WANAJESHI SABA WA TANZANIA WAUWAWA SUDAN

Wanajeshi saba wa Tanzania,
ambao ni miongoni mwa kikosi
cha Umoja wa Mataifa, cha kulinda
amani katika jimbo la Darfur
nchini Sudan, wanadaiwa kuwa
wameuawa.


Taarifa zilizotufikia jana zilisema
kwamba wanajeshi hao wa
Tanzania, wamekufa kutokana na
mashambulizi yaliyofanywa na
waasi wanaopigana na Serikali.


Kwa mujibu wa taarifa hizo, miili
yao wanajeshi hao bado ipo nchini
Sudan ikisubiri taratibu za
kusafirishwa kuletwa nchini.


Hii ni mara ya kwanza kuripotiwa
kwa idadi kubwa ya wanajeshi wa
Tanzania wanaolinda amani katika
nchi mbalimbali kufa kwa wakati
mmoja.


Agosti mwaka jana wanajeshi
watatu wa Tanzania huko Darfur
waliripotiwa kuuawa kwenye
tukio kama hilo.


Msemaji wa Jeshi la Ulinzi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ,
Kanali Kapambala Mgawe
alipoulizwa kwa njia ya simu
kuhusu vifo vya wanajeshi wa
Tanzania huko Darfur, alisema
kuwa naye amesikia, lakini hana
taarifa rasmi kwa mujibu wa
taratibu za kiofisi.


Hii ni mara ya pili kwa wanajeshi
wa Tanzania kuuawa katika Jimbo
la Darfur, ambapo Agosti mwaka
jana, Kanali Mgawe alinukuliwa na
vyombo vya habari akithibitisha
kutokea kwa vifo vya askari
watatu ambao gari lao lilizolewa
na maji walipokuwa wakivuka
mto uliokuwa umefurika maji.


Kanali Mgawe aliwataja askari hao
kuwa ni Sajini Julius Chacha, Sajini
Anthony Daniel na Koplo Yusuph
Said na kwamba askari wengine
walinusurika baada ya kuogolea.


Tanzania ina askari 850 kwenye
kikosi cha Umoja wa Mataifa cha
Kulinda Amani jimbo la Darfur,
ambao ni sehemu ya askari 1,081
wa kulinda amani katika jimbo la
Darfur.


Wanajeshi hao wa Tanzania
wametawanywa kwenye miji ya
Khor Abeche na Muhajeria kusini
mwa Darfur.


Aprili mwaka huu Tanzania
ilipeleka wanajeshi wa kulinda
amani katika Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Congo (DRC),
kupambana na kikundi cha waasi
wa nchi hiyo M23 kinachopigana
kuiangusha serikali ya DRC.


Majeshi ya Tanzania yalipelekwa
kulinda amani chini ya Umoja wa
Mataifa. Tanzania inaungana na
nchi za Afrika Kusini na Malawi
kukamilisha kikosi cha wanajeshi
3,000. Tanzania imepeleka
wanajeshi 850.


"Tanzania imekuwa ikijihusisha na
misheni za amani, mafunzo na
ushauri kwa nchi nyingi,"
alinukuliwa Kanali Mgawe, na
kueleza kuwa majeshi ya Tanzania
yamekuweko katika vikosi vya
kulinda amani huko Lebanon,
Darfur, Sudan Kusini, Visiwa vya
Comoro na Liberia. Liberia
waliuawa wanajeshi wa Tanzania
11.


"Tanzania daima haiendi kwa nchi
yeyote bila ya kuombwa na nchi
hiyo au kutoka Umoja wa
Mataifa," alisema.