KABILA AINGIZA WAPINZANI SERIKALINI

Rais wa Jamhuri ya kidemokrasi ya Congo, Joseph Kabila amebuni serikali ya Muungano ambayo inajumuisha viongozi kadhaa wa upinzani.

Afisaa mkuu wa chama cha upinzani cha '' Movement for the Liberation of Congo'' ametajwa kama naibu waziri mkuu.

Viongozi wengine wa zamani wa upinzani pia wamepewa nyadhifa katika serikali hio.

Serikali hio ya Muungano, imebuniwa huku kukiwa na wasiwasi kuwa Bwana Kabila, ambaye amekuwa mamlakani tangu mwaka 2001, anaweza kujaribu kubadilisha katiba ili awanie muhula wa tatu.

Wadadisi wanasema kuwa kujumuishwa kwa wapinzani katika serikali ya muungano inawezekana ni njama ya kuongeza ufuasi wake na kudidimiza upinzani.

Wanaongeza kuwa hatua ya Kabilani ya kujiandaa kwa mageuzi ya kikatiba au hata kuchelewesha uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwaka 2016.

Evariste Boshab, kiongozi wa chama cha (People's Party for Reconstruction and Democracy), pia ametajwa kama naibu waziri mkuu.