WALIOKUWA WAMEHUKUMIWA KESI YA EPA WAACHIWA HURU

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam imewaachia huru wafanyabiashara watatu, wakiwemo mume na mke, waliokuwa wamehukumiwa kifungocha miaka 13 na miezi sita jela kwasababu ya wizi wa Sh bilioni 1.1 katika Akaunti ya Madeni ya Nje ya(EPA) ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Walioachiwa huru ni mume Manase Makale na mkewe Edda Makale, na mfanyabiashara mwingine Bahati Mahenge.

Washitakiwa hao waliachiwa mwisho wa wiki iliyopita baada ya Jaji Augustine Shangwa kukubali rufaa iliyowasilishwa na wafanyabiashara hao kupinga hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mwaka jana.

Akisoma hukumu hiyo, Jaji Shangwa alisema anawaachia huru wafanyabiashara hao kwa kuwa upande wa Jamhuri ulishindwa kabisa kuthibitisha mashitaka dhidiyao.

Aliamuru wafanyabiashara hao waachiwe huru mara moja na kutengua amri ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu iliyowataka warejeshe fedha hizo mara baada ya kutumikia kifungo.

Katika rufaa, wafanyabiashara walikuwa wakipinga hukumu iliyotolewa na jopo la mahakimu Sekela Mushi, Sam Rumanyika na Lameck Mlacha, wakidai kuwa kulikuwepo na upungufu mkubwa wa kisheria na kihoja katika kuwatia hatiani.

Katika hukumu iliyotolewa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mahenge alitakiwa kutumikia kifungo cha miaka saba jela, Makale kifungo cha miaka mitano jela na mkewe Edda kifungo cha mwaka mmoja na nusu.

Aidha, mahakama iliamuru baada ya kutumikia adhabu hiyo, Mahenge na Makale warejeshe kiasi cha Sh bilioni 1.18 walichodaiwa kukiiba katika akauntiya EPA.

Washitakiwa walikuwa wanakabiliwa na mashitaka ya kula njama ya kutenda kosa, kughushi nyaraka mbalimbali na kuziwasilisha sehemu husika na kuiba fedha hizo.

Katika kesi hiyo, wafanyabiashara hao walikuwa wameshitakiwa na wenzao Davis Kamungu na GodfreyMushi ambao waliachiwa huru katika Mahakama ya Kisutu kwa kuwa upande wa Jamhuri ulishindwa kuthibitisha mashitaka dhidi yao bila kuacha shaka.