RAIS KIKWETE AFANYIWA UPASUAJI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais Kikwete afanyiwa upasuaji wa tezi dume

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete alfajiri ya jana, Jumamosi, Novemba 8, 2014, alifanyiwa upasuaji wa tezi dume (prostrate) katika Hospitali ya Johns Hopkins iliyoko Baltimore, Jimbo la Maryland, Marekani.

Rais Kikwete amefanyiwa upasuaji huo baada ya madaktari waliomfanyia uchunguzi wa afya yake kujiridhisha kuwa Rais alikuwa anahitaji matibabu ya aina hiyo.

Upasuaji huo uliofanyika alfajiri na kuchukua kiasi cha saa moja unusu, umefanyika salama na kwa mafanikio makubwa. Hali ya Mheshimiwa Rais Kikwete inaendelea vizuri, bado yuko wodini akiendelea kuwa chini ya uangalizi wa madaktari na kupatiwa tiba.

Wananchi wataendelea kupewa taarifa sahihi kuhusu hali ya Rais Kikwete kwa kadri zitakavyokuwa zinapatikana.
 
Mwisho.

Imetolewa na;
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
09 Novemba,2014