HAKUNA MGONJWA WA EBOLA TANZANIA

Tanzania imesema haina mgonjwa aliyethibitishwa kuwa na ugonjwa wa Ebola.

Kauli hiyo inakuja baada ya kufanyiwa uchunguzi kwa wagonjwa wawili waliotiliwa shaka kuwa na ugonjwa huo.

Waziri wa Afya wa Tanzania Seif Rashid ameiambia BBC, wagonjwa hao waliohisiwa kupata maambukizo kutokana na dalili za awali, ni wa kutoka Benin na Mtanzania, lakini vipimo vimeonesha hawana maambukizo hayo.

Amesema tayari eneo maalumu limetengwa kwa ajili ya kufanyia uchunguzi wagonjwa wanaotiliwa shaka kuwa na ugonjwa huo.

Mafunzo yametolewa pia kwa wataalamu watakao hudumia wagonjwa iwapo watatokea.

Vifaa maalumu vitakavyotumiwa na watoa huduma katika kuhudumia wagonjwa, vimewekwa pia.

Wizara ya Afya ya Tanzania inaongeza uwezo wa kufanya uchunguzi, katika Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere, ambao wasafiri wengi kutoka nje huutumia.