AUWAWA KWA WIZI WA KUKU WATATU

MTU mmoja ambaye hajatambuliwa jina lake na pia anakoishi, amekutwa amekufa baada ya kushambuliwa na watu wenye hasira baada ya kushutumiwa kuiba kuku watatu, ambao tayari alikuwa amewachinja huko Dunga vilima viwili wilaya ya Kati Unguja.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kusini Unguja, Juma Sadi Khamis alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Alisema juzi Polisi walipigiwa simu na kupewa taarifa kwamba yupo kijana amejeruhumiwa vibaya na watu wenye hasira kwa tuhuma ya wizi wa kuku watatu.

Alisema Polisi walipofika katika eneo la tukio, walimkuta kijana huyo akiwa amejeruhiwa vibaya, akiwa na kuku watatu waliochinjwa, ambao kwa mujibu wa maelezo ya watu wanaoishi eneo hilo, wameibwa.

"Ni kweli tumepata taarifa ya kijana mmoja anayekisiwa kati ya umri wa miaka 25 ameiba kuku na tulipofika alikuwa katika hali mbaya huku akiwa amekatwa viganja vyake viwilivya miguu yote na tulipomfikisha katika hospitali ya Mnazi Mmoja alifariki muda mfupi," alisema Sadi.

Sadi alisema Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi, kujua chanzo cha tukio hilo na mazingira ya kifo chake na wapi aliiba kuku hao.

"Jeshi la Polisi mkoa wa Kusini linafuatilia zaidi tukio hilo kujua chanzo na mazingira ya kifo cha kijana huyo pamoja na kuwatafuta ndugu wa marehemu," alisema.