MUUZA CHIPS ATUNUKIWA NISHANI NA RAIS KIKWETE

MUUZA chipsi wa Dar es Salaam, Kassim Said (28), alivuta hisia za waalikwa na viongozi mbalimbali akiwemo Rais Jakaya Kikwete, juzi jioni kwenye sherehe za kutunuku nishani, baada ya kupewa Nishani yaUshupavu, aliouonesha baada ya kumpiga jambazi kwa chepe na kufanikisha kukamatwa kwake.Sherehe za kutunuku nishani hizo zilifanywa juzi katika viwanja vya Ikulu, jijini Dar es Salaam ambapo Rais Kikwete aliwatunuku nishani viongozi na raia 28, walio hai na wafu, ambao katika uhai wao walikuwa na sifa zinazokidhi matakwa ya nishani husika.Nishani ya Ushupavu aliyopewa Kassim, hutolewa kwa maofisa wa majeshi ya ulinzi na usalama na watu wengineo kwa vitendo vya ushupavu walivyoonesha, ambapo Kassim yeye alionesha ujasiri wa kumpiga jambazi kwa chepe, kisha kuzirai na kurahisisha kukamatwa kwake.

Akisimulia tukio hilo, mara baada ya kuvalishwa nishani hiyo na Rais, Kassim alisema anakumbuka ilikuwaJulai 7, mwaka jana saa 3 usiku eneo la Buguruni Malapa, ambapo akiwa kwenye eneo lake la kazi ya kuuza chipsi kama mwajiriwa, alikuja jambazi huyo na kujidai ni mteja.

Baada ya muda jambazi huyo alitoa silaha na kuanza kutishia wateja na baadhi ya wateja walikimbia huku na huko, huku bosi wake akitishiwa kwa silaha kichwani, ndipo akapata wazo la kuchukua chepe na kumpiga nalo mara mbili kichwani na ndipo jambazi huyo akaanguka na kupoteza fahamu.

Tukio hilo lilisababisha iwe rahisi kuchukua silaha aliyokuwa nayo na kisha polisi walifika na kuondoka na mtuhumiwa na kijana huyo kwenda kutoa maelezo Polisi ya jinsi alivyofanikisha tukio hilo, lisilete madhara makubwa.

"Niliwaza sasa kama huyo jambazi atachukua na hizo hela, ina maana mimi leo sitapata kitu, ujira wenyewe ni mdogo halafu niukose, nikaona njia pekee ni kumdhibiti huyo jambazi ili asilete madhara zaidi, na kweli nilifanikiwa", alisema Kassim.

Katika hatua nyingine, watunukiwa 27 walipokea nishani zao, ambapo baadhi yao ni marehemu ambao waliwakilishwa na ndugu na jamaa zao.

Katika nishani hizo, Waziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Samuel Sitta, alikuwa miongoni mwa watunukiwa wa Nishani ya Kumbukumbu ya Miaka 50, ya Muungano Daraja la Pili.