MAREKANI YAENDELEZA MASHAMBULIZI IRAQ

Marekani imesema kuwa imetekeleza mashambulizi zaidi kazkazini mwa Iraq dhidiya maeneo yanayodhibitiwa na wapiganaji wa Jihad.

Taarifa kutoka Pentagon imesema kuwa ndege za Marekani pamoja na zile zisizo na rubani ziliharibu magari ya kijeshi ya wanamgambo hao likiwemo lile lilokuwa likiwashambulia raia wa Yazidi ambao wamekimbilia hifadhi katika mlima Sinjar.

Awali Rais Obama amesema kuwa kupitia washirika wake wa ulaya pamoja na wanajeshi wa Iraq watawakabili wanamgambo ambao wameuzunguka mlima huo.

Hata hivyo ameonya kuwa kampeni hiyo ya kijeshi itachukua miezi kadhaa na kwamba itachukua mda kwa jeshi la Iraq kujikusanya ili kutoa upinzani mkali dhidi ya wanamgambo hao.

Wakati huohuo Ndege za kijeshi za Marekani na zile za Uingereza zimeendelea kuangusha misaada kwa raia waliokwama katika Mlima Sinjar nchini Iraq,ijapokuwa viongozi wa mataifa hayo mawili wamekubaliana kwamba hatua hiyo sio suluhu ya kudumu.

Wamesema kuwa lazima njia ya kuwaondoa raia hao hadi katika eneo lililo salama itafutwe ili kuzuia mauaji ya kimbari.

Mfanyikazi mmoja wa shirika la Amnesty International kazkazini mwa Iraq, Donatella Rovera ameiambia BBC kwamba maelfu ya raia kazkazini na magharibi mwa mlima huo wamefanikiwa kutoroka, lakini wengi zaidi katika eneo la kusini la mlimahuo hawana mahala pa kwenda.

Amesema kuwa wale waliotoroka wako katika hali mbaya baada ya kukaa siku sita bila chakula na maji kidogo.