.
Baadhi ya vikosi vilisomewa taarifa hiyo jana.


Kwa mujibu wa chanzo hicho cha kuaminika Brigedia za Tembo na Kifaru (Tabora) tayari zimepewa maagizo ya kuwa katika hali ya utayari endapo watahitajika kufanya'movement'yoyote ya kijeshi."Unajua tangu sakata la Rwanda vyombo vyetu vya usalama na inteligensia vimeona kuwa kuna sababu ya msingi ya kujiweka katika hali ya utayari wa kijeshi"kilisema chanzo hicho. Akizidi kufafanua mtoa habari huyo amemdokeza mwandishi kuwa japo jambo hili limetokea wakati huu wa utete hata hivyo ni kawaida pia kwa jeshi kujiweka katika hali ya mazoezi wakiigiza hali ya kivita (war simulation) na hivyo watu wasije wakasoma mengi katika hili.

Nilipojaribu kufuatilia zaidi na kwa kina habari hizi inaonekana kuwa kuna taarifa za kiusalama ambazo pia zinasababisha uamuzi huu kuchukuliwa.

Pamoja na uamuzi huu habari hizi zinadokeza pia kuwa JWTZ linaweza kuwaita baadhi ya reserve ili kuliongezea nguvu. Kwa kawaida kama ilivyokuwa kabla ya Vita ya Kagera baadhi ya maafisa wanaoweza kuongeza nguvu jeshini ni pamoja na wale kutoka vyombo vingine vya usalama kama Polisi, Mgambo, Magereza, n.k ambavyo vinaweza kutakiwa kutoa idadi fulani ya watu kujiunga na JWTZ.


Wakati wa Vita ya Kagera kuongeza nguvu jeshi kulilipatia jeshi nguvu ya kufikia watu 100,000 ndani ya wiki chache tu na hivyo kulifanya kuwa miongoni mwa majeshi makubwa ya wakati huo katika Afrika. Pamoja na kujipatia watu kutoka vyombo vingine JWTZ pia linaweza kufungua milango yake kwa watu wanaojitolea kujiunga (volunteers).

Pamoja na maamuzi hiyo vyanzo vyetu vinataarifu kuwa hata wapiganaji wa JWTZ ambao walikuwa wanaandaliwa kwenye shughuli mbalimbali za kulinda amani nao wamesitishwa sasa hivi na wanapelekwa kwenye moja ya mikoa iliyoko mpakani kwa sababu ambazo mtoa habari wetu hakutaka kuziweka wazi mara moja.

Hata hivyo hadi hivi sasa hakuna uhamishaji wa vifaa na zana za kijeshi kuelekea maeneo yenye migogoro. Tutaendelea kuwaletea taarifa mpya kwa kadiri tukavyozipata.

Source: Jamii Forum