POLISI WAWILI WASHIKWA NA RISASI 3000

Polisi wawili wa
Musoma, Mkoa wa Mara
na Kibaha, Pwani
wanashikiliwa kwa
tuhuma za kukutwa
wakisafirisha risasi 3,000
kutoka Musoma kwenda
Dar es Salaam.

Wanaoshikiliwa kwa
tuhuma hizo ni aliyekuwa
mtunza chumba cha silaha
Kikosi cha FFU Musoma
na mwenzake mwenye
cheo cha Koplo Wilaya ya
Kibaha, Pwani. Inadaiwa
walikamatwa Juni 2,
mwaka huu saa 11:00
alfajiri.

Watuhumiwa
wanashikiliwa Kituo cha
Polisi Musoma na
wamefunguliwa jalada
MUS/RB/2465/013 wizi wa
risasi 1,056, wanasubiri
taratibu zingine za polisi.

Habari zinadai shehena
hiyo ilisafirishwa kwa
kutumia pikipiki hadi
Kituo cha Mabasi, lakini
polisi tayari walikuwa
wameweka mtego baada
ya kupata taarifa kuhusu
wizi huo.

Taarifa kutoka vyanzo
mbalimbali ikiwamo
wahusika wa basi na
nyumba moja ya kulala
wageni iliyopo jirani na
stendi, baadhi ya askari
waliovaa kiraia
walionekana maeneo hayo
mapema.

Kwa mujibu wa habari za
uhakika kutoka ndani ya
polisi, Koplo huyo
alikutwa na shehena hiyo
karibu na kituo cha
mabasi ya Kampuni ya
Mohammed Trans,
akijiandaa kuelekea Dar es
Salaam ambako
inasemekana wana wateja
wao.

Inadaiwa koplo huyo
aliomba ruhusa ya
ugonjwa kazini kwake na
kuitumia kusafiri hadi
Musoma kuchukua mzigo
huo, inadaiwa biashara
yao hiyo ni ya muda
mrefu na wana mtandao
na watuwanaojihusisha na
uhalifu.

Mtandao huo unadaiwa
kuwagusa baadhi ya polisi
Mkoa wa Tarime na
Rorya, ambao huwauzia
watu wanaojihusisha na
uhalifu wa kutumia silaha.

Kamanda wa Polisi Mkoa
wa Mara, Absalom
Mwakyoma alipotafutwa
kwa simu zake za
mkononi licha ya kuitwa,
hazikupokewa.

Hata hivyo, aliomba
atumiwe ujumbe, licha ya
kupelekewa huo ujumbe,
hakujibu ingawa taarifa
zinadai ameanza likizo ya
kustaafu hivi karibuni.
Mkuu wa Upelelezi Mkoa
wa Mara, Jafari
Mohammed alipoulizwa
kuhusu tukio hilo,
alikanusha kufahamu
suala hilo huku akigeuka
kuwa mkali kwa
mwandishi.

"Hilo mimi silijui, nani
kakwambia wewe… askari
kukutwa na risasi mfukoni
ni jambo la kawaida
huenda ni uzembe
tunamshughulikia kwa
uzembe," alisema.

Chanzo:Mwananchi